Image

Ugonjwa wa Moyo Unaosababishwa na Simanzi/Kuachana na Mpenzi Wako

Ugonjwa wa moyo unaosababishwa na simanzi au kuachana na mpenzi/mwenza wako yoyote yule hujulikana kitaalamu kama Takostubo au broken heart syndrome.

Ugonjwa huu husababishwa na kudhoofika ghafla kwa misuli ya moyo kwa muda mfupi na hauuhusiani na tatizo la kukosekana kwa damu ya kutosha katika moyo.Tatizo hili hujulikana kama broken heart syndrome kwa sababu hutokana na mtu;

  • Kufiwa na mpenzi/mwenza wake
  • Kuachana na mpenzi/mwenza wake
  • Kuwa na wasiwasi mara kwa mara kwa muda mrefu

Vilevile tatizo hili huweza kupelekea moyo kushindwa kufanya kazi  ghafla (Acute heart failure), moyo kupiga bila mpangilio usio wa kawaida (lethal ventricular arrhythmia) .

Dalili

  • Maumivu makali ya kifua
  • Matatizo ya upumuaji au kuhema kwa shida
  • Uchovu
  • Mapigo ya moyo yasiyo na mpangilio

Je tatizo hili husababishwa na nini?

Tatizo hili huweza kusababishwa na mambo yafuatayo:

  • Habari ya kufiwa na mpenzi wako
  • Kutambua unaugua ugonjwa sugu kama vile saratani
  • Kupoteza hela nyingi
  • Sherehe ya kushtukiza (surprise parties)
  • Kutakiwa kuongea hadharani
  • Ukiwa na matatizo kama ugonjwa wa pumu, maambukizi, ajali ya gari au baada ya upasuaji mkubwa.

Vipimo

  • ECG
  • X-ray ya kifua
  • Echocardiogram
  • MRI  
  • CAG
  • Kipimo cha damu kuangalia vimeng’enyo vya kwenye moyo
  • Ni muhimu kutofautisha na Shambulizi la moyo na hili tatizo

Matibabu

Hakuna tiba ya madawa iliyo maalum kwa ajili ya kutibu tatizo hili pekee. Matibabu yake yanaweza kufanana na matibabu ya shambulio la moyo, na mgonjwa anaweza kuhitaji kulazwa hospitali kwa muda ingawa si mara zote huwa hivyo.

Daktari akishathibitisha kuwa chanzo cha dalili zako ni broken heart syndrome na wala si shambulio la moyo anaweza kukupatia dawa kama vile zilizo katika kundi la angiotensin-converting enzyme (ACE) inhibitors mfano Benazapril, kundi la beta blockers kwa mfano carvedilol au kundi la diuretics kama vile frusemide (lasix). Dawa hizi husaidia kupunguza mzigo katika moyo na pia kuzuia usipate shambulio jipya. 

Kwa kawaida wagonjwa wengi hupata nafuu baada ya muda wa kama mwezi mmoja au miwili hivi. Hata hivyo ni vema kumuuliza daktari wako unapaswa kutumia dawa kwa muda gani. 

Kinga

Kuna uwezekano mkubwa sana wa hali hii kujirudia tena mara baada ya shambulio la kwanza. Mpaka sasa hakuna dawa zilizothibitishwa zinazoweza kusaidia kuzuia hali hii isijitokeze tena, ingawa baadhi ya madaktari wanashauri matumizi ya muda mrefu ya dawa zakundi la beta blockers kama vile atenolol, carvedilol, au dawa zenye kuzuia uzalishaji wa homoni zenye kuchochea shinikizo katika moyo.

Pamoja na matumizi ya dawa, ushauri nasaha pamoja na kubadili mfumo wako wa maisha ni mambo ya muhimu zaidi kusaidia kukukinga na tatizo hili. 

 

Imesomwa mara 39997 Imehaririwa Jumatatu, 16 Julai 2018 09:19
Dr.Mayala

Dr.Henry A Mayala ni daktari bingwa Wa Tiba ya moyo katika taasisi ya Jakaya Kikwete Cardiac Institute (JKCI), ambaye kwasasa anasomea shahada ya uzamivu (PhD) ya Tiba ya Moyo katika Chuo Kikuu cha Tongji  nchini China.

Anwani ya barua pepe hii inalindwa kutokana na spambots. JavaScript lazima iwe itawezeshwa kwa kuweza kuona.

Makala shabihana