Image

Unywaji wa vinywaji nishati  au vile vyenye kuongeza nguvu mwilini kwa mfano Red Bull unazidi kupata umaarufu mkubwa hasa miongoni mwa wanafunzi wa elimu ya juu. Wengi wa wanafunzi hawa hudai kuwa, vinywaji hivi huwaongezea nguvu ya kuweza kuwa macho na kujisomea kwa muda mrefu nyakati za usiku bila kuchoka hasa kipindi wanapojiandaa na mitihani yao. Aidha vinywaji hivi vinazidi kupata umaarufu miongoni mwa kundi jingine la vijana ambao mara nyingi hupendelea kuchanganya vinywaji hivi pamoja na pombe.

Kwa mujibu wa utafiti kuhusu unywaji wa vinywaji nishati uliofanywa miongoni mwa wanafunzi wa vyuo vikuu kadhaa vya mjini Maryland na Taasisi moja huko Marekani, na matokeo yake kuchapwa katika jarida la Alcoholism: Clinical & Experimental Research, tabia hii ya unywaji wa vinywaji nishati imeelezwa kuwa inaweza kuwa hatari kwa afya za wanywaji. Matokeo ya utafiti huo yameonesha kuwa hali ya kupunguza uchovu na kutopata usingizi inayosababishwa na vinywaji hivi inaweza kumfanya mnywaji aongeze muda wa unywaji zaidi.

Aidha watafiti hao wameonesha kuwepo kwa ushahidi kuwa vinywaji vya kuongeza nguvu mwilini hupunguza hisia ya ulevi wakati ambapo kiwango halisi cha ulevi mwilini tayari huwa kipo juu. Hali hii inaweza kuhatarisha zaidi hali ya mnywaji na pia kupelekea mnywaji kuwa mlevi sugu na hivyo kumuweka katika hatari ya kupata madhara makubwa zaidi ya pombe.

Wakiongozwa na tafiti zilizopita kuhusu hatari ya kuchanganya vinywaji nishati na pombe, Dr Arria (ambaye ni Mkurugenzi wa Kituo cha Afya na Maendeleo ya Vijana katika Chuo Kikuu cha Maryland)  na wenzake walichunguza ni kwa jinsi gani matumizi ya vinywaji nishati inavyoweza kusababisha hatari katika utegemezi wa pombe.

Utafiti huo ambao ulishirikisha jumla ya wanafunzi 1,097 wenye umri wa kati ya miaka 20 – 23 wa mwaka wa nne wa kimoja kikubwa cha Umma mjini Maryland ulifuata kipimo cha unywaji wa pombe kupindukia  kulingana na vigezo vya muongozoo wa ugonjwa wa akili. Aidha iliripotiwa kwamba karibu nusu ya wanafunzi wote walioshiriki kwenye utafiti huo walikuwa  watumiaji wadogo wa vinywaji hivyo, ambao walikuwa wakinywa kati ya siku moja mpaka siku 51 katika mwaka, na karibu asilimia kumi walikuwa watumiaji wakubwa wa vinywaji hivyo, ambao walikuwa wakinywa kwa zaidi ya siku 52.

Vilevile ilionekana kwamba watumiaji wakubwa wa vinywaji hivi, wana tabia pia ya kunywa pombe mara nyingi zaidi (siku 141.6 kwa mwaka kulinganisha na siku 103.1)  na kwa kiasi kikubwa zaidi (mara 6.15 kulinganisha na mara 4.64  kwa siku) ukilinganisha na wenzao wanaokunywa vinywaji nishati kwa kiwango kidogo. Aidha ilionekana kuwa watumiaji wakubwa wa vinywaji hivi walikuwa katika hatari kubwa zaidi ya kuwa wategemezi wa pombe tofauti na wale ambao hakuwa wakinywa kabisa pombe.

Pamoja na matokeo hayo, hata hivyo utafiti huo ulishindwa kuonesha utofauti wowote wa utegemezi wa pombe kati ya wanywaji wanaokunywa kwa kiasi kidogo na wale wasio watumiaji kabisa wa vinywaji nishati.

Matokeo ya utafiti huu yanatoa picha ya kuwa, kuna umuhimu hasa miongoni mwa vijana wanaopenda kuchanganya vinywaji nishati na pombe au wale wanaotumia vinywaji nishati kupita kiasi kuwa makini katika tabia zao ili kuwaepusha na madhara yake.

Wanasayansi wamegundua seli asilia (Stem Cells) kwenye mayai ya mwanamke (Ovaries) ambazo baadae zinaweza kutengeneza kiwango kikubwa kisicho na ukomo cha mayai ya uzazi ya awali (Oocytes).

Kwa kawaida mwanamke huwa na mayai mengi ya uzazi ya awali (Oocytes) wakati akiwa kwenye tumbo la mamake yaani bado akiwa kijusi (Fetus) ambapo anakadiriwa kuwa na mayai milioni 7, na mayai hayo kupungua hadi kuwa milioni 1 wakati anazaliwa na kufikia mayai 300,000 wakati wa kuvunja ungo au kubaleghe.

Mayai haya huisha kabisa akifika umri wa miaka 40 hadi miaka ya mwanzoni ya 50 (yaani kipindi cha ukomo wa kupata hedhi), na hii ndio huchangia mwanamke kutokuwa na uwezo tena wa kushika mimba ambao ni tofauti na wanaume ambao bado wanakuwa na uwezo wa kutoa shahawa hata wakiwa wazee.

Utafiti huo uliofanywa na wanasayansi katika hospitali ya Massacheutts nchini Marekani ambapo wanasayansi hao waliweza kuzitenganisha seli hizo kwenye maabara na kutengeneza mayai ambayo wamesema yanauwezo wa kurutubishwa (fertilized) na kuwa mimba.

Kutokana na utafiti huu, wataalamu wengi wa afya wamesema matokeo ya utafiti huu yatabadilisha kabisa tiba ya ugumba kwa wale wanawake wasioweza kushika mimba na pia yanaweza kusaidia wanawake kuwa na uwezo wa kushika mimba kwa muda mrefu zaidi kuliko ilivyo hivi sasa.

Watafiti nchini China wana matarajio makubwa kwamba nguruwe wanaozalishwa kijenetikia (Genetic modified cloned piglets) wanaweza kuwa suluhisho la matatizo ya viungo ambavyo vitaweza kupandikizwa kwa binadamu wenye kuhitaji viungo kutokana na viungo vyao kushindwa kufanya kazi baada ya kuathiriwa na magonjwa yasiyotibika.

Wanaume wanaovuta bangi wapo kwenye hatari ya kupata watoto wenye matatizo ya kiakili kama kutomudu masomo ya darasani, wamesema wanasayansi kutoka chuo kikuu cha Pennsylvania, nchini Marekani. Utafiti huu mpya umesema ya kwamba madhara ya bangi kwenye vina saba (DNA) yanaweza kurithishwa kupitia shahawa na hivyo kuathiri ukuaji wa ubongo wa mtoto.

Cha kushangaza ni kwamba madhara haya ya bangi kwenye ubongo wa mtoto huonekana sana kwa watoto wa kiume kuliko watoto wa kike au mtoto yoyote yule atakayezaliwa na mama ambaye alikuwa mvutaji bangi.

Wakati wanasayansi bado wanajaribu kutafuta ni kwa muda gani athari za bangi kwenye vina saba zinaweza kuwepo hata kama mvutaji ameacha kuvuta bangi miaka mingi iliyopita lakini tafiti hii ni muendelezo wa tafiti za hapo awali ambazo ziliwahi kueleza kuhusu madhara ya bangi kwenye vina saba kwa miaka mingi hata kama mvutaji ameacha kuvuta bangi. Profesa R. Christopher Pierce, mtaalamu wa sayansi ya akili (Neuroscience) katika chuo kikuu cha Pennsylvania pamoja na timu yake ya watafiti ambayo ndio walitafiti nadharia (hypothesis) hii ya kwamba ‘’uvutaji bangi huathiri vina saba kwa miaka mingi hata baada ya mtumiaji bangi kuacha kuvuta bangi’’.

Watafiti hawa walipima nadharia yao kwa kutafiti panya 16 wanaume ambao walipewa uwezo wa kutumia bangi wao wenyewe kwa kuwachanganyia bangi kwenye maji yao ya kunywa kwa muda wa siku 60.Panya wengine wa kiume walikunywa maji ya kawaida kwa muda huo wa siku 60.

Panya hawa walijamiana na panya majike na baadae kugundulika ya kwamba utumiaji bangi kwa mzazi hauna uhusiano wowote na uzito wa mtoto anaezaliwa, jinsia au ukuaji wa mtoto.

Hata hivyo kati ya watoto wote wa panya 46 waliozaliwa, watoto wa kiume ambao walitokana na wazazi ambao walitumia maji yenye mchanganyiko wa bangi walionekana kuwa na matatizo ya kiakili. Baada ya uchunguzi zaidi, watafiti hawa waligundua ya kwamba jeni (genes) ambazo ni muhimu kwa kumbukumbu za kiumbe zimebadilishwa (mutation) kutokana na matumizi ya bangi.

Asilimia ya watoto wa kiume ambao baba zao walitumia maji yaliyochanganya na bangi walikuwa na kiwango kidogo cha molekuli (molecule) aina ya D-serine ambayo ni muhimu kwa ajili ya kumbukumbu. Baada ya watafiti hawa kuwachoma molekuli hii ya D-serine kwenye sehemu ya ubongo ya watoto wa kiume wa panya inayojulikana kama hippocampus kutokana kuwa na kiwango kidogo cha D-serine, waligundua ya kwamba uwezo wao wa uelewa uliongezeka kwa kiwango kikubwa tofauti na hapo awali.

Yawezekana wanafunzi wasikubaliane na maelezo haya lakini wanasayansi wanatuthibitishia kuwa usingizi ni muhimu mno kwa mwanadamu kuweza kujifunza na kukumbuka alichojifunza.

Uwezo wa utendaji kazi wa usingizi umekuwa fumbo kwa muda mrefu lakini watafiti kadhaa wamekusanya ushahidi kuonesha kuwa kupata usingizi kwa masaa kadhaa husaidia sana katika kujifunza na kuongeza uwezo wa ubongo katika kutunza kumbukumbu.

Walau tafiti mpya mbili tofauti zinaonesha kuwa usingizi unahusika kwa kiasi kikubwa katika kujenga, kuhifadhi na kuzindua kumbukumbu na pia kuandaa ubongo kwa ajili ya kupokea kitu kipya wakati wa kujifunza.

Watafiti wakiongozwa na Paul Shaw wa Chuo Kikuu cha Washington huko St. Louis wanaripoti katika jarida la Science la June mwaka huu kuwa kitendo cha kugusa na kusisimua nyuroni kadhaa zilizopo katika sehemu ya juu ya ubongo wa aina fulani ya nzi waliotumika kwenye huo utafiti kilisababisha wadudu hao kupata usingizi.

Watafiti wanasema kuwa, kusisimua seli za ubongo zinazochochea usingizi hufanya kumbukumbu za muda mfupi (short-term memories) kubadilika na kuwa za muda mrefu (long-term memories).

Katika utafiti mwingine tofauti uliofanywa na wanasayansi kutoka Chuo Kikuu cha Wisconsin-Madison huko nchini Marekani na kuchapishwa katika jarida hilo hilo la Science, watafiti walionesha ushahidi kuwa wakati wa usingizi, mawasiliano katika ya seli mbalimbali za ubongo huchujwa kwa kiasi fulani.

Walionesha pia kuwa kuna ushahidi usio wa moja kwa moja wa kitendo hiki cha kuchuja mawasiliano kinachofanywa kati ya seli za ubongo husaidia kuandaa ubongo kupokea mafundisho na taarifa mpya ya siku inayofuata. Hata hivyo watafiti kutoka Chuo Kikuu cha Washington wao walionesha ushahidi wa moja kwa moja kuhusu suala hilo.

Watafiti nchini Japan wamegundua jinsi seli za mfumo wa fahamu zinavyoweza kutumika kama seli mbadala zinazofaa kupandikizwa kwenye seli kongosho ili kutibu kisukari. Ripoti ya utafiti huo ambayo imechapishwa kwenye jarida la kitafiti la EMBO Molecular Medicine, inaonesha kuwa seli zinazovunwa kutoka katika mfumo wa fahamu zinaweza kupandikizwa katika tezi kongosho na hivyo kumaliza tatizo la ukosefu wa seli za beta ambazo huitajika kwa ajili ya uzalishaji wa insulin.

Kisukari ni ugonjwa unaosababishwa na ukosefu wa kichocheo cha insulin kinachozalishwa na tezi kongosho, na ambao huathiri karibu watu milioni 200 duniani. Mpaka sasa hakuna tiba yeyote ya ugonjwa huu, hali inayowafanya wagonjwa wa kisukari kutegemea zaidi matumizi ya dawa au njia nyingine mbadala kuthibiti kiwango cha sukari mwilini.

Utafiti huo ulioongozwa na Dr Tomoko Kuwabara kutoka taasisi ya tafiti za Afya ya AIST ya Tsukuba nchini Japan, ulilenga katika kuchunguza jinsi seli za binadamu zinavyokua na kijiwagawa kulingana na kazi mbalimbali za mwili, na pia kuchunguza uwezekano wa kutumia seli mbalimbali kutekeleza kazi zilizo nje ya majukumu yake ya kawaida.  

Katika kufafanua, Dr. Kubawara anasema kuwa kwa vile kisukari ni ugonjwa unaosababishwa na ukosefu wa aina moja ya seli, ugonjwa huu unaweza kutibika kwa kutumia njia ya upandikizaji wa seli mpya zitakazotumika kuzalisha kichocheo cha insulin.

Anasema, hata hivyo kwa vile kupandikiza seli za beta kutoka tezi kongosho za watu wengine ni ngumu kwa sababu ya ukosefu wa watoaji, njia muafaka ni kutumia seli za mfumo wa fahamu wa mgonjwa mwenyewe katika kufanikisha upandikizaji huo.

Utafiti mpya uliofanyika nchini Marekani umesema ya kwamba kula machungwa na zabibu kunaweza kupunguza uwezekano wa kupata kiharusi (Stroke).

Utafiti huo uliangalia faida za matunda chachu (Citrus Fruit) pekee kwa mara ya kwanza tofauti na tafiti nyingi ambazo tumezizoea zinazoangalia umuhimu wa matunda na mboga za majani kwa afya kiujumla.

Utafiti huu umehusisha maelfu ya wanawake wanaoshiriki katika tafiti ya manesi Nurse’s Health Study lakini wataalamu wanaamini faida hizo za machungwa na zabibu pia zinapatikana kwa wanaume.

Timu ya watafiti katika chuo cha Norwich Medical School katika Chuo Kikuu cha East Anglia wamechunguza umuhimu wa kemikali aina ya flavonoids ambayo ni jamii ya antioxidant (kemikali zinauwa kemikali hatari za kwenye mwili) inayopatikana katika matunda, mboga za majani, chocolate nyeusi na wine nyekundu.

Utafiti huu ulifuatilia takwimu za miaka 14 za wanawake 69,222 ambao walikuwa wakishirki katika tafiti kwa kuandika kiwango chao cha kula matunda na mboga za majani kwa kila kipindi cha miaka 4.

Timu hiyo ya utafiti iliangalia uhusiano wa aina sita ya flavonoids - flavanones, anthocyanins, flavan-3-ols, flavonoid polymers, flavonols na flavones na hatari ya aina mbalimbali za kiharusi kama Ischaemic, Hemorrhagic na Total Stroke.

Ilionekana wanawake waliokula kiwango kikubwa cha flavanones kwenye matunda chachu walikuwa na asilimia 19 ya uwezekano wa kupunguza kiharusi kulinganisha na wanawake ambao walikula kiwango kidogo cha matunda hayo.

Kiwango kikubwa cha flavanones kilikuwa 45mg kwa siku kulinganisha na kiwango kidogo cha 25mg kwa siku.

Utafiti huu ulichapishwa katika jarida la Medical Journal Stroke umesema flavanones hupatikana kwa asilimia 82 kwenye machungwa na juisi ya machungwa na hupatikana kwa asilimia 14 kwenye zabibu na juisi ya zabibu. Hata hivyo watafiti hao wamesema kwa wale wenye kusudio la kuongeza kiwango kikubwa cha flavanones itawalazimu kula tunda la chungwa kwa wingi na si juisi za machungwa zinazotengenezwa kiwandani kutokana na kiwango kikubwa cha sukari kinachopatikana katika juisi hizo za viwandani.

Kimengenyo (enzyme) ambacho ni protini aina ya CYP2E1 kimegundulika kuwa ndio chanzo kinachochangia wanawake kupata saratani ya matiti kwa wanawake wanaotumia vilevi. Kwa muda mrefu wanasayansi walikuwa wakitafuta uthibitisho wa uhusiano wa kunywa pombe na saratani ya matiti, lakini sasa wameweza kupata uhusiano huo. Protini hii hupatikana kwenye matiti ya wanawake na hivyo kuwaweka kwenye hatari kubwa ya kupata saratani ya matiti kama watakuwa wanakunywa sana vilevi kama pombe, whiskey, wine na nk.

Utafiti uliofanywa na chuo kikuu cha Autonomous University of the State of Morelos cha nchini Mexico, umeonyesha ya kwamba protini hiyo ya aina ya CYP2E1 inauwezo wa kukivunja vunja kilewesho (ethanol) na kusababisha kutolewa kwa kemikali hatari zinazojulikana kama free radicals.

Watafiti hao wamesema ugunduzi wao utasaidia katika kuvumbua kipimo kitakachosaidia kujua ni wanawake gani walio na protini hii ya CYP2E1 na hivyo kuwasaidia kujikinga dhidhi ya saratani ya matiti.

Kemikali hizi hatari uhusishwa na kutokea kwa baadhi ya magonjwa kama saratani mbalimbali, ugonjwa wa kisukari, uharibifu wa mishipa ya damu aina ya ateri (arteries), kuchangia mtu kuzeeka na nk.

Swali kuu walilojiuliza watafiti wakati wa utafiti huo ni , Je kuwa na protini hii ya CYP2E1 kwa wingi huchangia mwanamke kupata ethanol-induced toxicity na hivyo kumhatarisha kupata saratani ya matiti?

Matokeo yetu yalionyesha ya kwamba seli za kutoka katika matiti ya mwanamke (mammary cells) zilizowekwa kilewesho cha aina ya ethanol, hutoa kemikali hatari kwa wingi, husababisha kuwepo kwa oxidative stress, huharakisha ufanyaji kazi wa seli na hivyo kuongeza kiwango cha ukuaji wa seli hizi kwa wingi na kusababisha saratani ya matiti” alisema Profesa Maria de Lourdes Rodriguez-Fragoso, kutoka chuo kikuu cha The Autonomous University of the State of Morelos cha nchini Mexico.

“Kama wewe ni mwanamke ambaye una kiwango kikubwa cha protini hii ya CYP2E1 katika matiti yako na unakunywa pombe basi utakuwa kwenye hatari kubwa ya kupata saratani ya matiti ikilinganishwa na mwanamke ambaye ana kiwango kidogo cha protini hii katika matiti yake.” Aliendelea kusema Profesa Maria de Lourdes Rodriguez-Fragoso.

Uchunguzi uliofanywa kutoka kwenye tishu za matiti ya wanawake wenye afya njema ambao wamefanyiwa upasuaji wa kukuza matiti yao umeonyesha viwango tofauti vya protini hii katika wanawake hawa.

“Hii inamaanisha ya kwamba wanawake wanatafautiana kwa umengenywaji wa pombe na hivyo inabidi kila mwanamke kuchukua hatua tofauti katika kupunguza uwezekano wa kupata saratani ya matiti” Alisema tena Profesa Maria de Lourdes Rodriguez-Fragoso.

Protini hii ya aina ya CYP2E1 hupatikana katika seli za matiti ya mwanamke zinazojulikana kama mammary epithelial cells ambapo pia ndio chanzo cha seli/chembechembe nyingi za saratani ya matiti na kusababisha watafiti hao kuanza kushuku uhusiano wake na saratani ya matiti.

Ili kuthibitisha shauku yao kwamba protini hii husababisha saratani ya matiti, watafiti hao walichukua tishu za matiti zilizo na viwango tofauti vya CYP2E1 na kuziweka kwenye pombe. Matokeo yalionyesha ya kwamba seli zenye kiwango kidogo cha protini aina ya CYP2E1 hazikuathiriwa sana ikilinganishwa na seli ambazo zilikuwa na kiwango kikubwa cha protini hiyo.

Utafiti huu ni ushindi mkubwa katika vita dhidhi ya saratani ya matiti kwani utasaidia kupunguza kiwango cha saratani hii kwa wanawake.

Kwa makala zaidi kuhusu saratani ya matiti na athari zake bonyeza hapa Saratani ya matiti.

 

Yawezekana wanafunzi wasikubaliane na maelezo haya lakini wanasayansi wanatuthibitishia kuwa usingizi ni muhimu mno kwa mwanadamu kuweza kujifunza na kukumbuka alichojifunza.

Uwezo wa utendaji kazi wa usingizi umekuwa fumbo kwa muda mrefu lakini watafiti kadhaa wamekusanya ushahidi kuonesha kuwa kupata usingizi kwa masaa kadhaa husaidia sana katika kujifunza na kuongeza uwezo wa ubongo katika kutunza kumbukumbu.

Walau tafiti mpya mbili tofauti zinaonesha kuwa usingizi unahusika kwa kiasi kikubwa katika kujenga, kuhifadhi na kuzindua kumbukumbu na pia kuandaa ubongo kwa ajili ya kupokea kitu kipya wakati wa kujifunza.

Watafiti wakiongozwa na Paul Shaw wa Chuo Kikuu cha Washington huko St. Louis wanaripoti katika jarida la Science la June mwaka huu kuwa kitendo cha kugusa na kusisimua nyuroni kadhaa zilizopo katika sehemu ya juu ya ubongo wa aina fulani ya nzi waliotumika kwenye huo utafiti kilisababisha wadudu hao kupata usingizi. Watafiti wanasema kuwa, kusisimua seli za ubongo zinazochochea usingizi hufanya kumbukumbu za muda mfupi (short-term memories) kubadilika na kuwa za muda mrefu (long-term memories).

Katika utafiti mwingine tofauti uliofanywa na wanasayansi kutoka Chuo Kikuu cha Wisconsin-Madison huko nchini Marekani na kuchapishwa katika jarida hilo hilo la Science, watafiti walionesha ushahidi kuwa wakati wa usingizi, mawasiliano katika ya seli mbalimbali za ubongo huchujwa kwa kiasi fulani. Walionesha pia kuwa kuna ushahidi usio wa moja kwa moja wa kitendo hiki cha kuchuja mawasiliano kinachofanywa kati ya seli za ubongo husaidia kuandaa ubongo kupokea mafundisho na taarifa mpya ya siku inayofuata. Hata hivyo watafiti kutoka Chuo Kikuu cha Washington wao walionesha ushahidi wa moja kwa moja kuhusu suala hilo.

Mwanasayansi wa masuala ya nyuroni na ubongo Marcos Frank kutoka Chuo Kikuu cha Pennsylvania, ambaye hata hivyo hakushiriki katika tafiti hizo, anasema kuwa matokeo ya tafiti hizo yanathibitisha dhana iliyokuwepo tangu awali kuwa kujifunza na kuweka kumbukumbu ni mambo yenye uhusiano na kupata usingizi.

Kundi la Shaw lilitumia nzi waliotengenezwa maalum (genetically engineered) ambapo walibadilisha aina fulani ya protein na kuifanya iwe na uwezo wa kusisimua seli za ubongo zinazochochea upatikanaji wa usingizi pindi kunapokuwa na mabadiliko ya joto ikiwemo joto kali au joto la kusababisha kuungua kwa aina fulani ya kemikali (capsaicin) ambayo hupatikana kwenye pilipili. Nzi waliokula aina pilipili zenye aina hii ya kemikali walionekana kusinzia, ingawa jambo hilo lilitokea baada ya muda mrefu kidogo wakati wale waliowekwa kwenye chombo chenye nyuzi joto 31°Celsius walipatwa na usingizi mara moja.

Aidha watafiti pia waliwakutanisha nzi wa kiume pamoja na nzi wengine wa kiume ambao walipandikizwa hormones na harufu ya kike ili kuchunguza kama kutatokea kitendo cha kujamiiana baina yao. Nzi wa kiume wasio na harufu ya kike walijaribu kuwapanda wenzao waliopandikizwa harufu ya kike lakini kitendo hicho kilishindikana hata baada ya kujaribu kwa masaa kadhaa kwa vile nzi waliopandikizwa harufu ya kike walikataa kufanywa hivyo. Lakini, kama vile mtu anapokesha usiku kucha akijaribu kusoma na kukariri kwa ajili ya mtihani wa kesho yake, uzoefu walioupata nzi wale wa kiume wasio na harufu ya kike haukuweza kusababisha nzi hao kutunza kumbukumbu ya muda mrefu iwapo wasingelala muda mfupi mara baada ya zoezi lao lililoshindikana. Hata baada ya kurudishwa tena kwenye chombo kile kile kwa ajili ya kujamiiana na nzi walewale wenye harufu ya kike, nzi hao wa kiume hawakuweza kukumbuka jaribio lao lililoshindwa, badala yake waliendelea kutaka kuwapanda wenzao ingawa matokeo yalikuwa kama awali.

Mara baada ya jaribio hilo lililoshindwa, wanasayansi hao walijaribu kusisimua sehemu ya ubongo inayohusika na usingizi kwa baadhi ya nzi wale wa kiume wasiokuwa na harufu ya kike. Kitendo hiki kilisababaisha kumbukumbu ya muda mfupi ya kukataliwa kujamiiana kugeuka na kuwa ya muda mrefu na ya kudumu (long-term memory). Watafiti walipojaribu kusisimua sehemu nyingine za ubongo wa nzi hao ili kuweza kuona kama kutakuwa na mabadiliko yeyote katika uwezo wa kutunza kumbukumbu, watafiti hao waliona kwamba sehemu hizo hazikuwa na uwezo wa kubadilisha kumbukumbu ya muda mfupi kuwa ya muda mrefu. Hali kadhalika, watafiti hao walijaribu pia kuwaacha nzi wengine bila kupata usingizi. Katika kundi hili la nzi, watafiti waligundua kuwa nzi hao hawakuweza kukumbuka kukataliwa kujamiiana kwao ikiwa ni uthibitisho kwamba kupata usingizi kuna husika zaidi na uwezo wa kubadili na kutunza kumbukumbu za muda mfupi kuwa za muda mrefu, na wala hivina uhusiano kabisa na usisimuaji wa ubongo kama ilivyodhaniwa hapo awali.

Shaw anasema, ingawa bado haifahamiki kwa uhakika kabisa ni kwa jinsi gani usingizi unawezesha utunzaji wa kumbukumbu lakini kwa hakika wanaweza kusema kuwa usingizi una nafasi kubwa mno katika utunzaji wa kumbukumbu.

Njia mojawapo ambayo wanasayansi wanadai usingizi unaweza kuathiri kumbukumbu ni kwa ubongo kuchuja kumbukumbu za ziada. Dhana hii ambayo kwa kitaalamu hujulikana kama dhana ya mizania ya sinapsi (synaptic homeostasis model) inasema kwamba wakati wa usingizi mawasiliano kati ya nyuroni na nyuroni, au kwa kitaalamu sinapsi, za baina ya seli na seli za ubongo huwa na dhaifu au pengine hukosekana kabisa. Mawasiliano ambayo yalianza yakiwa dhaifu huwa na tabia ya kupotea kabisa, wakati yale yaliyo imara huwa na tabia ya kutunzwa vizuri. Hali hii husababaisha ubongo uliojaa kumbukumbu ya shughuli za mchana kutwa nzima kujiweka sawa kwa ajili ya kufanya kazi za siku inayofuata. Kwa dhana hii, kundi la Shaw lilionesha kwamba kitendo cha kulala na kupata usingizi mzuri vinaenda sambamba na kitendo cha sinapsi za nyuroni za ubongo kuchuja habari na kumbukumbu zinazohitajika na zisizohitajika.

Katika utafiti mwingine, wanasayansi kutoka Chuo Kikuu cha Wisconsin–Madison wao walijaribu kuonesha kitendo cha uchujaji kumbukumbu na taarifa kwa undani zaidi. Wakitumia aina nyingine ya nzi wa utafiti, wataalamu hao walisema kuwa kadiri kiumbe kinavyojifunza, sinapsi nyingi zaidi huitajika na hutengenezwa katika ubongo wa kiumbe huyo, na ndivyo hitaji la usingizi linavyozidi kuwa kubwa ili kuuwezesha ubongo kurudi katika hali yake ya kawaida.

Wakitumia nzi waliotunzwa katika chupa maalum ambayo iliwafanya nzi hao wasiweze kutoka nje kwa muda wa wiki kadhaa, watafiti hao walichunguza ubongo za nzi hao baada ya wiki kadhaa za kuwa kifungoni. Ilionekana kuwa nzi wengi walikuwa na idadi kubwa ya sinapsi baada ya siku kadhaa za kukaa ndani ya chupa kuliko siku ya kwanza. Aidha nzi waliowezeshwa kupata usingizi walionekana kuwa na uwezo wa kuchuja idadi ya sinapsi zao na kuwa na idadi sawa kati ya asubuhi na muda wa kulala tofauti na nzi ambao walinyimwa uwezo wa kupata usingizi. Hata hivyo wanasayansi hawa walishindwa kujua ni aina gani ya sinapsi zinazochujwa na jinsi kitendo hicho kinavyofanyika. Ili kuweza kujibu hilo swali, watafiti wanapanga kufanya utafiti mwingine kwa kutumia panya.

Pamoja na hayo yote, hata hivyo kitu cha muhimu kukumbuka ni kuwa usingizi ni jambo la muhimu sana katika kujenga na kutunza kumbukumbu. “Si tu kwamba usingizi unawezesha ubongo kuweza kujifunza zaidi siku inayofuata kwa njia hii ya uchujaji taarifa, bali pia iwapo mtu asipolala, anakosa kabisa uwezo wa kujenga na kutunza kumbukumbu.”Anasema mmoja wa watafiti hao.

Makala hii imefasiriwa kutoka Jarida la Science ambalo pia hupatikana mtandaoni kupitia link hii

Matokeo ya utafiti mmoja huko nchini Uingereza yameonesha kuwa utumiaji wa wastani wa dawa aina ya Aspirini kila siku hupunguza uwezekano wa mtumiaji kufa kutokana na kansa.

Kwa mujibu wa ripoti ya utafiti huo, watafiti hao wanadai kugundua ushahidi wa uhakika kuwa utumiaji wa kila siku wa kiwango kidogo cha Aspirini hupunguza uwezekano wa kufa kutokana na kansa kwa karibu asilimia 30 ndani ya miaka mitano ya mwanzo ya utumiaji wa dawa hiyo.

Utafiti huo umeonesha kuwa, uwezekano wa kufa kwa sababu ya kansa hupungua kwa karibu asilimia hamsini kwa baadhi ya aina ya kansa na kwa kadiri mtu anavyotumia Aspirini kwa muda mrefu, uwezekano wa kufa kwa Kansa huzidi kupungua zaidi.

Watafiti hao wamedai kuwa watu wa umri wa kati ya miaka 45 hadi 50 na ambao hawana dalili ya magonjwa yeyote yale, ambao huanza kutumia dawa hii ya aspirini kwa kiwango kidogo kwa wastani wa miaka kati ya 20 hadi 30 wanaweza kufaidika zaidi kwa vile imeonekana kuwa uwezekano wa mtu kuugua kansa una uhusiano wa karibu na umri wake.

Inafahamika tangu awali kuwa kutumia kiwango cha milligrams kati ya 50 hadi 75 ambacho ni takribani robo ya kiwango cha kawaida cha kidonge cha Aspirini husaidia sana kuulinda moyo usipatwe na shinikizo. Faida hii imethibitika hata miongoni mwa watu ambao hawakuwahi kuonekana kuwa na magonjwa ya moyo hapo awali.

Ukurasa 1 ya 2