Image

Kwa kawaida, meno ya mtoto ya utotoni (meno ya awali) huanza kutoka kuanzia miaka 6. Kwa baadhi ya watoto, huweza kuchelewa kuanza kutoka meno ya utotoni hadi wanapoanza mwaka wA 7.

Meno ya kwanza yanayoanza kutoka ni yale mawili ya chini ya kati (lower central incisors) na hufuatiwa na yale ya juu ya kati (upper central incisors) (. Baada ya hapo, hufuatiwa na meno ya kutafunia ya kwanza na ya pili.

Kwa kawaida, meno ya ya awali hukaa bila kutoka mpaka pale meno ya kudumu yanapotaka kuanza kuchomoza, hivyo hulisukuma jino la utoto na kusababisha kutoka. Endapo mtoto atatoka meno mapema au jino litatoka kwa sababu ya ajali au kuoza, basi jino la kudumu litaziba pengo hilo baada ya muda kufika. Hii inaweza kusababisha meno kutokuwa na mpangilio mzuri kwakuwa wakati linachomoza kulikuwa na meno mengine ya utotoni, hivyo unashauri kuwasiliana na daktari wa kinywa na meno kwa ushauri zaidi.

Pale mtoto anapoanza kutoka meno, tafadhali zingatia kanuni bora za Afya ya kinywa na meno kama ;

  • Kuhakikisha anasubua meno angalau mara mbili kwa siku. Mkazanie kwa sababu umakini unahitajika.
  • Msaidie mtoto kusugua meno kila siku
  • Hakikisha anakula chakula bora na kupunguza matumizi ya vyakula vitamu
  • Weka miadi na daktari wa kinywa nameno

Kwa mazingatio haya, utaweza kuhakikisha afya bora ya kinywa na meno ya mtoto wako. Pia, unaweza kusoma makala zaidi juu ya Afya ya kinywa na meno wakati wa makuzi ya mtoto

Afya bora ya kinywa na meno kwa mtoto ni muhimu sana na ina uhususiano wa moja kwa moja na afya yake kwa ujumla. Humuepusha mtoto kupata maumivu, uwezekano wa uambukizo, kumfanya aweze kutafuna vizuri ili kupata virutubisho muhimu kwa ajili ya kujenga kinga dhidi ya magonjwa, na kusaidia ukuaji. Afya nzuri ya kinywa na meno pia itamfanya mtoto aweze kuhudhuria masomo ipasavyo na hivyo kupata matokeo mazuri.

Umuhimu wa meno ya utoto

Wazazi /walezi wengi hujiuliza kwanini wahangaike kutunza meno ya utoto ambayo yanatarajiwa kung’oka na kuota ya ukubwa. Meno ya utoto ni muhimu kutokana na sababu zifuatazo:
Humsadia mtoto kutafuna na hivyo kumwezesha kupata virutubisho muhimu
Hutunza nafasi kwa ajili ya meno ya ukubwa
Hali ya afya ya meno ya utoto huathiri hali ya afya ya meno ya ukubwani
Husadia uumbaji wa maneno (kuongea)

Kama mzazi / mlezi unatakiwa kuwa mstari wa mbele kutunza meno ya mtoto wako kwani, watoto hupenda kujifunza kutokana na mfano wa wazazi.

Zifuatazo ni dondoo muhimu kwa wazazi/walezi kwa ajili ya kutunza afya bora ya mtoto:

Umri wa kuzaliwa mpaka miezi 6

  • Mnyonyeshe mtoto maziwa ya mama pekee hadi umri wa miezi sita.
  • Maziwa ya mama ni muhimu sana kwa ukuaji na kinga dhidi ya magonjwa.

Umri wa miezi 7 hadi miezi 18

  • Usimlaze mtoto akiwa na chuchu ya maziwa au chuchu ya mama mdomoni ili kuzuia ugonjwa wa kuoza kwa meno (rampant caries)
  • Mpatie mtoto maji badala ya juisi akiwa na kiu.
  • Iwapo utampa mtoto juisi ya boksi unashauriwa kuongeza kiwango cha maji sawa na kile cha juisi ili kupunguza kiasi cha sukari kilichomo ndani ya juisi.
  • Ukitengeneza juisi nyumbani kwa ajili ya mtoto, jiepushe kuiongezea sukari.
  • Jino la kwanza litakapoota, anza kusafisha kinywa cha mtoto kutumia kitambaa laini kilicholoweshwa kwenye maji safi au mswaki laini bila dawa.
  • Panga miadi ya kwanza ya kumwona daktari wa meno (first appointment) wakati mwanao hana maumivu au shida yoyote ili kujenga mahusiano mazuri kati ya mtoto na daktari

Umri wa miezi 18 hadi miaka 6

  • Dhibiti ulaji wa vyakula vyenye sukari na zingatia ulaji wa vyakula vinavyojenga afya ya mtoto kama matunda, mboga mboga, karanga, maziwa na samaki.
  • Safisha meno ya mtoto kutumia maji safi na mswaki laini na dawa ya meno (zingatia kiwango cha dawa: kiasi cha mbegu ya kunde) asubuhi na jioni kila siku.
  • Mtoto asukutue mdomoni ili kupunguza kiwango cha dawa itakayobaki.
  • Chunguza mara kwa mara meno ya mtoto ili kugundua dalili za mwanzo za ugonjwa wa kuoza kwa meno (rangi kuwa nyeupe au kahawia zaidi katika eneo husika baada ya kukausha) na pia matatizo mengine kama uvimbe, vijipu au kutoka damu kwenye fizi.
  • Mpeleke mtoto kwa daktari wa meno angalau mara moja kwa mwaka na mara unapogundua tatizo lolote kinywani mwake.

Umri wa miaka 6 hadi 12

  • Msimamie mtoto kusafisha kinywa na meno mara mbili kwa siku.
  • Mtoto ateme dawa itakayobaki ila asisukutue na maji baada ya kupiga mswaki.
  • Mjengee mtoto tabia ya kusukutua na maji kila baada ya kula vyakula vyenye sukari kama keki, chokoleti au juisi.
  • Chunguza mara kwa mara meno ya mtoto ili kugundua dalili za mwanzo za ugonjwa wa kuoza kwa meno na matatizo mengine kinywani.
  • Mpeleke mtoto kwa daktari wa meno angalau mara moja kwa mwaka na mara unapogundua tatizo lolote kinywani mwake.

Umri wa miaka 12 na zaidi

  • Mtoto anaweza kuanza kusafisha kinywa na meno bila ya usimamizi.
  • Dhibiti ulaji wa vyakula vyenye sukari na zingatia ulaji wa vyakula vinavyojenga afya ya mtoto kama matunda, mboga mboga, karanga, maziwa na samaki.
  • Mpeleke mtoto kwa daktari wa meno angalau mara moja kwa mwaka na mara unapogundua tatizo lolote kinywani mwake.

CREDIT: Muhimbili University of Health and Allied Sciences (MUHAS)

Watoto wanapozaliwa, tayari wanakuwa na meno ambayo  yamefunikiwa kwa fizi. Meno huanza kutoka kwa mara ya kwanza mtoto akiwa na umri wa miezi sita ( 6) japo umri huu unaweza tofautiana kutoka kwa mtoto mmoja hadi mwingine.

Meno mawili ya kwanza yanayoonekana mara nyingi ni yale ya kinywa cha chini katikati yakifuatiwa na ya kinywa cha  juu katikati. Watoto wengi hufikisha meno yote 20 ya kwanza wakiwa na umri wa miaka 3.

Baadhi ya watoto hawaoti meno kama watoto wengine, yao huchelewa au kutokuota kabisa. Hii husababishwa na vitu mbalimbali. Kama mtoto wako hajaota jino hata moja hadi umri wa miezi 18 basi ni muhimu umpeleke hospitali aonane na daktari wa kinywa na meno kwa ajili ya uchunguzi zaidi.

Sababu za meno kuchelewa kuota

Zipo sababu nyingi za meno kuchelewa kuota. Wakati mwingine tatizo la meno kuchelewa kuota huwa ni tatizo la kwenye familia  hivyo linaweza kurithishwa kwa vizazi vinavyokuja. Mzazi pia ujiulize kama meno yako yalichelewa kuota, kama ni ndio basi tambua kwamba hata ya mwanao yataota tu japo kwa kuchelewa.

Sababu zinazochangia meno kuchelewa kuota kwa mtoto ni kama zifuatazo;

  1. Utapia mlo na upungufu wa madini na vitamini mwilini- Watoto wenye utapia mlo meno huchelewa kuota kwa sababu ya kukosa virutubisho muhimu vya ukuaji wa meno. Aidha madini ya calcium na vitamini  D ni muhimu sana katika ukuaji wa meno. Hivyo mtoto akipungukiwa na virutubisho hivi meno huchelewa kuota.
  2. Ugonjwa wa jeni unaofahamika kama Down Syndrome- Huu ni miongoni mwa mgonjwa wa kuzaliwa nayo (congenital).Ugonjwa huu unatokana na hitilafu kwenye kinasaba cha 21 (chromosome 21). Ugonjwa huu huambatana na tatizo la meno kuchelewa kuota.
  3. Magojwa ya yatokanayo na hitalifu kwenye chromosomes (chromosome anomalies)
  4. Mtoto kuzaliwa njiti-Kuzaliwa njiti au na kuzaliwa  na uzito mdogo kupita kawaida (chini ya 1.5kg) kunahusishwa na kuchelewa kuota kwa meno kwa mtoto. Watoto hawa wanaweza kuwa na matatizo ya meno yenyewe.
  5. Magonjwa kama Amelogenesis na Regional Odontodysplasia

Amelogenesis ni ugonjwa wa kuzaliwa nao (congenital disease) ambapo mtoto anazaliwa na hitilafu kwenye kwenye protini zinazotengeneza enameli (nyeupe ngumu ya jino) hii hupelekea kuwa  na enameli isiyo ya kawaida na meno yanakuwa ya njano. Hii huambatana na meno kuchelewa kuota.

Regional odondodysplasia ni hitilafu katika ukuaji inayohusisha mesodermal na ectoderm (hizi ndizo zinazotengeneza jino la ndani na nje) za meno. Ugonjwa huu huwa unaathiri sehemu moja tu ya kinywa (localized). Huu sio ugonjwa wa kurithi.

Kwanini uwe na wasiwasi kuhusu meno ya mtoto yanapochelewa kuota?

Watoto ambao hawajaota meno hadi umri wa miezi 18 wapelekwe kumuona daktari wa meno. Watoto wengi huwa na meno manne wakifikia umri wa miezi 12 na huwa na yote 20 wakiwa na miezi 27.

Kama meno ya mtoto wako hayajaota kwa wakati inaweza kuwa ni ishara ya ugonjwa  au upungufu wa madini  au vitamini fulani mwilini.

Je, meno kuchelewa kutoa ni dalili mbaya?

Meno kuchelewa kuota sio jambo kubwa sana ila linaweza kuongeza uwezekano wa mtoto kupata matatizo ya meno ukubwani. Tafiti nyingi zinaonyesha kuwa watoto waliopata tatizo la meno kuchelewa kuota wana nafasi kubwa ya kuhitaji matibabu ya meno wakiwa na umri wa miaka 30.

Meno kuota kwa wakati kwa mtoto humsaidia kutafuna vizuri na husaidia meno ya pili kujipanga vizuri kwenye kinywa.

Meno yakichelewa kuota husababisha mtoto kukosa au kupata virutubisho vichache maana atakuwa hawezi kutafuna vizuri hivyo kupata shida ya kumeng’enya chakula.

Jinsi ya kutunza meno mapya ya mtoto wako

  1. Epuka vyakula na vinywaji vyenye sukari
  2. Safisha fizi kwa kutumia kutambaa kisafi mara mbili kwa siku
  3. Epuka kumlaza mtoto na chupa ya maziwa kitandani
  4. Kumbuka kuswaki na kusafisha meno yaliyoota

Utaanza kutumia dawa ya meno pindi mtoto akifikisha miaka 2.

 

Wiki iliyopita niliongelea kulika kwa meno kama hali inayotokea wakati sehemu ngumu ya nje ya meno huondoka na kusababisha sehemu ya ndani kuwa wazi.

Nilitaja kuwa ziko aina mbali mbali za kulika kwa meno kulingana na nini kinasababisha tatizo. Aidha kinga au tiba hutegemea nini kinasababisha tatizo hilo. Nikaongelea kwa undani kulika kwa meno kunakosababishwa na meno kusagana yaani attrition.

Leo nitaongelea aina nyingine ya kulika kwa meno

Kuyeyuka kwa meno (tooth erosion)

Huku ni kulika kwa meno kunakosababishwa na kemikali hasa tindikali. Tindikali inayoyeyusha meno haya yaweza kutoka nje au ndani ya mwili wenyewe.

Kuyeyuka kwa meno kunakosababishwa na tindikali toka nje ya mwili: Baadhi ya vyakula na vinywaji tunavyokula na kunywa vina kiwango kikubwa cha tindikali (acid), hivyo vyakula na vinywaji hivyo vikikaa kinywani kwa muda huweza kusababisha meno kuyeyuka.

Kulika kwa meno ni hali ambapo sehemu ngumu ya nje ya meno huondoka na kusababisha sehemu ya ndani kuwa wazi. Tatizo hili huanza kwa kuondoka sehemu ngumu ya nje (enamel) na kuiweka wazi sehemu ya kati ambayo ni ngumu pia (dentine). Tatizo likiendelea bila matibabu hufanya kiini cha jino, sehemu ambayo kuna mishipa ya damu, mishipa ya fahamu na chembe chembe mbali, kuwa wazi (dental pulp exposure).

Dalili hutegemea na kiwango cha ulikaji wa jino. Ikiwa ni sehemu ya nje kabisa imetoka, dalili huweza kuwa msisimko (sensitivity) wakati wa kunywa vinywaji vya baridi, vya sukari na hata meno yakipulizwa na upepo. Kama kiini cha jino kitakuwa wazi basi maumivu huanza na yanaweza kuwa makali kabisa.

Matibabu hutegemea kiwango cha uharibifu. Kama uharibifu ni kidogo, utumiaji wa dawa za meno zenye madini zaidi hasa ya fluoride unaweza kuondoa dalili. Wakati mwingine kutumia dawa za kupaka kitaalam, kuziba na kuvalisha kofia ngumu (crown) meno husika na mwisho ni kufanya matibabu ya mzizi wa jino (root canal treatment) au kung’oa jino kama kiini cha jino kimebaki wazi.

Ziko aina mbali mbali za kulika kwa meno kutokana na nini kinasababisha tatizo, na kinga au tiba hutegemea nini kisababishi.

Kusagika kwa meno (attrition)

Huku ni kulika kwa meno kwenye sehemu ambapo meno ya juu na chini hukutana (occlusal surfaces). Katika hali ya kawaida meno hulika sehemu hizi kutokana na kadri yanavyoendelea kutumika kusaga vyakula. Hali hii huendelea polepole kadri mtu anavyoendelea kuishi (umri), kitaalamu inajulikana kama physiological attrition.

Ukimwi  “upungufu wa kinga mwili”, ni ugonjwa unaoshambulia na kuua chembe chembe nyeupe za damu zinazosaidia mwili kupambana na magonjwa. Kutokana na upungufu huu wa kinga, magonjwa nyemelezi huanza kumpata muathirika wa ukimwi. Magonjwa yatokanayo na ukimwi uweza kujidhihirisha sehemu mbali mbali za mwili ikiwemo eneo la kinywa na uso. Kwa sasa nitaandika juu ya magonjwa ya eneo la kinywa na uso.

Fangasi za mdomoni (oral candidiasis)

Ugonjwa huu hujidhihirisha kama utando mweupe kwenye ulimi, paa la kinywa au kuta za kinywa, utando huu ni rahisi kukwanguliwa na kuacha ngozi laini yenye vipele vipele vyekundu. Wakati mwingine uonekana kama vipele vipele vyeupe kwenye kinywa.

Matibabu

Ugonjwa huu hutibika kwa kutumia dawa za kawaida za fangasi, ziwe vidonge, za maji au za kumun’gunya katika hali ya gel
 

       fangasi kwenye paa la kinywa        

Naitwa Kissu K. Mpini, ni mwenyeji wa wilaya ya Ifakara,mkoa wa Morogoro, Tanzania, utakumbuka mara ya mwisho nilivyotoa ushuhuda wangu kuhusu shida ya kusigina/kusaga meno-bruxism ilivyonitatiza kwa muda mrefu bila kupata nafuu, kwa kifupi baada ya kupata huduma pale kwenye hospitali ya Taifa Muhimbili, Kitengo cha Meno, ninaendelea vizuri sana kwa sasa, ninalala usingizi vema, na kazi zangu nazifanya vizuri, hakika nimekuwa mwenye furaha kama wenzangu.

Utakumbuka nilijiuliza sana kama watoto pia hupata tatizo la kusigina meno kama inavyotokea kwa watu wazima, hivyo ili kukata mzizi wa fitina, nilimwandikia barua daktari aliyenihudumia pale Muhimbili siku ile, nimeona ni vema pia elimu aliyonipatia daktari nishirikishe wadau wengine, maana sio wote tunaweza kufika Muhimbili kirahisi, vilevile ninaamini kuwa yeyote atayeweza kusoma maelekezo haya ya daktari itakuwa ni msaada mkubwa sana kwake binafsi, familia na rafiki zake. Majibu ya daktari yamebainisha kwa kirefu kuhusu tatizo la kusigina meno linavyoathiri watoto, ifuatayo ni barua ya daktari kama alivyoniandikia.

Tafiti zinaonesha kuwa asilimia 20 ya watoto kati ya mwaka 1 hadi miaka 11 husumbuliwa na kusigina/kusaga meno tatizo ambalo kwa kitaalamu linajulikana kama Bruxism. Ingawa takwimu hii inakadiriwa kuwa chini ya hali halisi kwa vile wazazi wengi wanashindwa kutambua tatizo hili kwa watoto wao.

Kama ilivyo kwa watu wazima kwa vyanzo mbalimbali vinavyosababisha kusigina meno, kwa watoto dalili za tatizo hili zinafanana sana na matatizo mengine ya watoto hivyo inawawia vigumu wazazi ama walezi kutambua tatizo hili na hata kupuuzia.

Baada ya kujifungua mtoto wangu wa kwanza, daktari wangu wa meno alinilalamikia kuwa situnzi vema afya yangu ya kinywa na meno. Kiukweli sikuwa nikifanya jambo lolote la ziada kuhakikisha afya yangu ya kinywa na meno iko katika hali nzuri.

Daktari wangu wa meno aliendelea kunieleza kuwa wanawake wajawazito wote na mama watarajiwa mara nyingi hupuuzia usafi wa kinywa na meno wakati wa ujauzito. Kiukweli, sikumuamini kabisa pale aliposema kuwa ujauzito husababisha mama wajawazito kubadili tabia zao za usafi wa kinywa na meno, lakini alikuwa sahihi kwa kiasi kikubwa kwa kunieleza kuwa wakati wa ujauzito vichocheo (hormones) vya mwili wa mwanamke hubadilika kwa kiwango kikubwa sana na mara nyingi huathiri afya ya fizi, hivyo ikiwa afya ya fizi ni dhaifu haiyumkini hali hii ikaathiri ukuaji wa kichanga tumboni mwa mama.

Tafiti zimethibitisha kuwa afya duni ya kinywa na meno hususani ugonjwa wa fizi unasababisha kuharibika kwa ujauzito. Tafiti iliyofanyika huko Marekani, Karolina ya Kaskazini kuangalia hali ya afya ya kinywa na meno kwa wamama watarajiwa 812, uchunguzi ulifanyika kwa kila mwanamama kwa kipindi cha majuma 26, na kisha masaa 48 baada ya kujifungua.

Watafitii walihakiki kiwango cha kuharibika mimba (chini ya majuma 28) na uzito mdogo wa kuzaliwa (chini ya 1000 gms), takwimu zilizingatia rangi ya mama (race), namba ya watoto wanaozaliwa, na jinsia ya mtoto. Asilimia 1.1 ya wamama waliokuwa na afya bora ya kinywa na meno (wamama 201) walipjifungua watoto njiti.

Kiwango hiki kiliongezeka zaid miongoni mwa wamama 566 waliokuwa na afya dhaifu ya kinywa na meno kutoka asilimia 3.5 mpaka asilimia 11.1 miongoni mwa wamama 45 waliokuwa na afya mbaya na afya mbaya zaidi ya kinywa na meno hususani magonjwa ya fizi.

Baadhi ya watu wana meno yaliyojipanga visivyo. Katika hali ya kawaida meno yanatakiwa yawe katika mahusiano mazuri kiasi kwamba meno ya juu yaweze kukutana vizuri na yaliyo jirani yakae vizuri pia. Utakuta baadhi ya watu meno ya juu yamechomoza mbele sana kiasi kwamba hata kufunga mdomo ni tatizo, wengine ya chini kuvutika mbele zaidi na kuwa na kidevu kilichochongoka kwenda mbele na wengine yamepandana pandana.

Mpangilio mbaya wa meno unaweza kuwa mbaya zaidi kiasi cha kumughasi mhusika na wakati mwingine meno yenyewe kushindwa kufanya kazi zake vizuri. Tatizo lingine la meno yaliyojipanga vibaya ni vigumu kuyasafisha na hivyo kuyaweka meno katika hatari ya kuoza na kusababisha magonjwa ya fizi.

Nini kinasababisha matatizo haya?

  • Maumbile yatokanayo na vinasaba na urithi
  • Tabia kama kunyonya vidole utotoni hata ukubwani kwa wengine
  • Kuwahi kutoka meno ya utotoni
  • Kuchelewa kutoka kwa meno ya utotoni hivyo kuyafanya ya ukubwani kuota upande
  • Ajali wakati wa kujifungua ambayo inaweza kuathiri maeneo ya kukua kwa taya

Matibabu

Lengo kubwa la matibabu ni kuyaweka meno katika mpangilio unaokubalika, ili kuboresha muonekano, utafunaji na hata utamkaji wa maneno.

Watu wengi huwa na hofu ya sintofahamu hasa wanapofikiria kwenda kumwona daktari wa meno. Mambo 10 yafuatayo yatakusaidia sana kufahamu nini utarajie unapokwenda kufuata uchunguzi wa afya ya kinywa na meno ama matibabu ya magonjwa ya kinywa na meno.

1. Uchunguzi wa afya ya kinywa na meno hujuimuisha uchunguzi wa kansa kinywani

Unapokwenda kwa daktari wa kinywa na meno kwa uchunguzi wa kawaida wa kinywa na meno (dental check up visit), kwa kawaida daktari wa kinywa na meno hutazama hali ya kinywa na meno pia huchunguza uwepo wa dalili za kansa kinywani. Inakadiriwa kuwa mtu mmoja hufa kila saa la kutokana na ugonjwa wa kansa kinywani huko Marekani. Ugonjwa huu hatari unaoshambulia zaidi kuta za kinywa, midomo-hasa mdomo wa chini- pamoja na koo unatibika ikiwa utatambuliwa mapema na kutibiwa kikamilifu.

Hivyo, kumwona daktari wa meno walau mara mbili kwa mwaka (kila baada ya miezi sita) na kuepuka matumizi ya tumbaku/sigara vitakuwezesha kujikinga na ugonjwa wa kansa ya kinywa na madhara yake.

2. Magonjwa ya fizi huathiri afya ya mwili kwa ujumla

Magonjwa ya fizi na meno ni chanzo kikuu cha kupoteza meno kwa watu wenye umri mkubwa/watu wazima, na pia magonjwa haya huhusishwa na magonjwa ya moyo na kiharusi (stroke).

Ikiwa magonjwa haya ya fizi yatatambuliwa mapema (gingivitis), yanatibika vizuri na kuepusha madhara zaidi.

Ikiwa tatizo hili halitopata tiba mapema, ugonjwa hukomaa zaidi (periodontitis) ambapo mfupa unaoshikilia jino/meno hushambuliwa na kuharibiwa.

Kusafisha meno kwa kupiga mswaki mara mbili kwa siku, matumizi ya nyuzi-safishi (dental floss), kumwona daktari wa meno kwa uchunguzi mara kwa mara na kusafisha meno kitaalamu kwa tatibu wa meno, kutasaidia kuepuka madhara ya magonjwa ya fizi.

3. Uchunguzi wa kinywa na kusafisha meno kitaalamu ni tiba muhimu zaidi

Ni wangapi kati yetu wenye desturi ya kumwona daktari wa meno walau mara mbili kwa mwaka (walau kila baada ya miezi sita)? Mara nyingi wengi wetu huhangaika na foleni za kumwona daktari wa meno pale tu tunaposumbuliwa na maumivu ama ya jino ama kidonda kinywani ama kwa sababi ya hali zinginezo zinatotulazimisha kumwona daktari wa meno.

Kusubiri mpaka tusukumwe na maumivu ya meno/kidonda kinywani ama ajali yoyote kunatunyima fursa bora zaidi ya kuchunguzwa afya ya kinywa na meno na kusafishwa meno ili kuepusha madhara ya magonjwa ya kinywa na meno kabla hayajatokea ama kukomaa.

Ukurasa 1 ya 2