Image

Dawa za kuongeza makalio ni kitu kilichopata umaarufu wa ghafla miongoni mwa kina dada wengi duniani na hata katika jamii yetu. Siku hizi haishangazi kusikia dada mwenye makalio makubwa au yenye umbo duara akiambiwa kuwa anatumia dawa za kunenepesha makalio au ‘wowowo’ au 'zigo' kama wanavyopenda kuita vijana kwa kiswahili cha mtaani. Aidha matangazo juu ya dawa hizi nayo yamekuwa yakiongezeka kila kukicha. Leo hii ukienda kwenye mitandao ya kijamii kuna matangazo mengi sana ya dawa zenye kuongeza makalio na matiti. Pamoja na kwamba kuna simulizi tofauti juu ya faida na madhara ya matumizi yake, idadi ya watumiaji inazidi kuongezeka siku hadi siku.

Lakini dawa za kuongeza makalio ni nini hasa? Kwa ujumla hizi ni dawa zitumiwazo na akina dada na mama kwa ajili ya kunenepesha na kuongeza ukubwa wa makalio yao na kuyafanya yawe na umbo wanalodhani linawavutia wao au/na wapenzi wao. Ukisoma maelezo ya dawa hizi, nyingi hudai kuwa na uwezo wa kuboresha umbo la makalio kwa kuyafanya yawe na muonekano wa ujana zaidi, duara, laini na yenye mvuto.

Wanawake karibu dunia nzima huamini maelezo kuwa dawa hizi zina uwezo wa kuwajengea maumbo wanayoyatamani. Wengi, kuanzia watu mashuhuri (celebrities) mpaka watu wa kawaida, wanataka makalio makubwa; yale maumbo madogo na makalio ‘yasiyojazia’ hayana nafasi tena. Wanaamini kuwa makalio ‘yaliyojazia’ yanafanya hata nguo kukaa vema mwilini, huwafanya wanaume kugeuza shingo kuwashangaa (labda kuwatamani pia) na wengine hudai yanasaidia kuongeza mvuto wa ngono kwa wapenzi wao.

Hakuna ubaya wowote kwa mtu kutaka kupendeza. Swala la kuonekana mzuri au kuwa mtanashati limekuwa sehemu muhimu kwa maisha ya binadamu hususani upande wa dada zetu. Si kitu cha ajabu maana tangu enzi za mababu , tunasoma katika historia jinsi mwanamke alivyosifiwa kwa uzuri na urembo wake.

Swala la uzuri na urembo wa mwanamke linajadiliwa mara nyingi katika aya mbalimbali za misahafu ya dini zetu, kuonesha ni jinsi gani ambavyo hata Mungu mwenyewe anavyouthamini uzuri na urembo wa mwanamke. Si ajabu kuona jinsi ambavyo makampuni makubwa yanayojishughulisha na utengenezaji wa vipodozi na nguo, vitu ambavyo vinachangia sana katika kumfanya mwanamke aonekane mzuri na mrembo, yanavyotengeneza faida kubwa.

 Sikatai kwamba kuna uzuri wa kuzaliwa, la hasha. Ni dhahiri kabisa wapo watu waliojaliwa kuwa na muonekano mzuri ambao wamezaliwa nao. Na mtakubaliana na mimi kwamba kuna baadhi ya vitu katika miili yetu ambavyo hatuwezi kuvibadilisha hata kama hatuvipendi, lakini habari njema ni kwamba asilimia kubwa ya muonekano wa sura na miili yetu waweza kubadilishwa, na kuendana na matakwa yetu.

Siongelei wala sishauri utumiaji wa madawa au njia nyingine zenye madhara katika mwili wa binadamu. Bali naongelea jinsi ambavyo mfumo wa maisha waweza kukusaidia kupata muonekano unaoupenda bila kuwa na madhara yeyote ya kiafya katika mwili. Usifikirie sana, hapa naongelea vitu vya kawaida kabisa katika maisha yetu ya kila siku visivyo kuwa na gharama yeyote zaidi ya muda. Naongelea mazoezi na lishe bora.