Image

Ugonjwa wa Trichomoniasis ni ugonjwa unaosababishwa na vimelea vya jamii ya protozoan vinavyojulikana kama Trichomonas vaginalis. Ugonjwa huu huathiri mrija wa kupitisha mkojo unaojulikana kama urethra na tupu ya mwanamke (vagina). Trichomoniasis pia hujulikana kwa majina mengine kama Trichomonas vaginitis au Trich (tamka “Trick”).

Trichomoniasis huathiri watu milioni 8 kwa mwaka Nchini Marekani na watu milioni 170 kwa mwaka dunia nzima. Ugonjwa huu huonekana sana kwa wanawake kuliko wanaume labda kutokana na wanaume kutoonyesha dalili zozote wakati wa maambukizi au kutokana na majimaji ya kwenye tezi dume kuwa na madini ya zinc ambayo huathiri vimelea hivi vya Trichomonas vaginalis. Ugonjwa huu hupatikana kwa njia ya kujamiana bila kutumia kinga na mtu aliyeathirika na Trichomoniasis.

Nakumbuka mwanajumuiya mmoja wa TanzMed aliuliza swali na hapa naomba ninukuu “madaktari, poleni na kazi za kila siku. mimi nina tatizo napata sana hizi yellowish discharge au niseme kama rangi ya maziwa hivi zinatoka huku chini kwenye tupu, asubuhi, mchana na jioni kama dose ya panadol. lakini hazina harufu kabisa, maana nilisoma makala zenu inasema kama zinatoa harufu ni dalili ya infections. Halafu za kwangu ni nzito hasa na zinavutika. Naomba msaada wenu sijui itakuwa ni nini?” mwisho wa nukuu.

Katika jibu langu nilimuahidi kuendelea na makala za magonjwa ya zinaa na leo naendelea na sehemu hii ya nne.

Nini hutokea wakati wa maambukizi/Pathofiziolojia ya ugonjwa (Pathophysiology)

Umbile la vimelea vya Trichomonas vaginalis ni sawa na chembechembe moja ya damu nyeupe kwa upana (10 μm) ingawa wakati mwingine ukubwa waweza kutofautiana kulingana na mazingira. Kutokana kuwepo kwa mfano wa mikono kwa nje inayojulikana kama flagellum ambayo husaidia vimelea hivi kuingia kwenye tishu za mrija wa kupitisha mkojo pamoja na tupu ya mwanamke na hivyo kuharibu seli aina ya epithelium na kusababisha vidonda (microulcerations) katika tishu hizi. Hii ndiyo sababu kubwa ya kwanini watu wanaopata ugonjwa huu wako kwenye hatari kubwa ya kupata ugonjwa wa ukimwi (HIV) na magonjwa mengine.

Wagonjwa huwa na dalili zipi?

Kati ya magonjwa yanayoathiri watu wengi sana duniani ni magonjwa ya zinaa. Haya ni magonjwa yanayoambukizwa kutoka kwa mtu mmoja kwenda kwa mwingine kupitia vitendo vya ngono. Vitendo hivi vya ngono vinaweza kuwa kujamiana, kupiga denda (kissing), vitendo vya ngono kwa kutumia mdomo (oral genital sex), kujamiana kupitia njia ya haja kubwa (anal sex) iwe kwa mwanamume na mwanamke au kati ya wanaume wenyewe na hata wale wanaotumia vifaa vya kufanyia ngono (vibrators). Magonjwa ya zinaa huathiri sana watu walio katika umri wa miaka 15 – 24 lakini hata kwa watu wengine ambao wana umri chini au zaidi ya huu niliotaja pia yanaonekana kwa wingi.

Kuna magonjwa ya zinaa zaidi ya ishirini yanayotambulika duniani, baadhi ya magonjwa ya zinaa ni

  • Kisonono (Gonorrhoea – “Gono” kama wengi wanavyopenda kuita kwa kifupi).
  • Chlamydia
  • Kaswende (Syphillis)
  • Human papilloma virus (HPV)
  • HIV/AIDS (Ukimwi/Upungufu wa kinga mwilini)
  • Hepatitis B, C, A
  • Herpes virus
  • Trichomoniasis
  • Bacteria Vaginosis
  • Pubic lice (chawa kwenye nywele za kinena)
  • Chancroid

Magonjwa mengi ya zinaa yanatibika lakini kuna baadhi ambayo hayana tiba ya uhakika kama HPV, Hepatitis B na C, na HIV. Mengine yameanza kuwa sugu kutokana na matumizi ya dawa za antibiotics bila mpangilio, magonjwa hayo ni kama gono (gonorrhoea) na nk.

Visababishi vya magonjwa ya zinaa

  • Vitendo vya ngono kama nilivyoeleza hapo awali
  • Kuanza vitendo vya ngono mapema au wakati wa umri mdogo
  • Kuwa na wapenzi wengi
  • Kufanya mapenzi ambao sio salama
  • Maambukizi kupitia michibuko au sehemu zilizokatika kwenye ngozi kwa kugusana na majimaji ya aina yoyote yanayotoka kwa mtu mwenye ugonjwa wa zinaa kama damu, shahawa nk. Hii inaweza kutokea bila mtu kujua kwani mara nyingi dalili za magonjwa ya zinaa zinakuwa hazionekani kwa wanawake na hata baadhi ya wanaume.

Watu wengi huhisi kitendo cha kula denda (kissing) ni salama lakini si kama wanavyofikiria kwani baadhi ya magonjwa kama kaswende, herpes nk, yanaweza kuambukizwa kupitia njia hii. Kondomu husaidia kupunguza maambukizi ya magonjwa ya zinaa kama gono, Chlamydia lakini sio kinga muafaka dhidhi ya magonjwa ya zinaa kama kaswende, genital herpes, genital warts, na magonjwa ya upungufu wa kinga mwilini (AIDS).

Nitaanza kuzungumzia ugonjwa wa gono (gonorrhea) kwa leo na makala zitakazofuata nitakuwa nazungumzia ugonjwa mmoja baada ya mwengine

Kisonono (gonorrhea) ni nini?

Kisonono ni ugonjwa kati ya magonjwa ya zinaa unaosababishwa na bakteria aina ya Neisseria gonorrhoeae, bakteria ambao hukuwa na kuzaliana kwa haraka katika sehemu zenye unyevunyevu na joto mwilini kama kwenye shingo ya kizazi kwa wanawake (cervix), mirija ya kupitisha mkojo au shahawa (urethra), mdomoni na kwenye puru. Maambukizi mengi kwa wanawake hutokea kwenye shingo ya kizazi (cervix). Asilimia 75 ya ugonjwa wa gono hutokea kwa watu wenye umri wa miaka 15 – 29, wanawake walio katika umri wa miaka 15 -19 na wanaume walio katika umri wa miaka 20 – 24 wako kwenye hatari zaidi ya kupata ugonjwa huu.

Ugonjwa huu huambukizwa vipi?

Ugonjwa huu huambukizwa kupitia vitendo vya ngono kupitia uke, njia ya haja kubwa (anus), kupitia mdomoni (oral sex). Ugonjwa unaweza kujitokeza kwenye sehemu za kujamiana, kwenye mdomo na kwenye puru (rectum). Ugonjwa wa gono huonekana sana kwa vijana, watu wenye maisha duni kiuchumi, watu wanaoishi mijini, watu weusi na watumiaji madawa ya kulevya.

Dalili za ugonjwa wa kisonono

Dalili za ugonjwa wa kisonono huanza kujitokeza kuanzia siku ya 2 hadi ya 7 baada ya mtu kupata maambukizi na huweza kuchelewa kwa wanawake. Dalili ni kama zifuatazo

Kwa wanaume

  • Kuhisi kama kichomi wakati wa kukojoa (burning sensation)
  • Kutokwa na majimaji ya njano au meupe au ya kijani kutoka kwenye uume yanayoambatana na maumivu makali sana
  • Wakati mwengine maumivu au kuvimba kwa korodani (swollen testicles)
  • Maambukizi yakiwa kwenye puru (rectum) huambatana na maumivu wakati wa kujisaidia haja kubwa, kuwashwa sehemu za haja kubwa, na hata haja kubwa inaweza kutoka ikiambatana na damu, hii inatokea kwa wanaume na wanawake.

Kwa wanawake

Dalili kwa wanawake huwa si nyingi lakini wanawake wengi hawaonyeshi dalili zozote

  • Maumivu au kuhisi kama kichomi wakati wa kukojoa
  • Kuongezeka kwa kutoka majimaji kutoka kwenye tupu ya mwanamke ambayo ni ya njano au yamechanganyika na damu
  • Kutokwa na damu kupitia tupu ya mwanamke kabla ya hedhi kufika.
  • Kutokwa na damu baada ya kujamiana au baada ya tendo la ndoa
  • Kichefuchefu
  • Homa (fever)
  • Kutapika

Vipimo vya ugonjwa wa kisonono

  • Swab for culture – Kipimo hiki hufanyika maabara kwa kupandikiza bakteria baada ya kufuta sehemu za siri kwa kutumia swab ili kuona kama kuna bakteria wanaosababisha gono.
  • Polymerase Chain Reaction (PCR) – Kipimo cha kuangalia vina saba (DNA) ya bakteria, ni ghali sana.

Tiba ya ugonjwa wa kisonono ni nini?

Tiba ya gono inahusisha na tiba ya ugonjwa wa Chlamydia kwani mara nyingi magonjwa haya huambatana kwa pamoja.Tiba hutegemea na umri wa mgonjwa na kama mtu ni mjamzito au la. Tiba ya gono ambayo sio sugu iliyo kwenye shingo ya kizazi (cervix), urethra na puru, dawa zinazotumika ni aina za cephalosporin dozi moja pamoja na dawa za aina ya macrolide antibiotics (mfano azithromycin) na za jamii ya penicillin (mfano doxycyclin) ili kutibu ugonjwa wa chlamydia. Mara nyingi kwa wale chini ya miaka 18 na wanawake wajawazito, hutibiwa kwa kuchomwa sindano.

Fuata ushauri wa daktari kabla ya kutumia dawa hizi kwani dawa nyingi zina madhara kwa wajawazito (mfano doxycyclin). Ushauri nasaha hutolewa kwa wapenzi wote wawili na ni vizuri wapenzi wote wawili kutibiwa hata kama mmoja hana dalili za ugonjwa huu.

Madhara ya ugonjwa wa kisonono

  • Kutoweza kuzaa kwa mwanamke (tasa) au kutoweza kutungisha mimba kwa mwanamume (infertility)
  • Huweza kuathiri moyo (heart valves), ubongo,ngozi nk ambayo ni hatari sana kwa mtu yoyote.
  • Madhara kwenye sehemu za maungio au jointi (joint inflammation)
  • Kwa wanawake wale ambao hawajatibiwa wanaweza kupata ugonjwa wa PID (Pelvic Inflammatory Disease) ambao huongeza asilimia ya mwanamke kuwa tasa.
  • Wale wanawake ambao ni wajawazito na wameambukizwa gono wako kwenye hatari ya mimba kutoka au kuzaa mapema kabla mimba haijatimiza umri wake (preterm labor).
  • Kwa wale wanaoambukizwa gono kipindi cha kukaribia kujifungua, wanaweza kuwaambukiza watoto wao na hivyo watoto kupata ugonjwa wa uti wa mgongo (meningitis), kuwa kipofu (blindness), homa ya mapafu (pneumonia) na ugonjwa wa mifupa (septic arthritis).

Kinga ya kisonono

  • Kutumia kondomu wakati wa kujamiana
  • Kuwa na mpenzi mmoja mwaminifu
  • Kuacha vitendo vya ngono kama matumizi ya vifaa vya ngono hasa kwa wanawake mfano vibrators nk.
  • Kwa wanawake wajawazito – Hakikisha unahudhuria kliniki mapema ili upate kuchunguzwa na kupatiwa tiba muafaka kama utagundulika na ugonjwa wa gono au ugonjwa mwengine wowote.
  • Wanawake wajawazito wanashauriwa kujifungulia hospitali ili kama mtoto ameathirika na gono apate matibabu ya haraka baada ya kuzaliwa kuepusha kuwa kipofu.
  • Epuka kufanya ngono na mtu aliyeambukizwa gono.

“Kumbuka ya kwamba hakuna kitu kama ngono salama kwani huwezi kujua kama wewe au mwenzako wakati wa kujamiana ameathirika au la, au una michibuko au umekatika kwenye ngozi au la kwani michibuko mengine inaweza isionekane au kugundulika kwa urahisi. Njia pekee na nzuri ni kuacha au kujikinga na vitendo vya ngono”. Mtu aliyepata gono awali anaweza kupata tena.

Usikose mwendelezo wa makala hii.........

 

Katika sehemu hii ya pili ya muendelezo wa makala ya magonjwa ya zinaa tutazungumzia kuhusu ugonjwa wa Chlamydia.

Chlamydia ni nini?

Chlamydia ni aina ya ugonjwa wa zinaa unaosababishwa na bakteria aina ya Chlamydia trachomatis ambao wanaweza kuathiri viungo vya uzazi na pia husababisha aina ya homa ya mapafu ijulikanayo kama atypical pneumonia.

Miongoni mwa magonjwa ya zinaa yasababishwayo na bakteria, Chlamydia unaoongoza kwa maambukizi duniani ambapo kwa nchi ya Marekani pekee inakisiwa watu milioni 4 huambukizwa kila mwaka. Kutokana na ukosefu wa takwimu za nchi nyingi barani Afrika ikiwemo Tanzania, ni vigumu kujua idadi kamili ya maambukizi, ingawa bila shaka ndio ugonjwa wa zinaa utokanao na bakteria unaoongoza kwa maambukizi ukifuatiwa na ugonjwa wa gonorrhea.

Clamydia huambukizwaje?

Chlamydia huambukizwa kupitia njia zifuatazo

  • Kujamiana kwa njia ya mdomo, njia ya haja kubwa na kupitia tupu ya mwanamke
  • Kuambukizwa kutoka kwa mama kwenda kwa mtoto wakati wa ujauzito
  • Au kupitia manyoya au vinyesi vya wanyama kama ndege walioambukizwa aina ya Chlamydia inayopatikana kwa ndege kama vile kuku, bata, kasuku nk. Aina hii ya clamydia husababisha aina ya homa ya mapafu ijulikanayo kama psittacosis ambayo huambatana na homa kali yenye nyuzi joto kati ya 39.4 - 41.1 celsius

Chlamydia huathiri sehemu tofauti za mwili wa binadamu kama vile macho, mfumo mzima wa kupumua, sehemu za siri, viungo vya uzazi na tezi (lymph nodes). Chlamydia na gonorrhea huwa na tabia ya kuambatana kwa pamoja (rejea makala ya magonjwa ya zinaa sehemu ya kwanza).

Dalili na viashiria vya ugonjwa wa Chlamydia

Asilimia 75 ya wanawake na asilimia 50 ya wanaume wanaopata maambukizi ya ugonjwa huu huwa hawaoneshi dalili zozote za ugonjwa wa Chlamydia. Dalili hutokea wiki 1 hadi 3 baada ya mtu kupata maambukizi.

Dalili kwa wanawake zinaweza kuwa

  • Kutokwa na majimaji ya rangi ya njano yenye harufu kali na mbaya sehemu za siri
  • Maumivu wakati wa kukojoa (haja ndogo)
  • Kuhisi kama kuwaka moto wakati wa kukojoa
  • Kutokwa na damu katikati ya kipindi cha hedhi yaani baada ya kumaliza mzunguko wa hedhi na kabla ya kuanza mzunguko mwengine wa hedhi
  • Maumivu sehemu ya chini ya tumbo
  • Maumivu wakati wa kujamiana
  • Kutokwa na damu wakati wa kujamiana
  • Kuvimba na maumivu kwenye tezi zilizopo sehemu za siri

Dalili kwa wanaume zinaweza kuwa

  • Maumivu wakati wa kukojoa
  • Kuhisi kama kuwaka moto wakati wa kukojoa
  • Kutokwa na majimaji kwenye uume yanayoweza kuwa ya rangi nyeupe kama maziwa, kijivu au ya njano
  • Sehemu ya tundu la uume huwa jekundu, huvimba na kuwasha
  • Maumivu kwenye korodani
  • Tezi zilizopo sehemu za siri huvimba na huambatana na maumivu

Mara nyingi dalili hizi kwa wanaume zinakuja na kupotea au zinaweza kuonekana tu wakati anaenda kukojoa asubuhi baada ya kuamka kutoka usingizini

Dalili za ugonjwa huu kama umeathiri puru (rectum) ni kama ifuatavyo (kwa wanawake na wanaume)

  • Kuwashwa na kutokwa na damu kwenye puru
  • Maumivu wakati wa kujisaidia haja kubwa
  • Kutokwa na uchafu kama kamasi kwenye puru

Dalili za chlaymdia iliyoathiri macho (kwa wanawake na wanaume)

  • Kuvimba sehemu za macho
  • Macho kuwa mekundu, kuwasha na hata kutokwa na majimaji

Chlamydia inayoambukiza kwenye macho (Chlamydia conjunctivitis or trachoma) ndio inayoongoza kwa kusababisha upofu duniani.

Vipimo vya uchunguzi

  • Urethral swab for culture – Majimaji kutoka kwenye uume au uke huchukuliwa kwa kutumia swab maalum ambapo hupelekwa maabara ili kuotesha na kuangalia aina ya uoto wa bakteria
  • Urinalysis (urine test) – Vipimo vya mkojo
  • Polymerase Chain Reaction (PCR) – Kipimo cha kuangalia vinasaba vya bakteria na hufanyika maabara.

Tiba ya ugonjwa wa Chlamydia

Chlamydia ni kati ya magonjwa ya zinaa yanayotibika. Ugonjwa huu hutibiwa kwa dawa aina ya antibiotics zilizopo kwenye makundi ya ;

  • Macrolide antibiotics
  • Quinolones antibiotics
  • Polyketides antibiotics

Madhara ya ugonjwa huu

  • Kwa wanaume, Chlamydia huathiri korodani na kusababisha mwanamume kukosa uwezo wa kutia mimba mwanamke (infertility) na maambukizi
  • Maambukizi kwenye tezi dume (prostatitis)
  • Kwa wanawake, husababisha maambukizi kwenye mirija ya uzazi, mfuko wa uzazi, na mayai ya uzazi hivyo kusababisha ugonjwa aina ya Pelvic inflammatory disease (PID). Pia huongeza asilimia ya mwanamke kupata mimba zinazotunga nje ya mfuko wa uzazi (Ectopic pregnancy). Mbali na hilo, mwanamke hupata maumivu sugu ya kwenye nyonga, ugonjwa wa mifupa arthritis aina ya Reiters syndrome. Vilevile, Chlamydia huweza kusababisha ugumba kwa mwanamke kama hatapata tiba.
  • Kwa wajawazito, Chlamydia husababisha wanawake kujifungua kabla wakati. Mtoto anaweza kuzaliwa na maambukizi kwenye masikio, sehemu za siri, macho na kwenye mapafu (homa ya mapafu). Kama mtoto hatapata tiba ya haraka ya macho basi anaweza kuwa kipofu.

Dalili za Chlamydia kwa watoto wachanga hutokea ndani wiki mbili kwenye macho na homa ya mapafu (pneumonia) ndani ya wiki 2 hadi miezi 3 baada ya kuzaliwa.

Jinsi ya kujikinga na ugonjwa wa Chlamydia

  • Kama ilivyoelezwa kwenye makala iliyopita, njia sahihi ya kujikinga na magonjwa ya zinaa ni kuacha au kuepuka kufanya ngono au kujamiana.
  • Kwa wanawake wajawazito, ni vizuri kuhudhuria kliniki mapema wakati wa ujauzito
  • Wale wenye maambukizi wanashauriwa kuchukua tahadhari ya kutowaambukiza wapenzi wao kwa kufanya ngono salama (kutumia mipira), kuepuka kushika macho kwa kutumia mikono na hata ikiwezekana kuwaepuka wapenzi wao ili kuwalinda na maambukizi.
  • Kwa wale ambao wapenzi wao wameambukizwa au wameonyesha dalili za ugonjwa huu, wanashauriwa na wao kupata tiba hata kama hawana dalili zozote.
 

Madhara ya ugonjwa wa kaswende katika mfumo wa mishipa ya fahamu hutokea miaka 10-20 baada ya mtu kuugua ugonjwa wa kaswende na ambaye hakupata tiba yoyote hapo awali. Madhara haya huonekana kwenye uti wa mgongo na kwenye ubongo.

Kuna aina nne ya neurosyphilis kama ifuatavyo

  • Isiyo na dalili (Asymptomatic) – Katika aina hii mgonjwa anakuwa hana dalili zozote. Aina hii ndio huonekana sana kwa wagonjwa ambao hawakupata tiba hapo awali.
  • Ulemavu wa jumla (General paresis)
  • Inayoshambulia tando za ubongo na mishipa ya damu (Meningovascular)
  • Inayoshambulia sehemu za chini za uti wa mgongo (Tabes dorsalis)

General paresis hutokana na kuathirika kwa ubongo na hivyo kuleta upungufu katika ufanyaji kazi wa ubongo (impairement of mental function). Aina hii pia huweza kutokea kwa wagonjwa wa kisonono (gonorrhoea).

Dalili za general paresis

  • Kupungua uwezo wa kuzungumza (aphasia)
  • Kupungua uwezo wa kufanya maamuzi (impaired judgement)
  • Kutokuwa na uwezo wa kuhesabu kitu chochote
  • Kupungua kuhamasishika (impaired motivation)

Ugonjwa wa kaswende ni ugonjwa wa zinaa unaosababishwa na bakteria aina ya Treponema pallidum.  Ugonjwa wa huu ni kati ya magonjwa ya zinaa yanayoongoza kwa kusababisha madhara mengi.

Maambukizi ya kaswende wakati wa ujauzito huleta madhara mengi sana kama kujifungua kiumbe ambacho kimeshakufa, mtoto kuathirika na ugonjwa huu wakati wa kuzaliwa, mtoto kupata matatizo wakati wa   ukuaji wake, degedege na kuongezeka kwa vifo vya watoto wachanga nchini. 

Ugonjwa wa kaswende huathiri zaidi ya mimba millioni moja duniani kote kila mwaka na huchangia theluthi mbili ya vifo vya watoto wale wanaozaliwa tayari wameshakufa katika nchi za maeneo ya jangwa la sahara. Asilimia 30 ya mimba zinazoathiriwa na kaswende huishia watoto kufariki wakati wa kuzaliwa. Asilimia nyengine 30 ya mimba zinazoathiriwa na kaswende husababisha watoto kuzaliwa na ugonjwa huu wa kaswende, kupata matatizo ya ukuaji wao, degedege na kuongeza vifo vya watoto kwa asilimia 50.

Taasisi ya  kudhibiti Ugonjwa wa Ukimwi Tanzania (Tanzania National AIDS Control Programme) au NACP imesema maambukizi yote ya kaswende wakati wa ujauzito Tanzania bara kati ya mwaka 2003 hadi 2004 ni asilimia 6.7, kutoka asilimia 0.4 kwa mkoa wa Kilimanjaro hadi asilimia 32 kwa mkoa wa Tabora katika ripoti yake ya utafiti uliofanywa chini ya Wizara ya afya na ustawi wa jamii. Maambukizi yalionekana yako juu zaidi kwa wanawake walio na umri wa miaka 35 na zaidi (7%) na kiwango cha maambukizi kuwa chini zaidi kwa wanawake walio na umri kati ya miaka 15 – 24 (6.5%).

Ugonjwa wa ukimwi na kaswende mara nyingi huambatana pamoja. Ugonjwa wa kaswende huongeza uwezekano wa mtu kupata ugonjwa wa ukimwi.

Ushawishi wa kuandika makala hii ya tatizo la kutokwa usaha wakati wa kukojoa umetokana na swali la msomaji wetu ambaye aliuliza hivi kwenye tovuti hii na hapa na mnukuu,

 " Dr khamisi samahani sana mi nasumbuliwa nikikojoa mwisho wa mkojo unatoka kama usaha na sina dalili ya kaswende ambazo umezizungumzia nakuomba unisaidie’’.

Bila shaka wapo wengi ambao wana tatizo kama hili na ambao wamewakilishwa kupitia swali hili lililoulizwa na msomaji wetu huyu. Naomba tuwe pamoja kwenye makala hii ili ujifunze kuhusu tatizo la mtu kutokwa usaha wakati wa kukojoa.

Tatizo la Kuwepo kwa chembechembe za usaha au usaha kwenye mkojo hujulikana kama pyuria ambapo linaweza kuonekana kwa kutumia hadubini (microscope) au kama tatizo ni kubwa linaweza kuonekana kwa macho.

Visababishi vya tatizo la Kutokwa Usaha Wakati wa Kukojoa ni nini?

Visababishi vya tatizo hili ni kama vifuatavyo;

  • Ugonjwa wa mfumo wa mkojo (UTI)-Maambukizi kwenye figo, kwenye mrija wa mkojo na kwenye kibofu cha mkojo (cystitis- amabayo huonekana sana)
  • Magonjwa ya Zinaa-Kama ugonjwa wa kisonono au ‘’gono’’ kama wengi wanavyoita, ugonjwa wa Chlamydia na Trichomoniasis
  • Sumu inayotokana na kemikali (Chemical poisoning) kama 4-Aminodiphenyl inayotumika kwenye maabara na kwa ajili ya tafiti
  • Tatizo linajulikana kama Reiter’s syndrome
  • Pyelonephritis-Maambukizi ya bakteria kwenye sehemu za figo zinazojulikana kama calyces, renal pelvis na tishu za figo
  • Madhara ya pyelonephritis ambayo husabababisha ugonjwa unaojulikana kama renal abscess
  • Maambukizi kwenye tezi dume-Prostatitis (Kwa wanaume)
  • Upungufu wa kinga mwilini
  • Mcharuko (Inflammation) kutokana kuwa na mawe kwenye kibofu cha mkojo au kwenye figo
  • Mzio (Allergy) au kuota uvimbe sehemu yoyote ya mfumo wa mkojo

Viashiria vya tatizo hili ni;

  • Maumivu makali ya kuchoma (Painful burning sensation) wakati wa kukojoa
  • Maumivu chini ya kitovu
  • Homa
  • Kutapika

Tatizo hii likidumu kwa muda mrefu husababisha kupungua uzito kwa mgonjwa

Katika sehemu hii ya pili ya muendelezo wa makala ya magonjwa ya zinaa nitazungumzia kuhusu ugonjwa wa Chlamydia.

Chlamydia ni nini?

Chlamydia ni aina ya ugonjwa wa zinaa unaosababishwa na bakteria aina ya Chlamydia trachomatis ambao wanaweza kuathiri viungo vya uzazi na pia kusababisha ugonjwa wa homa ya mapafu unaojulikana kama typical pneumonia. Kati ya magonjwa ya zinaa yanayosababishwa na bakteria, Chlamydia ndio ugonjwa unaoongoza kwa maambukizi duniani ambapo kwa nchi ya Marekani pekee inakisiwa watu milioni 4 huambukizwa kila mwaka .