Image

Katika sehemu hii ya pili ya muendelezo wa makala ya magonjwa ya zinaa tutazungumzia kuhusu ugonjwa wa Chlamydia.

Chlamydia ni nini?

Chlamydia ni aina ya ugonjwa wa zinaa unaosababishwa na bakteria aina ya Chlamydia trachomatis ambao wanaweza kuathiri viungo vya uzazi na pia husababisha aina ya homa ya mapafu ijulikanayo kama atypical pneumonia.

Miongoni mwa magonjwa ya zinaa yasababishwayo na bakteria, Chlamydia unaoongoza kwa maambukizi duniani ambapo kwa nchi ya Marekani pekee inakisiwa watu milioni 4 huambukizwa kila mwaka. Kutokana na ukosefu wa takwimu za nchi nyingi barani Afrika ikiwemo Tanzania, ni vigumu kujua idadi kamili ya maambukizi, ingawa bila shaka ndio ugonjwa wa zinaa utokanao na bakteria unaoongoza kwa maambukizi ukifuatiwa na ugonjwa wa gonorrhea.

Clamydia huambukizwaje?

Chlamydia huambukizwa kupitia njia zifuatazo

  • Kujamiana kwa njia ya mdomo, njia ya haja kubwa na kupitia tupu ya mwanamke
  • Kuambukizwa kutoka kwa mama kwenda kwa mtoto wakati wa ujauzito
  • Au kupitia manyoya au vinyesi vya wanyama kama ndege walioambukizwa aina ya Chlamydia inayopatikana kwa ndege kama vile kuku, bata, kasuku nk. Aina hii ya clamydia husababisha aina ya homa ya mapafu ijulikanayo kama psittacosis ambayo huambatana na homa kali yenye nyuzi joto kati ya 39.4 - 41.1 celsius

Chlamydia huathiri sehemu tofauti za mwili wa binadamu kama vile macho, mfumo mzima wa kupumua, sehemu za siri, viungo vya uzazi na tezi (lymph nodes). Chlamydia na gonorrhea huwa na tabia ya kuambatana kwa pamoja (rejea makala ya magonjwa ya zinaa sehemu ya kwanza).

Dalili na viashiria vya ugonjwa wa Chlamydia

Asilimia 75 ya wanawake na asilimia 50 ya wanaume wanaopata maambukizi ya ugonjwa huu huwa hawaoneshi dalili zozote za ugonjwa wa Chlamydia. Dalili hutokea wiki 1 hadi 3 baada ya mtu kupata maambukizi.

Dalili kwa wanawake zinaweza kuwa

  • Kutokwa na majimaji ya rangi ya njano yenye harufu kali na mbaya sehemu za siri
  • Maumivu wakati wa kukojoa (haja ndogo)
  • Kuhisi kama kuwaka moto wakati wa kukojoa
  • Kutokwa na damu katikati ya kipindi cha hedhi yaani baada ya kumaliza mzunguko wa hedhi na kabla ya kuanza mzunguko mwengine wa hedhi
  • Maumivu sehemu ya chini ya tumbo
  • Maumivu wakati wa kujamiana
  • Kutokwa na damu wakati wa kujamiana
  • Kuvimba na maumivu kwenye tezi zilizopo sehemu za siri

Dalili kwa wanaume zinaweza kuwa

  • Maumivu wakati wa kukojoa
  • Kuhisi kama kuwaka moto wakati wa kukojoa
  • Kutokwa na majimaji kwenye uume yanayoweza kuwa ya rangi nyeupe kama maziwa, kijivu au ya njano
  • Sehemu ya tundu la uume huwa jekundu, huvimba na kuwasha
  • Maumivu kwenye korodani
  • Tezi zilizopo sehemu za siri huvimba na huambatana na maumivu

Mara nyingi dalili hizi kwa wanaume zinakuja na kupotea au zinaweza kuonekana tu wakati anaenda kukojoa asubuhi baada ya kuamka kutoka usingizini

Dalili za ugonjwa huu kama umeathiri puru (rectum) ni kama ifuatavyo (kwa wanawake na wanaume)

  • Kuwashwa na kutokwa na damu kwenye puru
  • Maumivu wakati wa kujisaidia haja kubwa
  • Kutokwa na uchafu kama kamasi kwenye puru

Dalili za chlaymdia iliyoathiri macho (kwa wanawake na wanaume)

  • Kuvimba sehemu za macho
  • Macho kuwa mekundu, kuwasha na hata kutokwa na majimaji

Chlamydia inayoambukiza kwenye macho (Chlamydia conjunctivitis or trachoma) ndio inayoongoza kwa kusababisha upofu duniani.

Vipimo vya uchunguzi

  • Urethral swab for culture – Majimaji kutoka kwenye uume au uke huchukuliwa kwa kutumia swab maalum ambapo hupelekwa maabara ili kuotesha na kuangalia aina ya uoto wa bakteria
  • Urinalysis (urine test) – Vipimo vya mkojo
  • Polymerase Chain Reaction (PCR) – Kipimo cha kuangalia vinasaba vya bakteria na hufanyika maabara.

Tiba ya ugonjwa wa Chlamydia

Chlamydia ni kati ya magonjwa ya zinaa yanayotibika. Ugonjwa huu hutibiwa kwa dawa aina ya antibiotics zilizopo kwenye makundi ya ;

  • Macrolide antibiotics
  • Quinolones antibiotics
  • Polyketides antibiotics

Madhara ya ugonjwa huu

  • Kwa wanaume, Chlamydia huathiri korodani na kusababisha mwanamume kukosa uwezo wa kutia mimba mwanamke (infertility) na maambukizi
  • Maambukizi kwenye tezi dume (prostatitis)
  • Kwa wanawake, husababisha maambukizi kwenye mirija ya uzazi, mfuko wa uzazi, na mayai ya uzazi hivyo kusababisha ugonjwa aina ya Pelvic inflammatory disease (PID). Pia huongeza asilimia ya mwanamke kupata mimba zinazotunga nje ya mfuko wa uzazi (Ectopic pregnancy). Mbali na hilo, mwanamke hupata maumivu sugu ya kwenye nyonga, ugonjwa wa mifupa arthritis aina ya Reiters syndrome. Vilevile, Chlamydia huweza kusababisha ugumba kwa mwanamke kama hatapata tiba.
  • Kwa wajawazito, Chlamydia husababisha wanawake kujifungua kabla wakati. Mtoto anaweza kuzaliwa na maambukizi kwenye masikio, sehemu za siri, macho na kwenye mapafu (homa ya mapafu). Kama mtoto hatapata tiba ya haraka ya macho basi anaweza kuwa kipofu.

Dalili za Chlamydia kwa watoto wachanga hutokea ndani wiki mbili kwenye macho na homa ya mapafu (pneumonia) ndani ya wiki 2 hadi miezi 3 baada ya kuzaliwa.

Jinsi ya kujikinga na ugonjwa wa Chlamydia

  • Kama ilivyoelezwa kwenye makala iliyopita, njia sahihi ya kujikinga na magonjwa ya zinaa ni kuacha au kuepuka kufanya ngono au kujamiana.
  • Kwa wanawake wajawazito, ni vizuri kuhudhuria kliniki mapema wakati wa ujauzito
  • Wale wenye maambukizi wanashauriwa kuchukua tahadhari ya kutowaambukiza wapenzi wao kwa kufanya ngono salama (kutumia mipira), kuepuka kushika macho kwa kutumia mikono na hata ikiwezekana kuwaepuka wapenzi wao ili kuwalinda na maambukizi.
  • Kwa wale ambao wapenzi wao wameambukizwa au wameonyesha dalili za ugonjwa huu, wanashauriwa na wao kupata tiba hata kama hawana dalili zozote.
 

Madhara ya ugonjwa wa kaswende katika mfumo wa mishipa ya fahamu hutokea miaka 10-20 baada ya mtu kuugua ugonjwa wa kaswende na ambaye hakupata tiba yoyote hapo awali. Madhara haya huonekana kwenye uti wa mgongo na kwenye ubongo.

Kuna aina nne ya neurosyphilis kama ifuatavyo

  • Isiyo na dalili (Asymptomatic) – Katika aina hii mgonjwa anakuwa hana dalili zozote. Aina hii ndio huonekana sana kwa wagonjwa ambao hawakupata tiba hapo awali.
  • Ulemavu wa jumla (General paresis)
  • Inayoshambulia tando za ubongo na mishipa ya damu (Meningovascular)
  • Inayoshambulia sehemu za chini za uti wa mgongo (Tabes dorsalis)

General paresis hutokana na kuathirika kwa ubongo na hivyo kuleta upungufu katika ufanyaji kazi wa ubongo (impairement of mental function). Aina hii pia huweza kutokea kwa wagonjwa wa kisonono (gonorrhoea).

Dalili za general paresis

  • Kupungua uwezo wa kuzungumza (aphasia)
  • Kupungua uwezo wa kufanya maamuzi (impaired judgement)
  • Kutokuwa na uwezo wa kuhesabu kitu chochote
  • Kupungua kuhamasishika (impaired motivation)

Ugonjwa wa matende ni aina ya ugonjwa unaosababisha ngozi na  tishu zilizo chini ya ngozi ya  mwanadamu kuwa nene (thickening of skin and underlying tissue).Ugonjwa huu  huathiri  miguu, mikono, figo,  korodani  na kusababisha korodani  kuvimba na kuwa kubwa sana.Inakisiwa watu milioni 120 duniani wana maambukizi ya ugonjwa huu ambapo kati yao milioni 40 wamepata madhara makubwa kutokana na ugonjwa huu.Kati ya hawa walioathirika theluthi moja huapatikana katika bara la Afrika, theluthi moja nyingine hupatikana India, na kiwango kilichobakia hupatikana katika  visiwa vya Pacific, Marekani na Asia ya kusini.

Ugonjwa wa matende husababishwa  na vimelea aina ya minyoo (parasitic worm) vinajulikana kama Wuchereria bancrofti, Brugia malayi, B. timori ambavyo huenezwa na mbu jike aina ya  culex quinquefasciatus mosquitoes na jamii fulani ya mbu dume (Anopheles species) wakati minyoo aina ya  Brugia roundworms huenezwa mbu wanaojulikana kama  Mansonia mosquitoes. Mbu hawa hueneza ugonjwa huu kutoka kwa mtu mmoja kwenda kwa mwengine.
 
Aina nyingine ya ugonjwa wa matende inayojulikana kama nonparasitic elephantiasis au podoconiosis ambayo haisababishwi na vimelea vyovyote hupatikana katika nchi za Afrika Mashariki (Kenya, Uganda, Tanzania, Rwanda, Burundi) Sudan, Egypt na Ethiopia. Asilimia 6 ya maambukizi ya aina hii ya podoconiosis hupatikana nchini Ethiopia.

Nini hutokea baada ya maambukizi?

Kwa kawaida mtu aliyeambukizwa ugonjwa huu huwa na mabuu (larvae) kwenye mfumo wa damu mwilini mwake wanaojulikana kama microfilariae. Mabuu haya husafiri kutoka kwenye mfumo wa damu hadi kwenye mfumo mwingine unaojulikana kama mfumo wa limfu (lymphatic system) na kukua kuwa minyoo kamili (adult worms) ambayo huziba mfumo huu wa limfu ambao unategemewa sana katika kuweka uwiano sawa  wa maji (fluid balance) kati ya mfumo wa damu na tishu ndani ya mwili na husaidia kuupa mwili kinga dhidhi ya magonjwa mbalimbali. Minyoo hii huishi kwa miaka minne hadi sita na katika uhai wake huzaa mamilioni ya mabuu (microfilariae)  mengine wakati ikiwa kwenye mfumo wa damu.

Mbu huenezaje ugonjwa huu?

Mtu ambaye ameambukizwa ugonjwa huu huwa na mabuu kwenye mfumo wake wa damu na anapongatwa na mbu ambawo wanauwezo wa kuchukua mabuu haya  ambayo  huendelea kukua na kufikia hatua ya kuambukiza mtu mwingine ndani ya mwili wa mbu.Kwa kawaida, ukuaji huu wa mabuu ndani ya mwili wa mbu huchukua wiki moja hadi tatu na baada ya kukua na kufikia hatua ya kuambukiza mtu mwingine, mabuu haya husogea mpaka kwenye sehemu ya mdomo wa mbu ambayo ndio huwa humng'ata mtu wakati mbu anapofyonza damu kutoka kwa mtu. Mbu mweye mabuu kwenye mdomo wake anapomngata mtu ili kufyonza damu, ndipo mabuu haya yanapoingia kwenye mwili wa mtu na hivyo kusababisha maambukizi ya ugonjwa huu.

Dalili za ugonjwa huu ni zipi?

• Dalili kubwa ya ugonjwa huu ni kuvimba sehemu ya chini ya mwili yaani kwenye miguu na vidole.Pia mtu anaweza kuvimba sehemu ya mikono au mkono wote pamoja na vidole vya mkononi. Wengine huvimba kwenye korodani (wanaume).
• Kuhisi uzito na kukamaa kwa mikono au miguu kutokana na uvimbe uliopo.
• Kutoweza kutumia kiungo husika kilichovimba.
• Maumivu au kutohisi vizuri kwenye mikono au miguu.
• Kupata maambukizi ya mara kwa mara kwenye sehemu iliyovimba.
• Ngozi kuwa nene na ngumu kwenye mikono au miguu.

Dalili nyingine ni pamoja na

  • Homa
  • Maumivu ya kichwa
  • Maumivu kwenye jointi na mifupa 
  • Kutapika
  • Vidonda kwenye mikono au miguu
  • Mistari ya rangi nyekundu inayoonekana kwenye mikono au miguu (red streaks)

Vipimo vya uchunguzi

• Blood examination under microscope - Kipimo cha kuangalia damu kwenye hadubini  ili kuangalia kama kuna mabuu ya ugonjwa huu wa matende.Kwa wale ambao wana ugonjwa huu kwa muda mrefu, mabuu hayaonekani kwenye damu kwani tayari yatakuwa yameshaingia kwenye mfumo wa limfu. Hivyo, kutoonekana kwa mabuu kwenye damu kwa kutumia hadubini si kigezo cha kusema kwamba mgonjwa hana ugonjwa huu wa matende.
• Vipimo vyengine vinavyoweza kutumika ni pamoja na CT Scan, MRI, Doppler Ultrasound, Radionuclide Imaging ili kuweza kutofautisha ugonjwa huu na magonjwa mengine yanayosababisha kuvimba kwa miguu au mikono kama saratani za  aina mbalimbali, kuganda kwa damu kwenye mishipa ya damu (blood clot) na kadhalika.
• Kwa wale wenye kuvimba korodani, ni muhimu kwa daktari  kuchukua kipimo kwa kukwangua sehemu husika kisha kuchanganya na potassium hydroxide na kutazama kwenye hadubini kama kuna dalili (Meddler bodies, sclerotic bodies)  za ugonjwa wa fangasi unaojulikana kama chromobalstomycosis  (unaosababishwa na fangasi aina ya Fonsecaea pedrosoi, Phialophora verrucosa, Cladosporium carrionii, au Fonsecaea compacta). Pia ukungu huu huweza kuoteshwa maabara ili kuangalia kama kuna fangasi aina yoyote ile niliyotaja hapo juu watakaota.

Tiba ya ugonjwa wa matende ni nini?

Tiba ya ugonjwa wa matende hutegemea na sehemu husika. Kwa wagonjwa walio katika jangwa la sahara, tiba ni dawa aina ya albendazole pamoja na ivermectin. Kwa wagonjwa waliopo sehemu nyingine duniani tiba huusisha matumizi ya albendazole pamoja na diethylcarbamazine.
 
Kusafisha sehemu iliyoathiriwa na ugonjwa wa matende mara kwa mara husaidia kupunguza dalili na viashiria vya ugonjwa huu.
 
Kwa wale waliovimba korodani kutokana na ugonjwa wa matende, tiba yake ni upasuaji.Wakati mwingine, kama mgonjwa atakuwa amevimba sana korodani, basi baada ya kufanyiwa  upasuaji wa kawaida, atahitaji kufanyiwa upasuaji kurekebishwa ngozi yake (plastic surgery).
 
Katika utafiti uliofanywa na chuo cha Liverpool school of tropical medicine mwaka 2005, umeonyesha dawa ya antibiotiki hususan doxycyline inaweza kutumika kutibu ugonjwa huu wa matende kutokana na  minyoo (adult worms) kuwa na bakteria aina ya wolbachia wanaoishi ndani ya minyoo hii, hivyo dawa hii hutibu kwa kuua bakteria hawa na kusababisha minyoo hii kufa, na kuondosha kabisa microfilariae kwenye damu ya mgonjwa na  hivyo mgonjwa kupona. Dawa hii hutumika kwa muda wa wiki 8. Hata hivyo, kama mgonjwa atakuwa na mabuu ndani ya mfumo wake wa limfu, basi itakuwa vigumu kwake kupona. Utafiti zaidi unahitajika ili kuwa na uhakika zaidi juu ya dawa hii kutibu ugonjwa huu.

Kinga ya ugonjwa wa matende ni nini?

• Shirika la afya duniani (WHO) limeanzisha jitihada za kutokomeza ugonjwa huu wa matende ifikapo mwaka 2020.
• Matumizi ya  dawa aina ya albendazole kwa wale walio katika hatari kupata ugonjwa wa matende unaosababishwa na vimelea.
• Kuvaa viatu wakati wa kutembea nje ili kujikinga kupata maambukizi ya aina ya podoconiosis.
• Kuosha miguu na mikono kwa kutumia maji na sabuni
• Kuosha miguu kila siku kwa kutumia antiseptic (bleach).

Marejeo

1. Nidhi Sharma, Y.S.Marfatia: Genital elephantiasis as a complication of chromoblastomycosis: A diagnosis overlooked, Indian J Sex Transm Dis. 2009 Jan-Jun; 30(1): 43–45.  
2. McNeil, Donald (2006-04-09). "Beyond Swollen Limbs, a Disease's Hidden Agony". New York Times. Retrieved 2008-07-17.
3. Davey, Gail (2008). "Podoconiosis: let Ethiopia lead the way". The Ethiopian Journal of Health Development 22 (1): 1–2.
 
 

Katika tafiti mpya zilizofanywa hivi karibuni zinaonyesha kuwa unyongovu na jaribio la kujiua ni viashiria hatari ambavyo huleteleza vijana kufa kwa magonjwa ya moyo.

Katika utafiti mkubwa uliohusisha washiriki zaidi ya 7000 walio chini ya miaka 40 ulionyesha kuwa kwa wale waliokuwa na historia ya unyongovu au jaribio la kujiua walikuwa na hatari kubwa zaidi ya kufa kutokana na magonjwa ya moyo hasa yale ambayo moyo hukosa oksijeni ya kutosha (ischemic heart disease) ukilinganisha na wale ambao hawakuwa na historia hiyo.

Ingawa jinsia zote zilikuwa kwenye hatari zaidi ya kufa kutokana na magonjwa ya moyo, lakini wanawake wenye unyongovu au waliofanya jaribio la kujiua walikuwa na hatari mara 14 zaidi ya kufa kwa magonjwa ya moyo yatokanayo na kukosa oksijeni ya kutosha (ischemic heart disease) kulinganisha na wale ambao hawakuwa na unyongovu au jaribio la kujiua.

Katika utafiti huu uliofanywa na Profesa Viola Vaccarino kutoka chuo kikuu cha Emory, Atlanta, Georgia aligundua jinsi matatizo ya kisaikolojia yanavyopelekea kuongeza hatari ya kufa mapema na magonjwa ya moyo katika idadi ya vijana.

Taarifa nyingi zilizopo za magonjwa ya moyo ambazo zilizokwisha tolewa huwa za umri wa kati na wazee, maana imekuwa ikizoeleka magonjwa haya huathiri zaidi rika hiyo, ambayo ni kweli kabisa hasa katika magonjwa yanao athiri zaidi mishipa ya damu ya moyo (CHD).

Naitwa Kissu K. Mpini, ni mwenyeji wa wilaya ya Ifakara,mkoa wa Morogoro, Tanzania, utakumbuka mara ya mwisho nilivyotoa ushuhuda wangu kuhusu shida ya kusigina/kusaga meno-bruxism ilivyonitatiza kwa muda mrefu bila kupata nafuu, kwa kifupi baada ya kupata huduma pale kwenye hospitali ya Taifa Muhimbili, Kitengo cha Meno, ninaendelea vizuri sana kwa sasa, ninalala usingizi vema, na kazi zangu nazifanya vizuri, hakika nimekuwa mwenye furaha kama wenzangu.

Utakumbuka nilijiuliza sana kama watoto pia hupata tatizo la kusigina meno kama inavyotokea kwa watu wazima, hivyo ili kukata mzizi wa fitina, nilimwandikia barua daktari aliyenihudumia pale Muhimbili siku ile, nimeona ni vema pia elimu aliyonipatia daktari nishirikishe wadau wengine, maana sio wote tunaweza kufika Muhimbili kirahisi, vilevile ninaamini kuwa yeyote atayeweza kusoma maelekezo haya ya daktari itakuwa ni msaada mkubwa sana kwake binafsi, familia na rafiki zake. Majibu ya daktari yamebainisha kwa kirefu kuhusu tatizo la kusigina meno linavyoathiri watoto, ifuatayo ni barua ya daktari kama alivyoniandikia.

Tafiti zinaonesha kuwa asilimia 20 ya watoto kati ya mwaka 1 hadi miaka 11 husumbuliwa na kusigina/kusaga meno tatizo ambalo kwa kitaalamu linajulikana kama Bruxism. Ingawa takwimu hii inakadiriwa kuwa chini ya hali halisi kwa vile wazazi wengi wanashindwa kutambua tatizo hili kwa watoto wao.

Kama ilivyo kwa watu wazima kwa vyanzo mbalimbali vinavyosababisha kusigina meno, kwa watoto dalili za tatizo hili zinafanana sana na matatizo mengine ya watoto hivyo inawawia vigumu wazazi ama walezi kutambua tatizo hili na hata kupuuzia.

Fangasi wapo kila mahali, kwenye miti, mimea, mchanga, ndani majumbani mwetu na hata kwenye ngozi ya binadamu.Aina nyingi ya fangasi hawasababishi madhara yoyote kwa binadamu isipokuwa wachache tu. Kuna aina milioni moja na nusu za wadudu aina ya fangasi wanaotambulika duniani, kati yao ni fangasi 300 tu wanaojulikana kusababisha maambukizi kwa binadamu .1,2 Uvutaji wa hewa iliyochanganyika na  mazalia ya fangasi yanayojulikana kama fungal spores pamoja na uwepo wa uvamizi au ukuaji wa fangasi kwenye ngozi ya binadamu husababisha maambukizi ya fangasi, hivyo basi maambukizi mengi ya fangasi huanza kwenye  mapafu au kwenye ngozi ya mtu.

Takribani watu milioni 984 walipata maambukizi ya fangasi kwenye ngozi  mwaka 2010 na hivyo kufanya maambukizi haya kuwa ugonjwa namba nne katika magonjwa yote kwa mwaka huo 3.

Watu walio kwenye hatari ya kupata maambukizi ya fangasi ni kama wafuatavyo;

  • Wagonjwa wanaotumia dawa za kuua vimelea vya wadudu bila kufuata masharti ya daktari -Dawa aina ya antibayotiki (antibiotics)
  • Wale wenye kinga dhaifu - Wagonjwa wa ukimwi,wagonjwa wa kisukari, wagonjwa wanaotumia dawa za jamii ya steroid, wagonjwa wanaotumia dawa za kutibu saratani (chemotherapy drugs), immunosuppressive drugs, wagonjwa wanaotibiwa kwa mionzi na  wajawazito
  • Watoto wadogo na wazee - Ingawa watu wote wapo kwenye hatari ya kupata maambukizi ya fangasi, hatari kubwa ipo kwenye kundi hili la wazee na watoto kutokana kuwa na kinga dhaifu

Aina za maambukizi ya fangasi

  1. Maambukizi ya fangasi nje ya mwili (Superficial mycoses) - Ni fangasi ambao husababisha maambukizi kwenye ngozi, nywele, kucha na hawaishi kwenye tishu mwilini. Fangasi aina hii hujulikana kama Dermatophytes.Fangasi hawa hushambulia sehemu tajwa hapo juu kwa kutoa vimengenyo (Extracellular enzymes) vinavyolainisha protini aina ya keratin inayopatikana katika maeneo hayo.Maambukizi haya ya fangasi yamegawanyika katika
  2. Tinea Corporis - Maambukizi ya fangasi yanayopatikana katika sehemu yoyote ile mwilini.
  3. Tinea Pedis (Athlete’s foot)-Maambukizi ya fangasi katikati ya vidole vya miguuni na kwenye nyao za miguu
  4. Tinea Unguium (Onchomycosis) - Maambukizi haya yanapatikana kwenye kucha za vidole vya miguuni na vya mikononi
  5. Tinea Capitis – Huonekana kwenye kichwa hasa kwa watoto wadogo.Husababisha mapunye kwenye kichwa, nywele kunyofoka, mabaka meusi kwenye kichwa yaliyoambatana na mcharuko (Inflammation), kutokwa na magamba kichwani, kuwashwa na kuvimba vimba  kwenye kichwa
  6. Tinea Cruris – Maambukizi ya fangasi sehemu za siri
  7. Tinea Barbae – Huonekana maeneo yenye ndevu kwenye uso na shingoni
  8. Tinea Vesicolor – Maambukizi ya fangasi kwenye ngozi ya watu wazima.Maambukizi haya hayaonekani kwenye uso ila husababisha ngozi kuwa na mabaka yenye rangi ya kahawia iliyochanganyika na rangi nyekundu (reddish brown).Tinea vesicolor huonekana sana kwenye ngozi ya watu wanaoishi sehemu zenye joto kali au wenye matatizo kwenye vichocheo vya miili yao (hormonal abnormalities) ingawa wote wanaopata maambukizi haya huwa ni watu wenye afya njema.
  9. Subcutaneous Mycoses- Maambukizi ya fangasi kwenye tishu chini ya ngozi zinazojulikana kama dermis, subcutaneous tissue, fascia na kwenye misuli.Fangasi wanaosababisha maambukizi haya hupatikana kwenye mchanga na mimea.Maambukizi haya sugu hutokea pale mtu anapokuwa na kidonda na hivyo kurahisisha fangasi kuvamia mwili.Magonjwa yanayosababishwa na fangasi kwenye tishu chini ya ngozi ni kama yafuatayo;
  • Sporotrichosis
  • Chromoblastomycosus
  • Mycetoma
  • Phaeohypomycosis 

Sporotrichosis

Husababishwa na fangasi aina ya Sporothrix schenckii.Fangasi hawa hupatikana kwenye mimea, miti, nyasi na kwenye maua aina ya waridi. Maambukizi yanayotokea kwenye mikono na miguu ingawa kwa watoto huonekana sana sehemu za usoni.Pia huweza kusambaa kwenye damu kwa watu wenye upungufu wa kinga mwilini. 

Ugonjwa wa kaswende ni ugonjwa wa zinaa unaosababishwa na bakteria aina ya Treponema pallidum.  Ugonjwa wa huu ni kati ya magonjwa ya zinaa yanayoongoza kwa kusababisha madhara mengi.

Maambukizi ya kaswende wakati wa ujauzito huleta madhara mengi sana kama kujifungua kiumbe ambacho kimeshakufa, mtoto kuathirika na ugonjwa huu wakati wa kuzaliwa, mtoto kupata matatizo wakati wa   ukuaji wake, degedege na kuongezeka kwa vifo vya watoto wachanga nchini. 

Ugonjwa wa kaswende huathiri zaidi ya mimba millioni moja duniani kote kila mwaka na huchangia theluthi mbili ya vifo vya watoto wale wanaozaliwa tayari wameshakufa katika nchi za maeneo ya jangwa la sahara. Asilimia 30 ya mimba zinazoathiriwa na kaswende huishia watoto kufariki wakati wa kuzaliwa. Asilimia nyengine 30 ya mimba zinazoathiriwa na kaswende husababisha watoto kuzaliwa na ugonjwa huu wa kaswende, kupata matatizo ya ukuaji wao, degedege na kuongeza vifo vya watoto kwa asilimia 50.

Taasisi ya  kudhibiti Ugonjwa wa Ukimwi Tanzania (Tanzania National AIDS Control Programme) au NACP imesema maambukizi yote ya kaswende wakati wa ujauzito Tanzania bara kati ya mwaka 2003 hadi 2004 ni asilimia 6.7, kutoka asilimia 0.4 kwa mkoa wa Kilimanjaro hadi asilimia 32 kwa mkoa wa Tabora katika ripoti yake ya utafiti uliofanywa chini ya Wizara ya afya na ustawi wa jamii. Maambukizi yalionekana yako juu zaidi kwa wanawake walio na umri wa miaka 35 na zaidi (7%) na kiwango cha maambukizi kuwa chini zaidi kwa wanawake walio na umri kati ya miaka 15 – 24 (6.5%).

Ugonjwa wa ukimwi na kaswende mara nyingi huambatana pamoja. Ugonjwa wa kaswende huongeza uwezekano wa mtu kupata ugonjwa wa ukimwi.

Makala ya leo ni muendelezo wa magonjwa ya moyo ya kuzaliwa nayo, na ugonjwa wa leo hujulikana kama Tundu katika moyo, au Tundu katika kuta za ventrikali za moyo, ni ugonjwa ambao hutokea mara nyingi zaidi.

Watoto wenye tundu dogo katika moyo, huweza kukua bila matatizo yoyote, wakati wale wenye tundu kubwa huanza kuonesha dalili mapema

Vifuatavyo ni vihatarishi ambavyo vinaweza kupelekea kupata tundu katika kuta za chini za moyo

  • Maambukizi ya Rubella katika kipindi cha ujauzito
  • Ugonjwa wa kisukari ambao haujadhibitiwa kwa mama mjamzito
  • Matumizi ya pombe au madawa ya kulevya na baadhi ya dawa za hospitali katika kipindi cha ujauzito

Dalili

  • Rangi ya ngozi, midomo na kucha hubadilika na kuwa bluu
  • Kunyonya au kula kwa shida sana, na ukuaji wa shida
  • Kupumua kwa shida
  • Kuchoka haraka
  • Kujaa miguu na kuvimba tumbo
  • Mapigo ya moyo ya haraka
  • Kwa mtaalamu anaweza kusikia ishara ya ongezeko la sauti ya ziada ya mapigo ya moyo ya mtoto hali ambayo wataalamu huiita holosystolic murmur kwa kutumia kifaa kitaalamu stethoscope

Moja ya madhara ya ugonjwa wa kisukari katika mwili wa binadamu ni ugonjwa wa figo (diabetic nephropathy). Ugonjwa huu ambao huwapata watu wenye kisukari, hutokea muda mrefu baada ya mtu kugunduliwa kuwa na kisukari.

Kinachotokea (Pathofiziolojia)

Figo zinaundwa na mamia kwa maelfu ya vijiumbo vidogo vidogo viitwavyo nefroni (nephrons). Kazi ya hizi nefroni ni kuchuja damu na kutoa uchafu mwilini mwako kwa njia ya mkojo.

Kwa watu wenye kisukari, nefroni huwa na tabia ya kukakamaa, kuzeeka na kuwa na makovu kadiri miaka inavyopita. Baada ya muda fulani, hushindwa kabisa kazi yake ya kuchuja uchafu, matokeo yake protini ambazo kwa kawaida huwa haziwezi kuchujwa, huchujwa na kutoka katika mkojo.

Chanzo hasa cha kuzeeka, kukamaa na kuwa makovu huku kwa nefroni hakijulikani. Hata hivyo inadhaniwa kuwa uthibiti mbaya wa sukari husababisha uharibifu wa figo, na madhara huongezeka maradufu kwa watu wenye shinikizo la damu lisilothibitiwa na kisukari kwa pamoja.

Kuharibika kwa chujio ama Glomerulonephritis ni aina ya ugonjwa wa figo unaoathiri sehemu maalum ya figo (chujio) inayohusika na uchujaji wa maji pamoja na uchafu kutoka katika damu. Sehemu hii huitwa glomelurus au chujio kama tutakavyokuwa tukitumia katika mada hii. 

Visababishi

Mara nyingi chanzo halisi cha kuharibika kwa chujio za figo (glomerulonephritis) huwa hakijulikani. Hata hivyo wakati mwingine uharibifu huu unaweza kusababishwa na kushambuliwa na mfumo wa kinga ya mwili. Uharibifu katika chujio husababisha damu pamoja na protini kuingia katika mkojo. 

Tatizo hili hukua kwa haraka na figo linaweza kupoteza uwezo wake wa kuchuja maji na uchafu kwa kasi ndani ya muda mfupi wa kati wiki chache mpaka miezi kadhaa. Aina hii ya kuharibika kwa chujio za figo kwa haraka hujulikana kitalaamu kama rapidly progressive glomerulonephritis. 

.

Ukubwa wa tatizo na vihatarishi vyake

Takribani robo ya watu wanaopatwa na tatizo sugu la glomerulonephritis huwa hawana historia ya kuwa na ugonjwa wowote wa  figo hapo kabla. 

Kuna mambo kadhaa yanayoweza kumfanya mtu awe katika hatari ya kupata glomerulonephritis. Mambo hayo ni pamoja na:

  • Matatizo katika mfumo wake wa damu au lymph
  • Kuwahi kutumia vimiminika vilivyotengenezwa kwa kemikali za hydrocarbon
  • Wenye historia ya saratani
  • Maambukizi ya bakteria aina ya streptococcus, virusi, majipu au maambukizi katika moyo 
  • Mambo mengine yanayoweza kuongeza hatari ya kupatwa na glomerulonephritis ni pamoja na:
  • Magonjwa ya mishipa ya damu kama vile vasculitis au polyarteritis
  • Matumizi yaliyopitiliza ya dawa za kutuliza maumivu za jamii ya Non steroidal anti-inflammatory drugs kama vile aspirin na diclofenac
  • Magonjwa ya mfumo wa kinga ya mwili kama vile Anti-glomerular basement membrane antibody disease na IgA nephropathy
  • Makovu katika chujio (Focal segmental glomerulosclerosis) au hali ya chujio kuwa na kuta nene kuliko kawaida (Membranoproliferative GN)
  • Magonjwa yanayoathiri viungo mbalimbali vya mwili kama vile Henoch-Schonlein purpura, IgA nephropathy, Goodpasture’s syndrome au Lupus nephritis 
  • Ugonjwa wa kimetaboliki wa Amyloidosis

 Dalili

Dalili kuu za glomerulonephritis ni kuwa na damu katika mkojo (hali inayoufanya mkojo kuwa na rangi kama nyeusi, kutu au samawati; mkojo kuwa kama wenye povu jingi (kwa sababu ya kuwa na protini nyingi kuliko kawaida) na kuvimba uso, macho, miguu au tumbo (hali inayojulikana kama edema) 

Ukurasa 5 ya 11