Image

Dalili, tiba na kinga ya ugonjwa wa maambukizi ya njia ya mkojo - UTI

Maambukizi ya njia ya mkojo (UTI) husababishwa na vimelea kitaalamu hujulikana E. Coli. Vimelea hawa huishi huishi kwenye mfumo wa chakula bila kuleta madhara yoyote wawapo humo, ila wakiingia kwenye njia ya mkojo huleta maambukizi na kusababishwa ugonjwa wa UTI.

Kutokana na sababu za kimaumbile, Wanawake huathirika zaidi na ugonjwa wa UTI kuliko wanamume, hii ni kwa kwasababu kuna ukaribu zaidi katika njia hizi mbili za chakula na mkojo. Na pale mtu anaponawa baada ya haja kubwa ni rahisi zaidi kuhamisha vimelea hivi vya E. Coli  kwenye njia ya mkojo pale ambapo hujifuta kuelekea mbele.  Na ndiyo sababu, kwa wanawake, hushauriwa kunawa kuanzia mbele kuja nyuma. Endapo utanawa kuanzia nyuma kuja mbele, kuna uwezekano wa kuhamisha vimelea hivi ambavyo husambaa hadi kwenye kibofu, na endapo hautotibiwa vyema, basi hupanda hadi kwenye figo.

Pia, Wanawake huathiriwa sana na UTI kwa sababu wana njia fupi ya mirija ya mkojo (urethra) ambayo, inawapa bakteria wa UTI urahisi wa kusafiri hadi kwenye kibofu cha mkojo. Kujamiiana pia kunaweza kunaweza kupelekea kupata bakteria wanaosababisha UTI. Matumizi ya vipandikizi vya kuzuia mimba vinavyowekwa kwenye shingo ya uzazi huongeza hatari ya kupata UTI. Magonjwa kama kisukari na matatizo ya kimaumbile katika mfumo wa mkojo huongeza asilimia za kupata UTI.

Dalili za maambukizi ya njia ya mkojo

  • Maumivu wakati wa haja ndogo, na hisia ya mkojo kuchoma choma
  • Kubanwa na mkojo mara kwa mara
  • Maumivu ya kiuno na maumivu ya chini ya kitovu
  • Mkojo wa njano sana, na muda mwingine unatoa harufu
  • Uchovu
  • Homa
  • Kuna baadhi ya watu hawawi na dalili yoyote (asymptomatic bacteriuria)
  • Kukosa hamu ya kula,Kichefuchefu na kutapika.

..

Unapohisi dalili hizi ni vyema kwenda kwa daktari ili upate tiba muafaka badala ya kuanza kutumia madawa bila ya mpangilio maalumu kitu kitakachoweza kukusababishia kukomaza ugonjwa. Pia, kuna baadhi ya dalili za UTI hufanana na zile za magonjwa ya zinaa (chlamydia, gonorrhea, and trichomoniasis), hivyo, vipimo vya maabara huitajika kuweza kutambua kama unachoumwa ni UTI au ni magonjwa ya zinaa (STD)

Vipimo:

  • Kupima mkojo kuangalia kama kuna chembe chembe nyeupe,na vimelea ambacho ni kiashirio cha maambukizi
  • Kuotesha mkojo kuangalia vimelea
  • Ultrasound ya tumbo chini ya kitovu kuangalia njia ya mkojo na hasa kibofu

Jinsi ya kujikinga na maambukizi ya njia ya mkojo

  • Kunywa maji mengi
  • Baada ya haja kubwa ni vizuri kunawa kuanzia mbele kurudi nyuma
  • Pendelea kwenda kukojoa pindi unapojisikia umeshikwa na mkojo. Na hakikisha umetoa mkojo wote.
  • Hakikisha sehemu za siri zipo safi kabla ya kujamiana
  • Ni vizuri kupata haja ndogo mara baada ya kujamiana ili kusafisha bakteria ambao wanaweza kuwepo kwenye njia ya mkojo,
  • Tumia juisi ya Cranberry ina vitu kitaalamu Vitamins and antioxidants ambavyo husaidia kuzia (siyo kutibu) maambukizi haya.
  • Hakikisha sehemu za siri zipo kavu, pendelea kuvaa nguo za ndani zilizotengenezwa kwa pamba, pia zenye kuacha unafasi (loose-fitting), epuka jinsi zinazobana au nguo za ndani za unailoni kwa sababu zitapelekea kuwa na hali ya unyevunyevu na kuleta mazingira rafiki kwa ukuaji wa bakteria.
  • epuka matumizi ya vipandikizi vinavyowekwa kwenye njia ya uzazi vinavyotumia dawa za kuuwa shahawa kuzuia mimba

UTI kwa wajawazito

Wanawake wajawazito wapo kwenye hatari kupatwa na ugonjwa wa UTI. Homoni wakati wa ujauzito hupelekea kutokea mabadiliko kwenye njia ya mkojo. Pia, uterus huongeza mgandamizo kwenye mishipa inayopitisha mkojo kutoka kwenye kibofu (ureter) na kibofu chenyewe, hali hii husababisha mkojo kupita kwa shida kutoka kwenye figo kuja kwnye kibofu au kutoka kwenye kibofu chenyewe. UTI isiyotibiwa huweza kuleta athari kwa mjamzito ikiwemo preterm labor.

UTI kwa watoto wadogo

Watoto wadogo, pia wanaweza kupata ugonjwa wa UTI ingawa mara nyingi ni ngumu kwa mzazi kutambua kwa sababu ni ngumu kujieleza. Mara nyingi unaweza kuona dalili zifuatazo

  • Homa
  • Harufu tofauti ya mkojo
  • Kukataa vyakula au kutapika
  • Kusumbuasumbua (Fussy behaviour)

Unashauriwa kumpelekea hospitali kwa ajili ya matibabu punde unapohisi ana UIT ili kuzuia athari Zaidi. Pia, kubadilisha nepi kunasaidia kupunguza uwezekano wa maambukizi. Kumbuka, kumsafisha kutokea mbele kuja nyuma wakati unambadilisha nepi na kumsafisha.

Hatari za UTI

Hatari kubwa ya kukaa na UTI ni kuwa, bakteria wanaweza kusambaa hadi kutoka kwenye kibofu hadi kwenye figo. Bakteria hawa huweza kuathiri ufanyaji kazi wa figo kitu ambacho ni cha hatari haswa kwa watu wenye matatizo ya figo. Pia, kuna uwezekano mdogo wa bakteria hawa kuingia kwenye mfumo wa damu, endapo hatua hii itatokea, basi huweza kusababisha kuthirika kwa viungo vingine. Hatari kwa mama mjamzito kupata maambukizi ya njia ya mkojo huweza kupelekea kujifungua kabla ya wakati, au kujifungua mtoto mwenye uzito mdogo.

Kama una maswali kuhusiana na ugonjwa wa UTI, usisite kuacha maoni hapo chini.

Imesomwa mara 82552 Imehaririwa Jumatatu, 27 Machi 2023 16:35
Dr.Mayala

Dr.Henry A Mayala ni daktari bingwa Wa Tiba ya moyo katika taasisi ya Jakaya Kikwete Cardiac Institute (JKCI), ambaye kwasasa anasomea shahada ya uzamivu (PhD) ya Tiba ya Moyo katika Chuo Kikuu cha Tongji  nchini China.

Anwani ya barua pepe hii inalindwa kutokana na spambots. JavaScript lazima iwe itawezeshwa kwa kuweza kuona.