Image

Ni moja kati ya magonjwa sugu ambayo sio ambukizi kutoka kwa mtu mmoja kwenda kwa mtu mwingine. Vilevile ni kati ya magonjwa ambayo ni endelevu.

Kuna magonjwa makuu manne yasiyo ambukizi

  • Magonjwa ya moyo na mishipa ya damu-shambulizi la moyo na kiharusi
  • Kansa au saratani
  • Kisukari
  • Magonjwa sugu yasababishayo kuziba mfumo wa upumuaji kitaalamu COPD’s

Kulingana na taarifa za shirika la afya duniani

  • Watu milioni 36 kila mwaka huathiriwa na magonjwa yasiyo ambukizi
  • Karibu asilimia 80 sawa na watu milioni 29 hufa kutokana na magonjwa yasiyo ambukizi katika nchi za vipato vidogo na vya kati.
  • Magonjwa ya moyo na mishipa ya damu ndio husababisha vifo zaidi watu milioni 17 kwa mwaka, ikifuatiwa na kansa watu milioni 7, mfumo wa upumuaji watu milioni 4, na kisukari milioni 1.
  • Magonjwa haya yote huweza kusababishwa na vifuatavyo: utumiaji wa tumbaku, kutofanya mazoezi kabisa, utumiaji wa pombe kupita kiasi, utumiaji wa vyakula visivyo bora.
Vichangizi vya mwenedo mbaya wa maisha (lifestyle factors) ya kila siku kwa wanawake, huchangia wanawake kuacha kupata hedhi, hii ni kutokana na utafiti uliofanya na kituo cha utafiti wa saratani nchini Uingereza (Institute of Cancer Research in UK).
 
Uvutaji sigara ndio huathiri zaidi wanawake na kuwafanya wanawake wavutaji sigara kuingia katika hatua hii ya kuacha kupata hedhi miaka miwili mapema zaidi ikilinganishwa na wanawake ambao hawavuti sigara.
 
Hata hivyo kuongezeka uzito kumeonekana kuwa na matokeo ghasi kwani, kuongezeka uzito kunasababisha mwanamke kuingia katika hatua ya kuacha kupata hedhi kwa kuchelewa kwa mwaka mmoja zaidi ikilinganishwa na wanawake ambao hawana uzito mkubwa. Hii inahusishwa na uingilianaji wa mafuta (kwa watu wanene/walio na uzito ulopitiliza) na homoni za kujamiana (sex homones).
 
Wanawake huingia katika hatua ya kuacha kupata hedhi kwa kuchelewa zaidi kwa mwaka mmoja kama watakuwa wanakunywa chupa mbili za pombe kwa siku kwa wale walio na  umri kati ya miaka 25 na 49, au  wale wanaofanya mazoezi mazito  mara kwa mara kati ya umri wa miaka 39 na 49 au wale ambao hawali nyama  au vyakula vinavyotokana na nyama (vegetarian).

Ugonjwa wa moyo unaosababishwa na simanzi au kuachana na mpenzi/mwenza wako yoyote yule hujulikana kitaalamu kama Takostubo au broken heart syndrome.

Ugonjwa huu husababishwa na kudhoofika ghafla kwa misuli ya moyo kwa muda mfupi na hauuhusiani na tatizo la kukosekana kwa damu ya kutosha katika moyo.Tatizo hili hujulikana kama broken heart syndrome kwa sababu hutokana na mtu;

  • Kufiwa na mpenzi/mwenza wake
  • Kuachana na mpenzi/mwenza wake
  • Kuwa na wasiwasi mara kwa mara kwa muda mrefu

Vilevile tatizo hili huweza kupelekea moyo kushindwa kufanya kazi  ghafla (Acute heart failure), moyo kupiga bila mpangilio usio wa kawaida (lethal ventricular arrhythmia) .

Dalili

  • Maumivu makali ya kifua
  • Matatizo ya upumuaji au kuhema kwa shida
  • Uchovu
  • Mapigo ya moyo yasiyo na mpangilio

Je tatizo hili husababishwa na nini?

Tatizo hili huweza kusababishwa na mambo yafuatayo:

  • Habari ya kufiwa na mpenzi wako
  • Kutambua unaugua ugonjwa sugu kama vile saratani
  • Kupoteza hela nyingi
  • Sherehe ya kushtukiza (surprise parties)
  • Kutakiwa kuongea hadharani
  • Ukiwa na matatizo kama ugonjwa wa pumu, maambukizi, ajali ya gari au baada ya upasuaji mkubwa.

Vipimo

  • ECG
  • X-ray ya kifua
  • Echocardiogram
  • MRI  
  • CAG
  • Kipimo cha damu kuangalia vimeng’enyo vya kwenye moyo
  • Ni muhimu kutofautisha na Shambulizi la moyo na hili tatizo

Matibabu

Hakuna tiba ya madawa iliyo maalum kwa ajili ya kutibu tatizo hili pekee. Matibabu yake yanaweza kufanana na matibabu ya shambulio la moyo, na mgonjwa anaweza kuhitaji kulazwa hospitali kwa muda ingawa si mara zote huwa hivyo.

Daktari akishathibitisha kuwa chanzo cha dalili zako ni broken heart syndrome na wala si shambulio la moyo anaweza kukupatia dawa kama vile zilizo katika kundi la angiotensin-converting enzyme (ACE) inhibitors mfano Benazapril, kundi la beta blockers kwa mfano carvedilol au kundi la diuretics kama vile frusemide (lasix). Dawa hizi husaidia kupunguza mzigo katika moyo na pia kuzuia usipate shambulio jipya. 

Kwa kawaida wagonjwa wengi hupata nafuu baada ya muda wa kama mwezi mmoja au miwili hivi. Hata hivyo ni vema kumuuliza daktari wako unapaswa kutumia dawa kwa muda gani. 

Kinga

Kuna uwezekano mkubwa sana wa hali hii kujirudia tena mara baada ya shambulio la kwanza. Mpaka sasa hakuna dawa zilizothibitishwa zinazoweza kusaidia kuzuia hali hii isijitokeze tena, ingawa baadhi ya madaktari wanashauri matumizi ya muda mrefu ya dawa zakundi la beta blockers kama vile atenolol, carvedilol, au dawa zenye kuzuia uzalishaji wa homoni zenye kuchochea shinikizo katika moyo.

Pamoja na matumizi ya dawa, ushauri nasaha pamoja na kubadili mfumo wako wa maisha ni mambo ya muhimu zaidi kusaidia kukukinga na tatizo hili. 

 

Ukweli kuhusu umuhimu wa mazoezi katika kuzuia na kutibu magonjwa mbalimbali

Iwe unafanya kwa nia ya kuwa na umbo lenye muonekano mzuri, au kupoteza muda wa ziada ulionao, mazoezi ni zaidi ya unavyoweza kufikiria.

Ongezeko la tafiti katika eneo la mazoezi na magonjwa yahusianayo na mifumo ya maisha (lifestyle-related diseases) lililotokea ndani ya takribani miaka kumi iliyopita, limefumbua macho ya wengi juu ya umuhimu wa mazoezi katika kujikinga na kutibu magonjwa mbalimbali. Tafiti katika eneo hili zinaonesha kwamba mazoezi yanaweza kutumika kujikinga na magonjwa zaidi ya ishirini na kutibu magonjwa takribani kumi.

Ni jambo lililowazi kabisa kwamba babu zetu waliweza kuishi kwa miaka mingi zaidi ya kizazi tulichopo sisi. Ni dhahiri pia kwamba kizazi chetu kinashuhudia milipuko ya magonjwa ambayo babu zetu hawakuwahi hata kuyasikia. Pia mtakubaliana nami kuwa, kumekuwa na mambo mengi ya kimaendeleo yaliyotokea katika kipindi chote hiki, ambayo wanazuoni wamekuwa wakiyahusisha na milipuko ya baadhi ya magonjwa.

Yapo mambo mengi katika mifumo yetu ya maisha ya kila siku yaliyo mazuri katika muonekano na hisia, lakini ukweli ni kwamba yaweza kuwa na athari kubwa kwa afya zetu.

Kila mtu anapenda kuendesha gari wakati wote anapohitajika kwenda sehemu, pia watu wengi wanafurahia kuketi na kuangalia vipindi wavipendavyo katika runinga muda wote wapatapo wasaa. Si ajabu pia watu wengi wanapenda shughuli zisizohitaji kutembea tembea au kutumia nguvu.

Miaka ya nyuma iliaminika kuwa ugonjwa wa kuoza kwa meno si wa kuambukiza; lakini tafiti nyingi zilizofanyika zimedhihirisha ni ugonjwa wa kuambukiza. Jino lililooza linaweza kuambukiza meno yaliyogusana nalo na pia mgonjwa aliyeoza meno au mwenye wadudu wanaosababisha kuoza kwa meno anaweza kuambukiza mwenzake/wenzake.

Wadudu wanaosababisha kuoza kwa meno ni sehemu ya wadudu wakazi kinywani (oral flora). Wadudu hawa hujishikiza kwenye meno na kufanya utando, wana uwezo wa kuchachua vyakula hasa vyenye asili ya sukari na kutoa tindikali. Ni tindikali hii ambayo huvuta madini kwenye meno na kuweka matobo. Utando huu wa wadudu kwenye jino moja unaweza kuwa na wadudu nusu bilioni, miongoni mwao wakiwemo jamii ya mutans streptococci ambao kimsingi ndiyo wasababishaji wakuu wa kuoza kwa meno. Wadudu wengine ni kama Lactobacillus na Actinomyces.

 Kujamiana (ama tendo la ndoa) ni moja ya mambo muhimu sana katika maisha ya mwanadamu. Ni ukweli usiofichika kwamba wengi wetu tungependa kuwa na mwenza ambaye mnaridhishana katika tendo la ndoa. Si hivyo tu, bali tendo hili huleta maelewano katika uhusiano wowote ule. Lakini, kuna faida zozote za kiafya za kufanya tendo hili? Ndiyo! Zipo faida kadhaa zinazotokana na kujamiana. Katika makala hii, mwandishi wako Dk. Khamis Hassan anajaribu kutueleza faida za kujamiana kiafya kama ambavyo imewahi kuonekana katika tafiti kadhaa zilizofanyika sehemu mbalimbali duniani.


1. Hulinda mwili dhidi ya magonjwa ya moyo:

Wanawake ambao hufika kilele (orgasm) angalau mara mbili kwa wiki kila wanapojamiana, wana uwezekano mdogo sana (30% tu) wa kupata maradhi ya moyo tofauti na wale wasiofikia kilele. Hii ni kwa vile homoni ya endorphin inayotolewa wakati wa kujamiana hupunguza msongo wa mawazo na hivyo kumuepusha mtu na magonjwa wa moyo. Aidha kujamiana angalau mara tatu kwa wiki, husaidia kupunguza uwezekano wa kupata shambulio la moyo (heart attack) na kiharusi. Uwezekano wa kupata mshtuko wa moyo wakati wa kufanya mapenzi ni mdogo sana, ni asilimia 1 tu ya vifo vyote vinavyotokana na mshtuko wa moyo ndivyo uhusishwa na kujamiana. Aidha, sababu nyingine inayoongeza uwezekano wa kupata mshtuko wa moyo ni kuwa na uhusiano nje ya ndoa ambapo huchangia karibu asilimia 75 ya vifo vinavyotokana na kujamiana, na karibu asilimia 90 ya vifo hivi hutokea kwa wanaume wazee. Uwezekano wa kupata shambulio la moyo wakati wa kujamiana huongezeka ikiwa mtu ana miaka zaidi ya 50, uzito uliopitiliza na matatizo ya afya. Hii ni sawa na kusema unaanza kufanya mazoezi mazito kwa ghafla wakati mwili na umri haviruhusu.

 
2. Huongeza ukakamavu wa mifupa:
 
Wanawake waliokoma kupata hedhi (menopausal women) ambao pia hujamiana angalau mara mbili kwa wiki wana kiwango kikubwa cha homoni ya  oestrogen mara mbili zaidi ya wale ambao hawajamiani. Homoni hii husaidia kulinda mifupa na kwa wanawake waliokoma kupata hedhi wakosapo homoni hii hupata ugonjwa wa mifupa ujulikanao kama osteoporosis. 
 

3. Hupunguza msongo wa mawazo:

Kujamiana hupunguza msongo wa mawazo na shinikizo la damu na humfanya mtu kupata usingizi mnono. Kufikia kilele ni sawa na kunywa 2-3mg za dawa ya diazepam (kumbuka diazepam hufanya mwili kupumzika, muscle relaxant), na hii ndiyo sababu kuu ya kwa nini watu hupata usingizi mzito baada ya kujamiana. Watu wanaojamiana huweza kuhimili vizuri msongo wa mawazo tofauti na wale ambao hawafanyi hivyo. Aidha watu wanaojamiana huwa na kiwango cha kawaida cha shinikizo la damu kuliko wale wasiojamiana. Pia kuwepo kwa viasili vya prostaglandins katika shahawa husaidia kupunguza msongo wa mawazo. Viasili hivi hunyonywa na sehemu za siri za mwanamke. Shahawa pia zina madini ya zinc, calcium, potassium, fructose na protini ambavyo vyote ni muhimu kwa afya njema.

  4 July 2012
MSIMAMO WA SIKIKA KUHUSU MGOMO WA MADAKTARI
UTANGULIZI
SIKIKA ni shirika lisilo la kiserikali linalotekeleza shughuli mbali mbali zenye lengo la kuchochea upatikanaji wa huduma za afya zenye uwiano, viwango na ubora unaokubalika, gharama nafuu na zilizo endelevu. SIKIKA imekuwa mstari wa mbele kufanya tafiti katika sekta ya afya na kuhimiza utekelezaji wa sera, uwajibikaji na upatikanaji wa huduma bora nchini Tanzania.
Kama neno ‘afya’ lilivyo tafsiriwa na Shirika la Afya Ulimwenguni (WHO) Mwaka 1948, sera ya afya ya Taifa (Tanzania Health Policy) ya mwaka 2007, nayo pia inatambua ‘afya’ kama hali ya ukamilifu wa binadamu kiakili, kimwili, kijamii na siyo tu kutokuwepo kwa maradhi. Afya bora ni mhimili wa maendeleo ya mtu binafsi, familia na taifa zima kwa ujumla hasa katika harakati za kuondoa umasikini uliokithiri katika taifa letu.
Katika nchi yetu, mfumo wa utoaji huduma katika sekta ya afya umegawanyika katika ngazi tatu yaani ngazi ya afya ya msingi kama vile zahanati na vituo vya afya, ngazi ya pili kama vile hospitali za wilaya au mikoa na ngazi ya hospitali za rufaa kama vile hospitali ya Muhimbili, Mbeya, Bugando, KCMC na hospitali maalumu kama taasisi ya magonjwa ya kansa ya Ocean Road au hospitali ya magonjwa ya akili ya Milembe. Hospitali hizi za rufaa hushughulika na magonjwa ambayo ama yameshindikana katika hospitali za ngazi za chini au wataalamu waliopo katika ngazi hizo na vifaa vilivyopo haviwezi kutoa huduma stahili kwa magonjwa hayo. Hivyo basi, iwapo kutakuwa na matatizo yanayoathiri utendaji wao wa kazi wa kila siku na kwa kuwa wagonjwa walioletwa katika hospitali hizi za rufaa hawawezi kurudishwa kule walikotoka (ngazi za chini), wagonjwa hawa wasio na hatia ndiyo waumiao kutokana na matatizo hayo.
Migomo ya watumishi katika sekta ya afya ni mojawapo ya matatizo yanayoweza kuathiri utendaji kazi wa wataalamu wa afya, siyo tu katika hospitali za rufaa hata pia katika hospitali za ngazi za chini. Kwa historia ya migomo hii, Mwananchi anayehitaji huduma za afya hana mchango wa moja kwa moja katika kusababisha migomo ya watumishi wa afya. Mwananchi ameiweka serikali madarakani na analipa kodi ili serikali hiyo itoe huduma bora za kiafya kwake ili awe na nguvu za kujiletea maendeleo yake na taifa kwa ujumla.
MGOMO WA MADAKTARI
Kwa muda mrefu sasa, kumekuwa na migomo ya mara kwa mara kuanzia kwa wanafunzi wa vyuo vikuu mpaka kwa wafanyankazi wa serikali. Mwaka 2001, tulishuhudia mgomo mkubwa wa wanafunzi wa chuo cha Sayansi za tiba Muhimbili wakishinikiza uboreshwaji wa mazingira ya kusomea hasa masomo kwa vitendo. Mwaka 2005, tukashuhudia mgomo mkubwa wa madaktari wa hospitali ya Muhimbili na sehemu nyinginezo waliokuwa wakidai uboreshwaji wa maslahi yao, mgomo ambao uliathiri utoaji huduma katika hospitali nyingi hasa za rufaa. Kuelekea Mwaka jana, vuguvugu la mgomo wa madaktari lilipelekea kuwepo kwa mgomo mwanzoni wa mwaka huu ambao umekuwa ukiendelea kwa vipindi tofauti hadi sasa.
Japo serikali imekuwa ikitafuta njia za mkato kuendeleza huduma katika hospitali ya Muhimbili kama vile kuleta madaktari waliostaafu ama madaktari kutoka jeshini ambao hawakidhi mahitaji ya huduma katika hospitali hiyo ya Taifa, huduma katika hospitali nyingine zisizonufaika na njia hizi za mkato hudorora siku hadi siku kwa kipindi chote cha migomo huku wananchi wakiendelea kupata taabu.
Vitendo vya ukiukwaji wa haki za binadamu kama vile kutekwa na kupigwa kwa Mwenyekiti wa kamati maalumu ya Jumuiya ya madaktari iyosimamia madai yao, Dr. Stephen Ulimboka, ubabe, vitisho na matumizi ya nguvu dhidi ya madaktari wanaodai haki zao badala ya kutatua matatizo hayo kwa njia ya amani, siyo tu vinakiuka Katiba ya nchi inayojichanganua kimataifa kama nchi ya amani bali pia vimepunguza morali ya watumishi hawa kutoa huduma kwa wananchi ambao kama tulivyosema awali hawana mchango wa moja kwa moja katika kusababisha mgogoro huu.
Madai ya Madaktari.
Katika mgomo huu unaoendelea, madai ya madaktari, mbali na dai la awali la kusisitiza kuondolewa kwa viongozi wakuu katika wizara ya afya wanaokwamisha maendeleo ya sekta hii, madai yao yamejikita katika sehemu kuu mbili ambazo ni uboreshwaji wa mazingira ya kazi na vifaa vya tiba na Uboreshwaji wa kipato, kinga na afya za madaktari (Mishahara, posho na Bima ya afya).
Uboreshwaji wa mazingira ya kufanyia kazi na vifaa vya tiba
Kulingana na maelezo ya madaktari, hii ndiyo hoja kubwa katika madai yao ambayo inalenga kuhimiza serikali kukarabati miundombinu ya afya, kuongeza vitanda na kuongeza upatikanaji wa vifaa vya kutendea kazi. Katika tamko la jumuiya ya madaktari Tanzania lililotolewa kwa waandishi wa habari tarehe 28 Juni 2012, sehemu ya tamko hilo inasema:
“…Madaktari wamechoka kuona huduma za afya nchini zikizidi kudorora mwaka hadi mwaka…
… Tumechoka kuona wagonjwa wakilala chini na watoto wakilala wanne katika kitanda kimoja…
…Tumechoka kuona msongamano mkubwa wa wagonjwa katika hospitali zetu huku kukiwa hakuna
mpango wowote wa uboreshaji…
…Tumechoka kuona wagonjwa wakikosa dawa, vipimo sahihi na watumishi wa afya wakifanya kazi katika mazingira magumu yanayoviza ubora wa huduma na misingi ya taaluma…
… Kwahiyo, kwa moyo wetu leo, tumejitolea kutetea uboreshaji wa sekta ya afya ….’’
Sera ya Taifa ya afya ya mwaka 2007 katika kipengele kinachohusu rasilimali watu inasema;
‘… Uboreshaji wa mazingira ya kazi ikiwa ni pamoja na upatikanaji wa vitendea kazi vya kutosha kwa
watumishi wa afya…
… Kuweka vivutio katika sehemu zenye mazingira magumu na hatarishi ili kuwavutia wataalamu kwenda kufanya kazi katika sehemu hizo…’
Katika madai ya awali ya madaktari, walisikitishwa na wimbi kubwa la viongozi wa kisiasa na serikali wanaotibiwa nje ya nchi. Zaidi ya hayo, madaktari walibaki kuwa waidhinishaji wa rufaa za kwenda kutibiwa nje ya nchi. Hali hii, siyo tu inaweza kuongeza mwingilio wa maamuzi ya kitaalamu kwa shinikizo za watawala wa kisiasa kwa kuwashinikiza madaktari kutoa rufaa kinyume na maadili yao, bali pia inapunguza nia ya kisiasa ama ‘political will’ ya viongozi wa kisiasa na serikali katika kushughulikia kero za afya za wananchi kwa kuwa ‘wao’ wana uhakika wa matibabu nje ya nchi. Hali hii siyo tu inaondoa usawa wa kimatibabu kati ya viongozi na wananchi, na serikali kutumia fedha nyingi ambazo zingeweza kutumika kuboresha sekta ya afya hapa nchini bali pia nchi hushindwa kuwa na miundo mbinu ya uhakika ya kushughulikia magonjwa ya dharura ambayo muda hautaruhusu kutibiwa nje ya nchi. Nchini Malawi kwa mfano, kifo cha Rais Bingu wa Mutharika, kutokana na shinikizo la damu tarehe 5 Aprili mwaka huu kilihusishwa na serikali yake kushindwa kuboresha miundombinu na huduma za afya nchini mwake.
Katika utafiti wa Sikika kuhusu upatikanaji wa madawa na vifaa tiba uliofanyika katika wilaya 71 mwaka 2011, waganga wakuu wa wilaya waliohojiwa, walithibitisha kutokuwepo kwa gozi (gauze) katika asilimia 48 ya wilaya zote huku asilimia 44% ya wilaya zikiwa na gozi zisizotosheleza mahitaji. Katika ngazi ya vituo vya afya na zahanati, asilimia 63% hazikuwa na gozi huku asilimia 27% ikiwa haina gozi za kutosha. Kukosekana au kuwa na idadi pungufu ikilinganishwa na mahitaji uliendelea kuwepo kwa kati ya miezi mitatu hadi sita. Vivyo hivyo, katika ngazi za wilaya, glovu (surgical gloves) hazikuwepo katika asilimia 28% ya wilaya, dawa za kutibu malaria aina ya ALU asilimia 32% ya wilaya na sindano za Quinine asilimia 13% ya wilaya zote zilizoshiriki katika utafiti. Katika ngazi ya vituo vya afya na zahanati, asilimia 17% hazikuwa na glovu, asilimia 30% hazikuwa na ALU, asilimia 23% hazikuwa na sindano za Quinine na asilimia 17% haikuwa na vidonge vya Amoxcycillin. Katika utafiti huo pia, Sikika iligundua kuwa katika ngazi ya wilaya asilimia 93% ya wilaya hupata dawa na vifaa tiba chini ya maombi na mahitaji halisi na katika ngazi ya vituo vya afya na zahanati asilimia 90% hupata dawa na vifaa vya tiba chini ya maombi na mahitaji halisi.
Yapo madhara makubwa yatokanayo na upungufu wa dawa na vifaa vya tiba. Madhara hayo yaweza kupelekea kuona wagonjwa waliozidiwa au walio na dharura pekee (critical patients & emergencies) hali ambayo inajitokeza katika zahanati na vituo vya afya vingi. Madhara mengine ni kuongezeka kwa usugu wa vimelea vya magonjwa dhidi ya dawa kutokana na kupata kiasi kidogo, kuongezeka kwa madhara ya magonjwa yatokanayo na kutopata tiba sahihi (complications) kama ulemavu kwa watoto ambao wamekosa tiba sahihi ya malaria, kuongezeka kwa malalamiko toka kwa wananchi dhidi ya watumishi wa afya na mbaya zaidi kupungua kwa morali ya kazi kwa watumishi wa afya na kufanya kazi kinyume na misingi au maadili ya kitaalamu kama walivyosema madaktari hapo juu, ‘mazingira magumu yanayoviza ubora wa huduma na misingi ya taaluma’.
Wengi wetu ni mashahidi wa huduma zisizoridhisha katika hospitali za serikali, msongamano wa wagonjwa wodini hasa akinamama na watoto, ukosefu wa mara kwa mara wa vifaa vya tiba na matatizo mengine.
Tanzania hupoteza takribani asilimia 6% ya wagonjwa wanaohitaji huduma za CT Scan kwa mwaka. Hata hivyo, kifaa cha CT Scan katika hospitali ya Muhimbili kimeharibika kwa zaidi ya miezi saba sasa bila matengenezo ikiwalazimu wagonjwa wanaohitaji majibu ya kipimo hicho ili wapate tiba stahili, kwenda katika hospitali binafsi. Gharama za kipimo hicho katika hospitali ya Muhimbili ni takribani shilingi 170,000/= lakini katika hospitali binafsi ni kati ya shilingi 200,000/= hadi 500,000/=. Mbali ya hayo, katika ufuatiliaji wa Sikika wa mwaka 2011 kwenye wilaya 6 za mkoa wa Dar Es salaam, Pwani na Dodoma, kati ya vituo 38 vinavyotoa huduma kwa watu waishio na VVU (Care and treatment Centers) ni vituo 13 tu vilivyokuwa na mashine za CD4+ zinazotumika kuangalia maendeleo ya tiba kwa watu waishio na VVU na kati ya hizo ni mashine tano (5) ndizo zilikuwa zikifanya kazi. Ni wajibu wa serikali kuboresha mazingira ya kazi ya watumishi wa afya na kuhakikisha upatikanaji wa vifaa tiba kwa muda wote, kwa sababu hii Sikika tunaungana na madaktari katika kudai uboreshaji wa mazingira ya kazi kwa watumishi wa afya, kuhakikisha dawa na vifaa tiba vinapatika hasa maeneo ya vijijini ili kuboresha afya za wananchi kwa maendeleo yao na taifa kwa ujumla.
Uboreshaji wa kipato, kinga na afya za madaktari (Mshahara, posho, Bima ya afya).
Madai mengine ya madaktari ni uboreshwaji wa mapato yao ikiwa ni pamoja na mishahara, posho ya kuitwa kazini baada ya saa za kazi (on call allowance), posho ya kufanya kazi katika mazingira magumu (hardship allowance) na posho ya makazi. Vile vile madaktari wanadai posho ya kufanya kazi katika mazingira hatarishi (risk allowance) na chanjo ambayo ni muhimu ili kuzuia uwezekano wa madaktari kupata magonjwa ambayo wanaweza kuyasambaza kwa wagonjwa wengine ambao tayari wana matatizo yao ya kiafya.
Madai ya nyongeza ya mishahara
Katika madai yao ya mishahara, madaktari walipendekeza kiwango cha shilingi milioni 3.5 kwa mwezi. Hata hivyo, wakati akiongea na madaktari Tarehe 9/2/2012, waziri mkuu Mh. Mizengo Pinda alitoa ufafanuzi wa madai yanayohusu maslahi ya watumishi wa afya bila kutoa majibu ya moja kwa moja ya kiwango gani kitalipwa na serikali kama mishahara na posho kwa sababu ‘wataalamu’ walikuwa wanafanyia kazi suala hilo ili waweze kumshauri, na hadi sasa serikali haijatamka kiwango halisi itakachoweza kulipa. Pia waziri mkuu hakuweza kueleza moja kwa moja kuhusu madai ya uboreshaji wa mazingira ya kazi na upatikanaji wa vifaa tiba. Kwa sasa, mshahara wa daktari ni Tshs 957,700/= na baada ya makato ya kodi hubaki na Tshs 680,000/= kwa mwezi. Katika ufuatiliaji wa Sikika wa Disemba 2011 hadi January 2012, katika hospitali ya Regency, ilibainika kuwa hakuna daktari anayepata mshahara chini ya shilingi milioni mbili (gross pay) na Agha Khan hospitali, daktari mwenye uzoefu wa chini ya miaka minne alikuwa akilipwa shilingi milioni 1.8 kuachilia mbali mafao mengine kama vile bima ya afya, posho za nyumba n.k. Sikika inatarajia kuwa serikali pia itaboresha mishahara ya madaktari na mafao mengine ili kuongeza tija katika hospitali za umma.
Madai ya Posho
Katika madai yao, madaktari wamependekeza viwango vifuatavyo kwa posho mbali mbali: posho ya muda wa ziada wa kazi (call allowance) asilimia 5% ya mshahara kama ilivyo kisheria kwa kada yoyote; posho ya kufanya kazi katika mazingira magumu asilimia 40% ya mshahara; posho ya makazi asilimia 40% au nyumba kama ilivyo kisheria na posho ya kufanya kazi katika mazingira hatarishi asilimia 30% au chanjo (Homa ya ini-hepatitis, HIV/AIDS, TB)
Hoja za Serikali
Serikali imeendelea kusisitiza ufinyu wa bajeti na kwamba, kuwaongezea mishahara madaktari peke yaokutaondoa ulinganifu na kuongeza migogoro katika sekta nyingine. Hata hivyo, sehemu ya sheria yakazi ya mwaka 2004 (Employment and Labour Relations Act, Kifungu cha 6: (20) (4)), inasomeka hivi“Mwajiri atamlipa mwajiriwa walau 5% ya mshahara wa msingi wa mwajiriwa kwa kila saa aliyofanya kazi usiku’’.Kwa mahesabu rahisi, daktari alipaswa kupata angalau Tshs 47,000/= kwa saa anapofanya kazi usiku.Hata hivyo waraka wa serikali wenye Kumb. No. C/AC.17/45/01/F/73 wa tarehe 21 February 2012kutoka kwa George D. Yambesi (Katibu Mkuu Utumishi) kwenda kwa Katibu Mkuu wa Wizara yaAfya na Ustawi wa Jamii wenye kichwa, ‘Malipo ya kuitwa kufanya kazi baada ya saa za kazi (On callallowance)’ unaelekeza kulipa viwango vifuatavyo kwa siku kwa watumishi wa afya kuanzia tarehe 9February 2012 (Siku 12 Nyuma); Wataalamu bingwa Tshs 25,000/= na madaktari wa kati Tshs20,000/=. Katika nchi ya jirani ya Kenya kwa barua yenye Kumb No. MSPS/2/1/3A Vol.III/(77), yatarehe 12 January 2012 toka ofisi ya Waziri Mkuu kwenda kwa Katibu Mkuu wa wizara husika,madaktari, wataalamu wa kinywa na wafamasia wanalipwa takribani Tshs 38,000/= kama posho ya ‘call allowance’ hali ambayo inaweza kusababisha kupungua kwa rasilimali watu katika sekta ya afya nchini Tanzania (Brain Drain) kwa kukimbilia nchi jirani kufuata kipato kizuri hasa wakati huu wa soko huria la ajira katika shirikisho la Afrika Mashariki.
Sikika imekuwa mstari wa mbele kupinga pesa zinazotumika kama posho za vikao kwa watumishi ambao tayari wanalipwa mishahara kwa kazi husika. Hata hivyo, katika waraka wenye Kumb. No. C/AC.17/45/01/125 wa tarehe 11 Februari 2010 wenye kichwa ‘Waraka wa Utumishi wa Serikali Na.2 wa mwaka 2010: Posho ya vikao (Sitting Allowance) Serikalini,’ viwango ‘vipya’ vya posho ya vikao vilivyotajwa ni Mwenyekiti/Katibu 200,000/=, Wajumbe 150,000/= na sekretarieti 100,000/=. Posho hizi kubwa si tu kwamba zinadhihirisha matumizi mabaya ya fedha za walipa kodi bali pia zinapunguza nguvu kazi katika sekta ya afya kwani watumishi wengi wanahangaika kutafuta nafasi ya kushiriki katika vikao badala ya kufanya kazi zao.
Hoja ya ‘ulinganifu’ au ‘lawama’ kwa sekta nyingine haina nguvu kwani nchini Marekani kwa mfano, pato la daktari ni zaidi ya mara 100 ya kima cha chini cha mshahara kwa saa katika nchi hiyo, na nchini Botswana, ambako Madaktari wengi Watanzania hukimbilia kwa sababu za kimaslahi, mshahara wa daktari ni sawa na Tshs kati ya milioni 3.2 hadi 5.8 kwa mwezi. Hoja hii pia, kwamba madaktari wakipewa mshahara mkubwa italeta malalamiko katika kada nyingine inadhihirisha jinsi ambavyo serikali inawakandamiza kimaslahi watumishi wake. Hili lilidhihirika wakati wa mgomo wa walimu mwaka 2010, Kaimu Katibu Mkuu wa shirikisho la vyama vya wafanyakazi (TUCTA) bwana Nicholas Mgaya, alisema … ‘Tumedai kwamba Kima cha chini cha mishahara kiwe ni Tshs 315,000/=. …………lakini serikali ikang’ang’ania Tshs 135,000/= kiasi ambacho bado ni kidogo’’ (Daily News, August, 2010). Vivyo hivyo, utafiti wa “Motivation of Health Care Workers in Tanzania: A Case Study of Muhimbili National Hospital” uliotolewa katika Jarida la East African Journal of Public Health Volume 5 Number 1, April 2008 ulionesha kuwa Asilimia 88 ya watumishi waliamini kuwa mwajiri wao hawajali (madaktari asilimia 82.4, wauguzi asilimia 90.7 na watumishi wengine asilimia 87.9). Hata hivyo sababu tatu kubwa zilizoonekana kuwafanya watumishi hao kutokuwa na motisha mzuri wa kazi ni mishahara, mazingira ya kazi, na vifaa duni vya kazi na asilimia 30 ya wauguzi walikuwa hawajaridhika na kazi zao kiasi cha kutaka kuacha kazi hizo. Hali ya kuwa serikali imekuwa haikubali mapendekezo ya watumishi wake au hata mapendekezo ya tume zinazoundwa na serikali yenyewe hasa katika uboreshaji wa maslahi ya wafanyakazi wa sekta ya afya kwa ujumla, inatufanya Sikika tuungane na madaktari katika madai yao.
Katika bajeti ya sasa 2012/213, kipengele cha uendelezaji wa rasilimali watu katika sekta ya afya kimetengewa bilioni 23.4 na matumizi ya kawaida (recurrent expenditure) yametengewa Tshs bilioni 24.5). Hata hivyo kati ya fedha iliyotengwa kuendeleza rasilimali watu, bilioni 21.6 sawa na asilimia 92.3% inategemea msaada wa wafadhili. Hali hii ya utegemeji inapingana na sera ya afya ya Taifa inayotamka kuwa serikali iwe mfadhili mkuu wa sekta ya afya.
Wakati huo huo, mpango mkakati wa sekta ya afya (Health Sector Strategic Plan III) umeweka malengo ya bajeti ya sekta ya afya kufikia asilimia 10% ya bajeti yote ya serikali mwaka 2015. Hii inapingana na azimio la Abuja (asilimia 15) ambalo Rais wetu alitia saini na inapingana pia na sera ya afya ya mwaka 2007 inaposema, ‘Serikali itaendelea kuongeza bajeti ya sekta ya afya …hadi kufikia azimio la Abuja….ilikukidhi mahitaji muhimu ya kisekta’ . Kwa ukiukwaji wa makubaliano ya azimio la Abuja na kutoitekeleza sera ya afya ya Taifa kama inavyotakiwa, yote haya yanadhihirisha kuwa serikali haina nia ya dhati ya kusimamia maamuzi yake katika ngazi za kimataifa na kitaifa. Tukirejea tena katika sera ya afya ya mwaka 2007 inasema, ‘kuwepo kwa watumishi wa kutosha wenye ujuzi katika ngazi zote za kutolea huduma kulingana na vigezo vilivyokubalika’. Udaktari ni mojawapo ya fani ambazo katika nchi nyingi zimepewa jina la ‘scarce skills’ yaani ujuzi adimu. Kwa miaka kadhaa sasa, idadi kubwa ya wanafunzi wa shule katika ngazi za chini wameendelea kuyakimbia masomo ya sayansi na wanafunzi wanaodahiliwa kusomea masomo ya udaktari ni wale ambao kiwango chao cha ufaulu katika masomo ya fizikia, kemia na biologia kiko juu sana, hivyo madaktari kulipwa mishahara mikubwa ili waweze kuokoa maisha ya watanzania si tatizo, kwa maoni ya Sikika.
Tena, hoja ya ufinyu wa bajeti inakosa nguvu katika madai haya kwani, katika tafiti za Sikika tumeonyesha jinsi ambayo serikali imeendelea kuwa na matumizi mabovu ya fedha za walipa kodi na ukosefu wa vipaumbele katika matumizi yake.
Katika chapisho la Sikika lenye kichwa, ‘Matumizi yasiyo ya lazima, Taarifa fupi kuhusu mpango wa serikali katika kuangalia Upya matumizi’ toleo no. 2 la July 2010 lililotolewa kwa ushirikiano wa Policy forum linaonyesha kuwa matumizi yasiyo ya lazima serikalini yalikuwa bilioni 684 mwaka 2008/09, billioni 530 mwaka 2009/10 na bilioni 537 mwaka 2010/11. Zaidi ya hayo,, matumizi katika posho mbali mbali yaliongezeka toka bilioni 171 mwaka 2008/09 hadi bilioni 269 mwaka 2010/11. Gharama za kusafiri nje na ndani ya nchi zilikuwa bilioni 155 mwaka 2008/09 na bilioni 124 mwaka 2010/11. Gharama za mafuta ya kuendeshea na kulainisha magari ya kifahari ya serikali (Mbali na ununuzi) zilikuwa zaidi ya bilioni 52 mwaka 2010/11 na manunuzi ya magari ya serikali yaligharimu Bilioni 15.3 mwaka 2010/11 pekee. Mbali ya hayo, serikali imekosa vipaumbele katika matumizi yake mfano ni matumizi ya zaidi ya bilioni moja kwenye wizara ya afya wakati wa sherehe za Nane Nane..
Katika sekta ya afya pekee, matumizi yasiyo ya lazima (unnecessary expenditure) yaliongezeka toka bilioni 16.1 mwaka 2010/11 hadi bilioni 22 mwaka 2011/12, na inakadiriwa kufikia bilioni 25 katika bajeti ya 2012/13, posho mbalimbali zikiongoza katika matumizi. Posho hizo zinalenga watu wachache sana hasa watawala na hazina tija katika utoaji wa huduma za afya. Posho zimefanya utendaji kazi uwe hafifu na kupunguza uwajibikaji ilhali watumishi wasio katika nafasi za kitawala wakiendelea kuambulia maslahi madogo
Taarifa za CAG pia zinadhihirisha matumizi mabovu na usimizi mbovu wa rasilimali za taifa kwa mfano msamaha wa kodi uliongezeka toka bilioni 680 mwaka 2009/2010 hadi Trilioni 1.016 kwa mwaka wa 2010/11. Hii inawakilisha asilimia 18% makusanyo yote ya pato la Taifa na ni kiwango kikubwa sana kuliko nchi nyingi za Afrika. Matumizi yasiyokusudiwa bilioni 8, bilioni 31 zimelipia vifaa ambavyo havikufika na Malipo yanayotia shaka bilioni 1.4.
Rasimali watu katika Sekta ya Afya
Tumeshuhudia matamko ya hospitali kadhaa hospitali za mikoa ya Mbeya, Dodoma, Morogoro, Kilimanjaro na Mwanza zikiwafukuza madaktari waliogoma badala ya kushiriki katika kutatua mgogoro huu ili warejee kazini na kuepuka kupoteza nguvu kazi yenye upungufu mkubwa katika sekta ya afya. Shirika la afya duniani (World Health Organization), linapendekeza kwamba kila daktari anatakiwa ahudumie watu wasiozidi 5,000. Kwa mujibu mkutano mkuu wa chama cha madaktari Tanzania (MAT) tarehe 10 hadi 11 August, 2010 pale Mlimani city, uwiano wa daktari mmoja kwa idadi ya watu ulikuwa 1:300 wakati wa uhuru na hali ikawa mbaya kwa kasi hadi uwiano wa 1: 30,000 mwaka 2010. Kwa upande wa wafamasia kwa mfano, wakati kukiwa na vituo vya kutolea dawa 4,185 vya serikali na 1,056 vya binafsi nchini mwaka 2009, kulikuwa na wataalamu 1,506 pekee waliopata mafunzo ya ufamasia na wafamasia 703 wenye shahada ya ufamasia. Katika utafiti wa Sikika wa HRH Tracking Study 2010, ulionyesha kuwa asilimia 54% ya wilaya zote zilizoshiriki katika utafiti zilikuwa na upungufu mkubwa wa watumishi wa afya. Hata hivyo, idadi ya watumishi wanaopangiwa vituo vya kazi na kuripoti ni asilimia 70% kwa wilaya za vijijini na asilimia 93% kwa wilaya za mijini. Zaidi ya hayo, wilaya nyingi hazipati wafanyakazi kulingana na maombi yao, kwa mfano katika utafiti huu, wilaya nyingi zilipata ni asilimia 35% ya wafanyakazi katika maombi yao, huku hali ikiwa mbaya maeneo ya vijijini.
Katika mpango wa kukuza rasilimali watu unaoisha mwaka 2013, bajeti ya jumla ya mpango huo ilikiwa bilioni 470, wastani wa bilioni 91 kwa mwaka. Mwaka 2011/12, wizara ya afya na ustawi wa jamii iliomba bilioni 66.3 ili kutekeleza mkakati wa rasilimali watu kisekta, hata hivyo serikali ilitenga bilioni 13.2 pekee na hadi kufikia January 2012, asilimia 20% (bilioni 2.7) pekee ndiyo iliyokuwa imetolewa kwa wizara.
Wakati mkakati wa kuboresha sekta ya afya (HSSP III) ukionyesha upungufu wa rasilimali watu kufikia 92,000, mpango wa ukuzaji wa afya ya msingi (Primary Health Service Development Program 2007- 2017) unahitaji watumishi wa afya 137,813 kuutekeleza. Hata hivyo, udahili katika vyuo vya afya kwa mwaka 2010 ulikuwa wanafunzi 6,949 pekee, na iwapo udahili hautaongezeka, tutahitaji miaka 21 ili kuziba pengo la watumishi katika mpango wa kukuza afya ya msingi (PHSDP) iwapo mambo yatabaki kama yaliyo. Hii inaonyesha kuwa tutaendelea kuwa na upungufu wa watumishi wa afya kwa miaka mingi ijayo. Hata hivyo, katika mwendelezo wa hotuba zake za kila mwisho wa mwezi, Tarehe 01/07/2012, mheshimiwa Rais Jakaya Mrisho Kikwete, siyo tu amedhihirisha kutokutilia maanani upungufu mkubwa wa wataalamu wa afya unaoisumbua nchi yetu, bali pia kama kiongozi wa nchi, ameonyesha jinsi ambavyo serikali ilivyo tayari kupoteza rasilimali hii adimu kwa kushindwa kutatua mgogoro kati yake na madaktari, ambao iwapo wataamua kuacha kazi wote, itatuchukua miaka mingi kuziba pengo hilo.
 
Hitimisho
Kwanza, kutokana na mapungufu mengi tuliyoeleza hapo juu, Sikika inaona kuwa madai ya madaktari ni ya msingi na tunaamini kuwa serikali inaweza kuboresha huduma za afya na maslahi ya wafanyakazi hasa ikidhibiti matumizi yasiyo ya lazima, ikidhibiti ufujaji wa kodi za wananchi kwa baadhi ya watendaji wake, ikipunguza misamaha ya kodi na ikitekeleza mikakati iliyopo katika sera zake kikamilifu.
Pili, Sikika inaungana na madaktari, wanaharakati na wananchi kulaani vitendo vya ukiukwaji wa haki za binadamu aliofanyiwa mwenyekiti wa kamati maalumu ya jumuiya ya madaktari Dr. Stephen Ulimboka na kupendekeza uundwaji wa tume huru yenye mchanganyiko wa wananchi katika kuchunguza tukio hilo.
Tatu, Sikika inaihimiza serikali kuacha kutumia vitisho na ubabe katika kutatua mgogoro wake na madaktari. Vitendo hivi vinaweza kupunguza morali na ufanisi wa madaktari kiutendaji na pengine kupelekea wengine kuhama sekta ya afya au kukimbilia nje ya nchi. Badala yake serikali ifanye mapatano na wataalamu hawa muhimu, ili waweze kurejea kazini haraka kutoa huduma kwa wananchi wanaoendelea kuumia kwa kukosa huduma.
 
 
 
P.o.Box 12183 Dar Es Salaam,
 
Phone: +255222666355/57 Fax: +255222668015
E-Mail: info@sikika.or.tz web: www.sikika.or.tz
 
 

 

 

 

Nodding disease

Mtoto Saul amekumbwa na ugonjwa wa ajabu wa kusinzia na kutikisa kichwa. Mama yake anasema Saul hupatwa na degedege linaloweza kumchukua muda wa hadi si chini ya saa tatu kupata nafuu na kila shambulio huwa kali kiasi cha kumfanya mama abaki asijue la kufanya. Mama Saul anasema, tangu mwanaye akumbwe na ugonjwa huu amekuwa si yule anayemfahamu, amekuwa kama mtoto aliyechanganyikiwa akizungukazunguka bila kujua alifanyalo. Mama Saul anasema, kuna wakati Saul aliwahi kupotea kijijini bila kujulikana yupo wapi kiasi kwamba hivi sasa inampasa kuwafungia ndani watoto wake wengine ili wasipotee kama ndugu yao.

Mtoto Saul ni miongoni tu mwa mamia kwa maelfu ya watoto waliokumbwa na ugonjwa wa ajabu wa kusinzia na kutikisa kichwa huko nchini Uganda pamoja na Sudan ya Kusini na sasa inasemekana umeshaingia nchini Tanzania. 

Mpaka sasa si madaktari wala wanasayansi wanaoelewa kwa undani chanzo halisi cha ugonjwa huu ingawa juhudi za kitafiti zinaendelea. 

Ugonjwa wa kusinzia na kutikisa kichwa umepewa jina la 'Nodding disease' kwa sababu watoto wanaokumbwa na ugonjwa huu huonesha dalili ya kutingisha kichwa kama mtu anayeitikia kitu pamoja na dalili nyingine zinazofanana na za mtu mwenye kifafa zikiambatana na kusinzia. 

Zipi hasa ni dalili za ugonjwa huu?
Watoto wenye ugonjwa wa kusinzia huathirika zaidi mfumo wao wa fahamu pamoja na ubongo [1] wa kupatwa na shambulizi kali la degedege, kushindwa kula chakula na kubadilika kabisa kitabia. 

Mtoto huanza kuonesha hali ya kutikisa kichwa kama anayeitikia jambo, hufumba macho, kisha huinamisha kichwa chake kama anayesinzia, lakini akiwa haoneshi dalili yoyote ya kuchoka na pia huonekana kupambana ili asipoteze ufahamu. Kisha huinua kichwa chake juu na kukaza macho yake kama mtu anayetazama kitu kabla ya macho yake kuwa mazito na kope kufunga na kupitiwa na usingizi mzito. Hali hii hufuatiwa na kuanguka kwa ghafla na wakati mwingine kujiumiza mwili. 

Shambulizi la degedege huchochewa na vitu tofauti kidogo na vile vinavyochochea degedege  linalowapata kwa mfano watoto wenye kifafa. Imeripotiwa na baadhi ya wakazi wa maeneo yaliyokumbwa na ugonjwa huu kuwa, baadhi ya watoto walikumbwa na degedege baada ya kutokea mabadiliko ya hali ya hewa au baada ya kuoneshwa chakula ambacho hawajawahi kula hapo kabla. 

Dalili nyingine ni pamoja na kitendo cha watoto kupoteza ufahamu wa wapi walipo, kuzurura zurura bila kujielewa na wakati mwingine kupotea vichakani. Katika hali ya kushangaza yameripotiwa pia matukio ya baadhi ya watoto waliokumbwa na ugonjwa huu kuchoma moto nyumba za vijiji bila kujitambua, kuchanganyikiwa na kuwa kama walioumizwa kiakili na kihisia.

Mahudhurio yao shuleni huwa hafifu, lishe huzidi kuwa duni hatimaye watoto hupatwa na utapiamlo, magonjwa nyemelezi na hatimaye kifo.

Je, Tanzania ni salama?
Miaka kadhaa nyuma kumewahi kuripotiwa milipuko kadhaa ya ugonjwa huu katika nchi za Tanzania, Liberia na Sudan lakini haikuwa mpaka mwaka 2009 ndipo mamlaka za Afya duniani zilipouchukulia kwa uzito unaostahili pale kulipotokea mlipuko wa kwanza mkubwa huko nchini Uganda. 

Miaka kadhaa nyuma kumewahi kuripotiwa matukio ya ugonjwa wenye dalili zenye kufanana na huu huko nchini Tanzania [4], ingawa ugonjwa huu wa sasa wenye kuhusisha kutikisa kichwa umeripotiwa zaidi maeneo ya Sudan ya kusini na Uganda Kaskazini hususani kwenye maeneo fulani fulani [2, 3, 5].

Hivi sasa, timu ya watafiti kutoka shirika la Afya Duniani (WHO), mamlaka za Afya za Uganda pamoja na wataalamu kutoka kituo cha magonjwa ya maambukizi (CDC) cha nchini Marekani ipo nchini Uganda ikifanya utafiti kufahamu chanzo cha ugonjwa huu na jinsi ya kuutibu. 

Nini hasa chanzo cha ugonjwa huu?
Chanzo halisi cha ugonjwa huu bado hakijafahamika ingawa kuna fununu fununu za hapa na pale. Watalaamu wamependekeza mambo mbalimbali kuwa yawezekana yakawa visababishi vya ugonjwa huu, yakiwemo maambukizi ya vimelea mbalimbali, ukosefu wa lishe, mazingira, na sababu za kisaikolojia. Wengine walikwenda mbali zaidi na kupendekeza uhusiano wa mabadiliko katika muundo wa vinasaba, maambukizi ya virusi wa surua, ulaji wa nyama ya nyani, matumizi ya vyakula vya msaada au hata mbegu za msaada kuwa yanaweza kuwa chanzo cha ugonjwa huu ingawa hakuna uthibitisho wa madai hayo mpaka sasa [2,3,5]. 

Wataalamu kutoka shirika la Afya Duniani wanasema karibu asilimia zaidi ya 90 ya watoto waliokumbwa na ugonjwa huu walikuwa wakiishi kwenye maeneo maarufu sana kwa ugonjwa wa upofu (river blindness) unaosababishwa na vimelea wanaojulikana kama Onchocerca Volvulus ambao husambazwa na aina fulani ya mbu [2,3,5]. 

Hata hivyo, November 2010, jopo la watafiti wa WHO lilifika eneo la kaskazini mwa Uganda kufanya uchunguzi wa chanzo na dalili za ugonjwa huu. Katika uchunguzi wao wa awali, walifanikiwa kuorodhesha watoto 38 waliokumbwa na ugonjwa huu na wale wasio na ugonjwa, na kuchunguza kama wana maambukizi ya vimelea vya Onchocerca volvulus ambapo vimelea hivi vilionekana zaidi kwa watoto waliokuwa na ugonjwa (76%) wakati ni 47% tu ya watoto wasiokuwa na ugonjwa wa kusinzia ndiyo waliokutwa navyo. Uchunguzi wao wa kistatistiki haukuonesha uhusiano wowote kati ya ugonjwa huo na vimeleo hivyo. Hali iliyoonesha kuwa pamoja na kwamba ugonjwa wa onchocerca ulikuwa umeenea sana eneo hilo, haikuweza kuthibitika moja kwa moja iwapo ugonjwa huo ulikuwa chanzo cha ugonjwa wa kusinzia [1]. 

Juu ya hilo, watoto wengi wenye ugonjwa huu walikutwa pia na upungufu mkubwa wa Vitamin B6,  aina ya vitamini ambayo ni muhimu sana katika kuimarisha mfumo wa fahamu. 

Aidha uchunguzi zaidi unaonesha kuwa lishe duni pia inawezekana ikawa chanzo kimojawapo au kihatarishi cha mtoto kupatwa na ugonjwa huu. 

Ukubwa wa tatizo
Kutokana na taarifa zisizothibitishwa zilizopatikana kutoka kwa wafanyakazi wa afya walio maeneo yaliyoathiriwa na ugonjwa huu, waathirika ni watoto walio kati ya umri wa mwaka 1 mpaka 19, ingawa kundi la watoto wenye umri wa kati ya miaka 3 mpaka 11 huathirika zaidi, na tayari umesharipotiwa katika nchi za Liberia, sudan ya Kusini, Guinea ya Ikweta, [2] na sehemu za kaskazini za Uganda na kusini mwa Tanzania [3,4]. Mlipuko huu wa sasa nchini Uganda umejikita zaidi maeneo ya kaskazini mwa nchi hiyo, ingawa haijathibitika bado kama ugonjwa huu unaambukizwa japokuwa wataalamu wa afya wanalichukulia hilo kwa uzito mkubwa wakitilia maanani hofu yao ya kusambaa kwa ugonjwa huo sehemu nyingine za dunia.

Ripoti kutoka baadhi ya vijiji vya maeneo ya kaskazini mwa Uganda zinasema kuwa karibu kila kaya imeripotiwa kuathiriwa na ugonjwa huu. Mpaka sasa haijulikani idadi kamili ya vifo vilivyosababishwa na ugonjwa huu ingawa kuna idadi kubwa tu ya watoto walioathiriwa vibaya kiasi cha kushindwa kujihudumia wenyewe na kuwaongezea mzigo wa huduma wazazi na walezi wao. 

Ugonjwa huu unatibiwaje?
Mpaka sasa hakuna tiba ya uhakika ya ugonjwa huu. Hii ni kwa vile wataalamu bado hawafahamu chanzo halisi cha ugonjwa na jinsi unavyoambukizwa. Maisha ya watoto katika maeneo yaliyoathirika yamekuwa ya mashaka sana na kuna ripoti za baadhi ya wazazi kutupa watoto wao kwa vile hawajui ni kwa jinsi gani wanaweza kuwasaidia. Hofu yao nyingine ni kuogopa kuambukizwa kwa vile hawajui ni kwa vipi ugonjwa huu husambaa.

Ni hapa majuzi tu, mamlaka za afya za nchini Uganda ziliona umuhimu wa kufungua kituo cha kwanza cha afya kwa ajili ya kuwahudumia watoto waliokumbwa na ugonjwa huu baada ya kipindi kirefu cha kusuasua kuchukua hatua, ingawa hakuna tiba inayojulikana wala chanjo iliyogundulika mpaka sasa. 

Hata hivyo katika hali ya majaribio, baadhi ya madaktari wameanza kutumia dawa za kutibu na kuthibiti kifafa kwa ajili ya kuthibiti na kutuliza degedege linaloambatana na ugonjwa huu ingawa mafanikio ya njia bado si ya kuridhisha sana, kwa vile wanasema njia hii husaidia tu kupunguza kasi ya kutokea kwa dalili na si kuzikomesha kabisa. 

Tanzania ijiandae
Ripoti zisithothibiitishwa kwamba tayari ugonjwa huu umeshaingia Tanzania au kuna uwezekano mkubwa ukavuka mipaka na kuingia nchini si jambo la kulichukulia kijuujuu hata kidogo. Ni wakati muafaka sasa mamlaka zinazohusika kujiweka tayari na kujiandaa kulikabili tatizo hili kabla au pindi mlipuko utakapotokea. 

Marejeo
1. Lul Reik, MD, Abdinasir Abubakar, MD, Martin Opoka, MD, Godwin Mindra, MD, James Sejvar, MD, Scott F. Dowell, MD, Carlos Navarro-Colorado, MD, Curtis Blanton, MS, Jeffrey Ratto, MPH, Sudhir Bunga, MD, Jennifer Foltz, MD, EIS officers, CDC. Nodding Syndrome — South Sudan, 2011 Weekly January 27, 2012 / 61(03);52-54. Inapatikana mtandaoni kupitia http://www.cdc.gov/mmwr/preview/mmwrhtml/mm6103a3.htm
2. Nyungura JL, Akim T, Lako A, Gordon A, Lejeng L, William G. Investigation into nodding syndrome in Witto Payam, Western Equatoria State, 2010. Southern Sudan Medical Journal 2010;4:3–6.
3. Winkler AS, Friedrich K, Konig R, et al. The head nodding syndrome—clinical classification and possible causes. Epilepsia 2008;49:2008–15.
4. Winkler AS, Friedrich K, Meindl M, et al. Clinical characteristics of people with head nodding in southern Tanzania. Trop Doct 2010;40:173-5. 
5. Lacey M. Nodding disease: mystery of southern Sudan. Lancet Neurol 2003;2:714.

 


Ukurasa 3 ya 3