Katibu Mkuu Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Prof. Mabula Mchembe akifungua Mkutano wa Maafisa Afya mazingira uliofanyika Jijini Dodoma.
Maafisa Afya mazingira wakifuatilia kwa makini neno kutoka kwa Katibu Mkuu Wizara ya Afya (hayupo kwenye picha) wakati wa ufunguzi wa Mkutano wa tathmini wa Afya mazingira uliofanyika Jijini Dodoma.
TIMIZENI WAJIBU WENU KWA WELEDI NA MAADILI.
Na Rayson Mwaisemba, WAMJW- DOM.
KATIBU Mkuu Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Idara kuu ya Afya Prof. Mabula Mchembe amewataka Maafisa Afya ngazi zote kufanya kazi zao kwa weledi na kufuata maadili wakati watimizapo majukumu yao katika jamii.
Prof. Mchembe ameyasema hayo, wakati akifungua Mkutano wa Maafisa Afya mazingira wenye kauli mbiu ya "Zingatia mahitaji ya Jinsia kwa usafi wa mazingira endelevu " uliofanyika Jijini Dodoma.
"Tusimamie maadili sana, usitende kitu kwa kufikiria kwamba unamfanyia fulani, natambua changamoto zipo katika baadhi ya sehemu, lakini tunahitaji kutimiza wajibu wetu kwa maadili na uwaminifu wa hali ya juu" alisema Prof. Mchembe.
Pia, Prof. Mchembe amewataka Maafisa Afya mazingira kusimamia usafi katika maeneo ya huduma za vyoo katika jamii, hususan katika ofisi na vituo vya daladala ambavyo huudumia Jamii kwa kiasi kikubwa ili kuikinga Jamii dhidi ya magonjwa ya milipuko.
Aidha, Prof. Mchembe amewaagiza Maafisa Afya mazingira nchini kusimamia usafi na ubora wa vyakula katika maeneo yote yanayotoa huduma za vyakula, yakiwemo maeneo ya migahawa na hoteli ili kuikinga jamii na magonjwa ya tumbo na kuhara.
Mbali na hayo Prof. Mchembe ametoa wito kwa Maafisa afya mazingira kujiepusha na vitendo vya Rushwa wakati wa wakitimiza majukumu yao na kuhakikisha usafi wa mazingira unaendelea kufuatwa katika ngazi zote za Jamii.
"Tuachane na Rushwa, inawezekana baadhi ya sehemu unafika pale, unapewa 10,000 au unapewa bia mbili au tatu unaondoka zako, kitu ambacho hakina maana, sasa kama wewe ni Mtaalamu wa Afya simama kwenye maadili yako" alisema Prof. Mchembe.
Hata hivyo, Prof. Mchembe amewaagiza Maafisa afya mazingira nchini, kusimamia udhibiti wa takataka zinazotokana na utoaji wa huduma za afya ili kuendelea kuikinga jamii dhidi ya maambukizi yatokanayo na taka hizo.
Naye Kaimu Mganga Mkuu wa Serikali, ambae pia ni Mkurugenzi wa huduma za Kinga Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Dkt. Leonard Subi amewaagiza Waganga wakuu wa mikoa kutoa elimu mara kwa mara kwa watendaji wao juu ya maadili badala ya kusubiri kuchukua hatua baada ya kosa