Image

Kichwa kikubwa ni ugonjwa wa watoto wachanga wa kutanuka chemba za maji za kichwani na hivyo kupeleka muonekano wa kichwa kuwa mkubwa. Ugonjwa huu ni matokeo ya kuzalishwa kwa maji mengi kichwani ama kuziba kwa njia za kupitisha/kufyonzwa maji hayo.

Hutokana na sababu za kinasaba, hivyo mtoto kuzaliwa na kichwa kikubwa. Aina hii huambatana na matatizo mengine kama vile mgongo wazi (SPINE BIFIDA) na mguu kifundo (TALIPES). Sababu nyingine ni maambukizi ya mishipa ya fahamu pindi mtoto anapozaliwa au mara tuu baada ya kuzaliwa.

Ukweli kuhusu kichwa kikubwa  

  • Asilimia 50 ya watoto wa kichwa kikubwa huwa na changamoto ya ukuaji.
  • Kuanza matibabu mapema baada ya mtoto kuzaliwa hupunguza changamoto hizi za ukuaji.

Vihatarishi vyake

  • Ukosefu wa virutubisho (vitamins) aina ya folic acid wakati wa ujauzito.
  • Unywaji holela wa baadhi ya dawa za hospitali wakati wa ujauzito.
  • Ajali, hususani kwa watu wazima
  • BAADHI YA WATU WALIOZIDI MIAKA 60 (NORMAL PRESSURE HYDROCEPHALUS)

Dalili zake

Kwa watoto wachanga chini ya umri wa mwaka 1

  • Kulialia hovyo
  • Kushindwa kunyonya au kula vizuri.
  • Kuchelewa kukaza shingo
  • Kuvimba/kujaa utosi

Kwa watoto wakubwa na WATU WAZIMA

  • Kichwa kuuma
  • Kichefuchefu na kutapika
  • Matatizo ya kuona, kutembea, balance
  • Macho kuzama chini kamaa jua linalokuchwa

Matibabu yake

  • Kuwekewa mirija maalum ya kutoa maji (shunt)
  • Njia ya kisasa ya matundu (ETV)

Kumekuwa na taarifa mbalimbali zinazoripotiwa hapa nchini kuhusu watoto wanaozaliwa wakiwa wameungana. Jamii ya watanzania itawakumbuka sana watoto wa aina hiyo waliofahamika kwa majina ya Mariamu na Consolata ambao kwa sasa ni marehemu.Watoto hawa walikuwa faraja kubwa kwa taifa baada ya kuweza kuishi na kusoma hadi ngazi ya kuingia Chuo Kikuu.

Aidha kumekuwa na riporti za watoto wengine walioungana hapa nchini. Ripoti hii ilitolewa  na zahanati ya St. Theresa Health Centre iliopo Kyaka wiliyani Misenye.

Tafiti zinaonyesha kwenye kila uzao wa 50,000-200,000 kunakuwepo na pacha moja iliyoungana. Mara nyingi huzaliwa wamekufa na wengine hufa kipindi kidogo tu baada ya kuzaliwa na wengine huweza kuishi kwa kipindi fulani. Aina hii ya pacha hutokea zaidi kwa jinsia ya kike kwa uwiano wa 3:1 na jinsia ya kiume.

Tafadhali tuungane pamoja katika makala hii ili tujifunze kuhusu watoto hawa wanaozaliwa huku wameungana.

Watoto walioungana (conjoined twins) ni mapacha ambao maumbile yao yameungana tangu wakiwa katika mfuko wa uzazi na baada ya kuzaliwa. Hali hii hutokea kufuatia kuungana au kutokugawanyika kwa yai lililopevushwa wakati wa ukuaji wa awali.

Kawaida yai moja lililopevushwa hugawanyika zaidi katika siku ya 13 baada ya yai hilo kupevushwa (monozygotic twin pregnancy).Kutokugawanyika kwa yai hili lililopevushwa husababisha mapacha kuzaliwa wakiwa wameungana.Kuna aina mbili za mapacha walioungana;

  1. Mapacha wanaotumia kondo moja la nyuma (single placenta) hujulikana kama monochromic twins au
  2. Mapacha wanaotumia amniotic sac moja hujulikana kama monoamniotic twins

Mapacha walioungana husababishwa na kushindwa kuungana au kutengana kwa yai liliopevushwa wakatii wa ukuaji wa awali, japo hii haiwezi kuelezea kila aina ya kuungana (conjuction)

Ziko aina nyingi za mapacha walioungana (conjoined twins) na wanaweza kuwekwa kwenye makundi makubwa mawili;

  1. Non dorsally conjoined twins- Aina hii ya mapacha walioungana huchangia kitovu kimoja (umbilical cord) moja na  baadhi ya viungo vya ndani ya mwili (internal organs) 
  2. Dorsally conjoined twins -Hapa kila pacha anakuwa na (umbilical cord ) yake na mara nyingi hawachangii viungo vya ndani ya mwili.Hii hutokea pindi pacha hawa wamegawanyika na baadaye kuugana tena ( secondary fusion) katika hatua ya ukuaji wa awali.

Pathofiziolojia

Pacha hawa hutokea baada ya mgawanyiko (cleavage or axis duplication) kutokea baada ya siku ya 13 ya kupevushwa kwa yai. Inaaminika kawaida mgawanyiko huu hutokea siku ya 8 hadi ya 12. Sasa ukitokea baada ya hapo mgawanyiko huo ukianza huishia njiani hivyo husababisha aina hii ya mapacha.

Tafiti nyingine husema pacha waliogawanyika vizuri wanaweza kuungana tena katika hatua za awali za ukuaji kwenye mfuko wa uzazi na kupelekea aina hii ya pacha.

Kisababishi cha matukio haya kutokea bado hakijulikani.

Zifuatazo ni aina za mapacha walioungana (conjoined twins)

Thoraco-omphalopagus-Aina hii ya pacha wameungana  kifuani na kwenye tumbo. Hii ndo aina inayoonekana sana kwa asilimia 28. Mara nyingi hawa huchangia moyo mmoja, ini (liver) na hata sehemu ya juu ya utumbo (upper intestine).

Thoracopagus- Aina hii ya pacha wameungana kifuani tu. Ndo aina inafuatia na hutokea kwa asilimia 18. Wanaweza kuchangia moyo mmoja na ini.

Omphalopagus- Aina hii ya pacha huungana tumboni  karibu na kitovu.  Aina hii hutokea kwa asilimia 10. Hawa huchangia ini moja na sehemu ya utumbo mkubwa (colon) na utumbo mdogo wa chini.

Heteropagus (Parasitic twins). Aina hii nayo hutokea kwa asilimia 10. Aina hii kunakuwa na pacha mmoja mwenye hitilafu ameungana na pacha mwingine mzima.

Craniopagus- Aina hii hutokea kwa asilimia 6. Vichwa vinakuwa vimeungana. Na mara nyingi wachangia ubongo mmoja.

Ziko aina nyingine ambazo hutokea mara chache sana kama zifuatavyo;

Pyopagus- Aina hii mapacha wanaungana kwenye mgogo wa chini na makalio. Hawa huweza kuwa wanachangia sehemu ya utumbo na sehemu za siri mfano uume au uke

Rachipagus -Aina hii mapacha wameungana nyuma kwenye mgongo wote juu hadi chini.

Ischiopagus- Aina hii ya mapacha wameungana kwenye nyonga upande au uso kwa uso. Pacha hawa wanaweza kuchangia utumbo wa chini na sehemu za siri. Pia wanaweza changia miguu miwili au mitatu.

Cephalopagus- Aina hii ya mapacha wanaungana kuanzia kwenye kichwa hadi kwenye kitovu. Aina hii hi ngumu kuishi.

Historia ya mama

Mama wa mapacha aina huu hana tofauti na mama mwenye mapacha wa kawaida. Hamna dalili yoyote ya tofauti kwake.

Uchunguzi

Mapacha hawa wanaweza kugundulika kwa kipimo cha ultrasound mwanzo kabisa mwa ujauzito. Au kwa kutumia Prenatal Magnetic Resonance imaging (MRI)

Tiba

Mapacha wanaoishi baada ya kujifungua  wanaweza wekwa kwenye makundi makuu mawili

  1. Wale ambao wanaweza kutenganishwa kwa upasuaji
  2. Wale wasioweza kutenganishwa kwa upasuaji

Kwenye tiba ya upasuaji uchunguzi wa kina unafanywa ili kubaini uwezekano wa kuwatenganisha hasa kama wanachangia baadhi ya viungo muhimu kama moyo. Upasuaji wa kuwatenganisha mapacha walioungana uhusisha timu za wataalamu wa afya wabobezi kutoka fani mbalimbali za afya. Wakati mwingine upasuaji unaweza sabibisha pacha mmoja ua wote kupoteza maisha.

Tanzania ilishafanikiwa kufanya upasuaji wa aina hii wa kutenganisha mapacha walioungana katika hospitali ya taifa ya Muhimbili National Hospital(MNH)

 

Picha: BBC

Utangulizi

Degedege ni mojawapo ya matatizo hatari sana kwa watoto na huogopesha sana wazazi na walezi wengi. Katika hili kuna dhana tofauti tofauti zilizojengeka miongoni mwa wanajamii, ambapo baadhi huamini degedege ina uhusiano na mambo ya ushirikina na kwamba huweza kutibiwa kwa njia za namna hiyo.
Wazazi na walezi wenye imani za namna hii hukataa kuwapeleka watoto wao hospitali wakiamini kuwa watakufa iwapo wataachwa wapate matibabu ya hospitali. Dhana nyingine iliyojengeka ni ile ya kuwa degedege ni tatizo linalotokea mara moja tu maishani mwa mtoto kitu ambacho si kweli. Aidha wapo pia baadhi ya wanajamii wanaohusisha degedege na ugonjwa wa Malaria pekee.

Ukweli ni kwamba karibu asilimia 3 ya watoto chini ya miaka 15 hupata degedege, nusu ya hawa hupata degedege linalosababishwa na homa kali. Kwa maana hiyo basi, degedege pia linaweza kumpata mtoto asiye na homa kama kifafa. Inakadiriwa kuwa mtoto 1 kati ya 100 hupata degedege la kifafa.

Degedege ni nini?

Degedege ni dalili inayoonesha mvurugano katika ufanyaji kazi wa seli za ubongo. Kwa kawaida, seli za ubongo ambazo kwa kitaalamu huitwa neurons huwasiliana kwa njia ya mtiririko wa umeme (electrical impulses). Ni mtiririko huu wa mawasiliano ya umeme kati ya seli za ubongo ndiyo unaofanya mwili uweze kufanya kazi ipasavyo. Iwapo basi itatokea kuwepo sababu yeyote ile itakayosababisha mawasiliano kati ya seli za ubongo kutokuwa katika mtiririko sahihi mfano kuwepo msisimko wa mawasiliano, hali hiyo husababisha degedege.

Degedege husababishwa na nini?

Zipo sababu nyingi zinazoweza kusababisha degedege. Moja ya mambo yanayoweza kusababisha degedege ni kuwepo kwa jeraha katika ubongo (brain injury) ambalo linaweza kuwa kwa sababu yeyote ile ikiwemo jeraha analopata mtoto wakati wa kuzaliwa (brain ischemia).

Lakini pia kuna baadhi ya familia ambazo zinakuwa na matatizo ya kimaumbile katika ubongo zinazorithiwa toka kizazi hadi kizazi (mfano kifafa). Familia za namna hii huwa na watoto ambao hupatwa na degedege kwa kiasi kikubwa zaidi kuliko familia ambazo hazina matatizo haya.

Vilevile degedege inaweza kuhusishwa na hali ya mabadiliko ya muda mfupi katika ubongo kama vile joto kali, matumizi ya madawa ya kulevya kama cocaine, amphetamine, viwango visivyo vya kawaida vya sukari na sodium katika damu (electrolytes imbalance) na uwepo wa uvimbe katika ubongo (brain tumor).

Sababu nyingine zinazoweza kusababisha degedege 

  • saratani ya ubongo,
  • matatizo ya kimaumbile katika ubongo ya kuzaliwa nayo (congenital brain defects),
  • mashambulizi ya vimelea vya bakteria, virusi, fangasi katika ubongo kama vile ugonjwa wa uti wa mgongo (meningitis).

Utangulizi

Kuharisha kwa watoto ni tatizo linaloshika nafasi ya pili duniani kwa kusababisha vifo miongoni mwa watoto chini ya miaka mitano. Inakadiriwa kwamba kwa kila watoto 5 wanaofariki , 1 hufa kwa sababu ya kuharisha. Watoto milioni 1.5 kila mwaka hufa kutokana na kuharisha.

Leo hii, inakadiriwa asilimia 39 tu ya watoto wanaoharisha katika nchi zinazoendelea hupata matibabu sahihi.Hata hivyo, mwenendo wa kitakwimu unaonesha kwamba kumekuwa na mafanikio kidogo tangu mwaka 2000.

Kuharisha huelezwa kuwa ni upotevu wa maji na madini muhimu kwa mwili wa binadamu (electrolytes) kupitia kinyesi na kupelekea upungufu wa maji mwilini. Katika hali ya kawaida, watoto wachanga hutoa kiasi cha gramu 5 za kinyesi kwa kila kilo ya mtoto (5g/ kg) kwa siku, wakati mtu mzima hutoa wastani wa gramu 200 kwa siku. 

Mtoto ale chakula muda gani?

Chai ya asubuhi

Saa 12:00 mpaka 2:00 kutegemeana na ni muda gani mtoto anakwenda shule. Jambo la muhimu ni kuwa, mzazi/mlezi ahakikishe mtoto anakula asubuhi ili asiende shle akiwa na njaa, ikibidi mzazi/mlezi amfungie mtoto chakula abebe.

Chakula cha mchana

Muda wa kati ya saa 5:30 mpaka saa 7:00 mchana.

Chakula cha jioni

Saa 10:00

Chakula cha usiku

Saa 1:00 usiku

Jinsi ya kuandaa chakula cha siku ya Jumatatu

Asubuhi

Kifungua kinywa (Breakfast)

Mlo 1: Chapati Maji Na Juisi Ya Chungwa

Mahitaji: 250 gram Unga wa ngano, 1 yai, 100 gram maziwa ya maji, 20 gram mafuta ya mahindi, 10 gram baking powder

Jinsi ya kuandaa chapati maji

Changanya vitu vyote katika bakuli kisha piga na mchapo mpaka upate mchanganyiko safi na laini kabisa. Iwapo mchanganyiko bado mzito ongeza maji kiasi.

Jinsi ya kuandaa juisi ya chungwa: Menya chungwa safi kabisa ili kuondoa uchungu wa gesi iliyopo katika maganda. Kisha tumia chombo maalumu cha kukamulia juice, kamua kisha hifadhi katika friji bila kuweka sukari ili ikae kwa muda bila kuharibika. Kumbuka pia kuweka sukari wakati wa kunywa.

Mlo 2: Uji wa Ulezi na Mtindi

Mahitaji: 200 gram unga wa ulezi, 100 gram maziwa ya maji, 350 gram maji, 100 gram mtindi usio na ladha ya matunda

Jinsi ya kuandaa uji wa ulzei na mtindi: Changanya unga wa ulezi na maziwa katika bakuli kisha chukua sufuria weka maji kiasi cha gram 350. Chemsha maji yakishachemka weka mchanganyiko wa maziwa na unga wa ulezi koroga mpaka uchemke na kuchanganyika safi kabisa ili uji wako usishike chini na kuungua. Acha uchemke vizuri kisha onja ukipata ladha ya kuiva kwa nafaka utakua tayari.

Toa jikoni weka katika bakuli litakalotumiwa na mtoto kisha changanya mtindi usio na ladha ya matunda pamoja na sukari tayari kwa mtoto kunywa.

Mchana

Chakula cha mchana

Mlo: Glass ya maziwa na mkate wa nyama za kusindika

Jinsi ya kuandaa: Mpatie mtoto 200 gram za maziwa sawa na glasi moja ya uvuguvugu au ya baridi lakini kumbuka yawe yamechemshwa vizuri na yakapoa kwa ajili ya usalama.

Kisha chukua vipande viwili vya mkate paka siagi au mayonaisi. Kisha chukua beef salami na beef backon weka kati kati pamoja na slice ya nyanya na tango mbichi mpatie mtoto ale.

Jioni

Chakula cha jioni

Mlo: Sahani ya mchanganyiko wa mboga mbichi

Jinsi ya kuandaa: Chukua caroti, tango, pilipili hoho nyekundu na ya kijani zote mbichi na zuchini ichemshe kidogo kisha weka mtindi wenye ladha ya matunda kwa ajili ya kulia hizo mboga.

Huu ndio muonekano wa sahani ya mchanganyiko wa mboga kama mtoto ni mdogo sana zisage kwenye mashine ya kusagia nyama kisha utapata mchanganyiko laini mpatie mtoto asiyeweza kutafuna hizo mboga mbichi.

Usiku

Chakula cha usiku

Mlo 1: Supu ya uyoga

Mahitaji: 300gram Uyoga fresh au wa kopo, 50 gram kitunguu maji, 10 gram kitunguu swaumu, 10 gram tangawizi, 50 gram leeks, 100 gram viazi mbatata, 100 gram maziwa fresh, 50 gram mafuta ya kupikia, 300 gram maji

Jinsi ya kuandaa supu ya uyoga: Kaanga katika mafuta ya kupikia vitunguu maji na vitunguu swaumu pamoja na tangawizi. Kisha weka viazi mbatata, leeks na uyoga kaanga tena kiasi kisha weka maziwa na maji acha ichemke mpaka viazi viive kisha toa na saga kwenye blenda. Rudisha jikoni kama itakuwa nzito sana ongeza maziwa au maji kiasi. Usisahau kuweka chumvi kulingana na ladha.

Mlo 2: Kuku maziwa, muhogo na njegere

Mahitaji: 200 gram nyama ya kuku isiyo na mifupa, 100 gram njegere, 200 gram maziwa, 150 mihogo iliyochemshwa kwanza, 300 gram maji

Kulia ni machine ya kusagia nyama utakayoitumia kwa ajili ya kusagia vyakula mbali mbali.

Jinsi ya kuandaa kuku maziwa, muhogo na njegere: Chemsha vyote kwa pamoja kuku na njegere mbichi pamoja na muhogo uliokwisha chemshwa kwanza mpaka ikaribie kukauka mchuzi  kisha toa jikoni. Chuja kisha weka mchuzi pembeni.

Chukua mchanganyiko wa njegere, kuku na muhogo. Tumia machine ya kusagia nyama weka huo mchanganyiko kisha saga upate rojo zito kisha rudisha katika sufuri, changanya na ule mchuzi uliochuja ongeza chumvi kulingana na ladha mpe mtoto ale chakula kikiwa cha moto.

Kama huna mashine ya kusagia nyama tumia mwiko kuponda itakua safi kabisa kisha unachanganya na ule mchuzi uliochuja.

Kwa mtoto mkubwa usisage. Baada ya kuchemsha ikaiva ongeza chumvi kisha mpakulie ale chakula cha moto atafurahia sana mchanganyiko wa ladha ya chakula hiki.

Orodha kwa ajili ya manunuzi siku ya Jumatatu

Uyoga wa kopo au fresh, mihogo mibichi, pili pili hoho, tangawizi, unga wa ngano, mayai, maziwa, sukari, chumvi, njegere, nyama ya kuku, tango, zucchini, mtindi usio na ladha ya matunda, mtindi wa ladha ya matunda, baking powder, viazi mbatata, mafuta ya mahindi na leeks.

Vitu hivi vyote sio vingi na unaweza kuvitumia siku inayofuata maana menu yetu ina uwiano safi kabisa. Vitu vingi vinatumika karibu kila siku na manunuzi yake sio ghali kabisa. Mpe mwanao raha kwa kula chakula safi na salama.

Kwa maelezo zaidi, tembelea blog ya www.activechef.blogspot.com ambapo Chef Issa anachambua na kuelezea namna ya kuandaa mapishi mbali mbali kwa ufundi na ubora wa hali ya juu. Kwa mawasiliano, unaweza kumuandikia kupitia email yake ya issakesu@gmail.com

Tafsiri za maneno “rampant caries” ni nyingi katika fani ya meno lakini la msingi ni kuoza kwa meno kunako enea kwa kasi na kuharibu vichwa (crowns) vya meno mengi au yote yaliyoota. Hii ni hali mbaya ya kuoza kwa meno ambayo hushambulia zaidi meno ya utotoni (milk teeth or primary dentition), japo wakati mwingine hata ukubwani.

Ugonjwa huu unajidhihirisha kwa kuanza na kuongezeka kwa kasi na kwa namna unavyo yashambulia meno na vyanzo vyake. Meno hushambuliwa kwa mpigo hasa kuanzia meno ya juu mbele, ingawa meno ya chini mbele ni mara chache kushambuliwa kwa vile yanakingwa na visababisha vya kuoza na ulimi.

Ugonjwa huu hushambulia hata maeneo ya meno ambayo kwa hali ya kawaida si rahisi kuoza, kama sehemu ya kukatia kwa meno ya mbele (incisal edges) na sehemu ya mbele kati na nyuma kati (facial and lingual surfaces).

Nini husababisha meno kuoza kwa kasi utotoni?

Homa ya mapafu ni aina ya maambukizi yanayoathiri mapafu. Ni ugonjwa ambao unaua watoto wengi hasa katika nchi zinazoendelea duniani. Inakadiriwa kwamba watoto karibu milioni 1.6 walio chini ya miaka 5 wanakufa kila mwaka kutokana na ugonjwa huu. Kutokana na vifo vingi vinavyotokana na homa ya mapafu tarehe 12 ya mwezi wa Novemba kila mwaka imefanywa kuwa siku rasmi ya homa ya mapafu duniani, ambapo nembo ya siku hiyo ni nguo za rangi ya bluu.

Muundo wa Mapafu

Mapafu yanajumuisha mirija mikubwa ya hewa (bronchi) ambayo hugawanyika kufanya mirija midogo zaidi ya hewa (bronchioles), ambayo nayo hutengeneza vifuko vidogo vidogo ya hewa (alveoli). Vifuko hivi vidogo vya hewa (alveoli) vina mishipa ya kupitisha damu (capillaries) ambayo husaidia kuchuja na kusafirisha hewa safi ya oksijeni tunayovuta kuingia kwenye damu na hewa chafu ya ukaa (kaboni dioksidi) kuondolewa kwenye damu na kuingizwa kwenye mapafu tayari kwa kutolewa nje ya mwili.

Kwa kawaida vifuko hivi vidogo hujaa hewa muda wote tayari kwa kusafirishwa. Inapotokea mtu akapata homa ya mapafu, vifuko hivi hujaa maji au usaha hivyo kuathiri upitishaji wa hewa safi kwenye damu na kusababisha tatizo la kupumua.

Homa ya mapafu husababishwa na nini?

Kuna aina kadhaa ya vimelea ambao vinaweza kusababisha maambukizi ya mapafu. Vimelea hivi hujumuisha bakteria, virusi, parasite na fangasi.

Vimelea hawa hushambulia mwili wa binadamu kulingana na umri na kinga ya mwili. Kwa mfano, bakteria wanaosababisha homa ya mapafu kwa watoto wachanga ni tofauti na wale wanaosababisha ugonjwa huo kwa watoto wakubwa.

 

Surua ni mojawapo ya magonjwa ya kuambukiza yanayotisha  kwa binadamu. Huu ni  ugonjwa ulio na  kiwango cha juu cha karibu asilimia 100 cha mashambulizi  pindi mtu apatapo vimelea vya ugonjwa huu.
Pamoja na kuwepo chanjo ya ugonjwa huu, bado surua ni miongoni mwa magonjwa yanayosababisha vifo vingi vya watoto walio chini ya umri wa miaka 5 katika baadhi ya maeneo  duniani hasa kwa nchi zinazoendelea. Ugonjwa huu ambao ulitoweka katika baadhi ya nchi, umeanza kuonekana tena hivi karibuni miongoni mwa watu ambao hawakupata chanjo katika nchi za Uingereza na nyingine za Ulaya.
 
Surua husababishwa na nini?
Surua huenezwa na aina ya virusi jamii ya paramyxovirus. Jamii hii ya virusi hupatikana katika mfumo wa njia ya hewa. Hukaa katika kamasi na majimaji yaliyopo katika mfumo wa hewa. Kwa sababu hii basi virusi hawa huenezwa kwa njia ya upumuaji.
Virusi hawa wanaweza kuishi hewani kwa muda wa hadi saa moja baada ya kutolewa kwa kupiga chafya au kukohoa au hata mazungumzo na mgonjwa. Hii ina maana kuwa, ili kuambukizwa surua, si lazima mtu akutane uso kwa uso na mgonjwa.
Baada ya kuingia ndani ya mfumo wa hewa virusi hushambulia seli za utando wa nje wa njia ya hewa (respiratory tract epithelium) na kuingia katika mzunguko wa wa limfu na kufika kwenye tezi zilizo karibu. Katika tezi huzaliana zaidi na kusambaa mwilini.
 
Muonekano wa mgonjwa
Kawaida dalili za mwanzo zinaanza kuonekana baada ya siku 8 ya kupata uambukizi. Mgonjwa huwa na mafua mepesi, homa, kukohoa na macho kuwa mekundu.
Baada ya siku 2-4 tangu kuanza kuonekana kwa dalili za awali, ukichunguza mdomo wa  mtoto, na kama utamchunguza pembeni (ndani ya shavu) utaona vidonda vyeupe kwenye utando mwekundu wa ndani ya mdomo. Vidonda hivi huonekana kama chumvi iliyomwagwa kwenye zulia jekundu. Hali hii huitwaKoplik spots. Hii ni dalili tosha ya kuthibitisha uwepo wa surua.
Lakini vilevile mgonjwa anaweza kuwa na vipele vidogo sana ambavyo inaweza kukuwia vigumu kutambua. Vipele hivi huweza kuonekana vizuri siku mbili baadaye. Kwa kawaida, vipele hivi huanzia usoni au nyuma ya sikio na kushuka chini kabla ya kutapakaa mwili mzima siku zinazofuata. Vipele huongezeka na kuwa vingi kadiri siku zinavyopita. Kawaida hali hii ya vipele inaweza kuchukua kati ya wiki 1-2. Vipele hupotea baada ya siku 7 na kuacha ngozi iliyobabuka. Hata hivyo, kukohoa kunaweza kuendelea zaidi ya siku 10.
 
Athari za Surua ni zipi?
Ingawa baadhi ya wagonjwa hupona katika kipindi cha siku 10 mpaka 14, baadhi hupata matatizo zaidi yanayoweza kuwa ya muda mrefu kama;
•Maambukizi njia ya masikio (Otitis media)
•Maambukizi njia ya chini ya mfumo wa hewa kama vile
  1. Uambukizi kwenye mirija ya hewa ya koo (bronchitis) maambukizi kwenye njia ya sauti (laryngitis) na croup. Surua inaweza kusababisha kuvimba katika sehemu ya sauti na kuathiri uwezo wa kutoa sauti lakini vilevile inaweza kusababisha uvimbe  katika kuta za utando wa njia ya hewa.
  2. Homa ya mapafu (pneumonia) ambayo ni sababu kuu inayosababisha vifo vinavyotokana na surua. Mgonjwa wa surua ni rahisi kupata homa ya mapafu kwa sababu kinga ya mwili wake huwa imepungua. Homa hii ya mapafu yaweza kusababishwa na aina nyingine ya virusi kama adenovirus, herpes simplex au bakteria kama Staphylococcus aureus, Streptococcus pneumonia, Haemophillus influenza, Klebsiella pneumonia. Lakini vilevile Kifua kikuu kinaweza kutokea kwa kusababishwa na upungufu huu wa kinga mwilini.
•Surua pia inahusishwa na aina mbalimbali ya mashambulizi kwenye ubongo kama vile
  1. Acute encephalitis ambayo hutokea wakati au ndani ya wiki chache baada ya maambukizi.
  2. Progressive encephalitis ambayo hutokea kwa wagonjwa walio na upungufu wa kinga mwilini unaotokana na sababu yeyote ile ikiwemo wale anaopata tiba ya kemikali (Chemotherapy) au kwa sababu ya VVU. Hali hii hutokea  miezi 6 baada ya maambukizi, na inaweza kusababisha mgonjwa kufa.
  3. Subacute sclerosing panencephalitis (SSPE) ni nadra sana kutokea. Mara nyingi kama likitokea, basi humpata mgonjwa baada ya mwaka mmoja wa ugonjwa wa surua. Sifa mojawapo ya hili tatizo ni kupungukiwa kwa uwezo wa kufikiri na akili kuzorota na hatimaye mgonjwa kufariki dunia.
•Surua inaweza kusababisha utapiamlo kwa sababu ya ukali wake hasa kwa watoto ambao hawapati lishe nzuri. Inahusishwa pia na kuharisha na kutapika na kusababisha upungufu wa maji mwilini.
•Surua husababisha upungufu wa Vitamini A na kusababisha tatizo la kutoona vizuri ambalo hijulikana pia kama Keratitis. Kwa mtoto ambaye ana upungufu wa Vitamini A tatizo la macho huwa kubwa zaidi na kwa kitaalamu hujulikana kama Keratomalaciaambapo sehemu nyeupe ya jicho hutoboka.
•Maambukizi katika misuli ya moyo  (Myocarditis)
•Upungufu wa chembe sahani kwenye damu (Thrombocytopenia)
 
Utambuzi wa surua
Utambuzi wa surua inajumuisha historia ya mgonjwa kuwa na homa kwa angalau siku 3 na kuwepo kwa mojawapo ya dalili za mwanzo za surua ambazo ni kukohoa, kuwa na mafua mepesi, macho kuwa mekundu na upele mwilini. Aidha ikithibitika mgonjwa ana Koplik spotsbaada ya uchunguzi ndani ya mdomo ni utambuzi tosha wa surua.
Vilevile vipimo vya kimaabara ni pamoja na uthibitisho chanya wa antibodi dhidi ya surua(measles IgM antibodies) na uwezekano wa kuwapata virus wa surua kutoka katika mfumo wa hewa, damu au mkojo wa mgonjwa (isolation of measles virus RNA) au kwa njia ya kuoteshwa maabara (culture).
 
                                                                        Matibabu
Hakuna tiba maalum kwa ajili ya surua. Lengo kubwa la matibabu ya surua ni kuhakikisha mgonjwa anapata mapumziko, maji ya kutosha, oksijeni na faraja. Mgonjwa anaweza kupewa dawa za kutuliza homa kama vile paracetamol. Imeonekana kuwa matumizi ya dawa ya virusi wa surua (antivirus) hayana msaada wowote katika kutibu surua.
Aidha dawa kwa ajili ya kuzuia magonjwa yanayosababishwa na bakteria (Prophylactic antimicrobial therapy) isipokuwa tu iwapo itathibitika kuwepo kwa maambukizi ya bakteria. Inasisitizwa sana mgonjwa apatiwe Vitamini A. Vitamini A hupunguza hatari ya kifo na madhara ya surua.
Kwa vile ugonjwa wa surua unaenea kwa njia ya hewa ni vizuri mgonjwa akatengwa na watoto wengine. Muhimu ni kutafuta ushauri wa daktari haraka pale unapoona mtoto ana dalili za surua.
 
Kinga
Surua huzuiwa kwa urahisi kwa njia ya chanjo. Watoto ambao hawajapata chanjo ya surua wapo katika hatari kubwa sana ya kupata surua.
 
Kumbuka
Surua ni ugonjwa hatari. Unaweza kuua au kusababisha madhara ya muda mrefu lakini chanjo dhidi yake inazuia hatari hiyo.  Kwa hiyo pale unapohisi mtoto wako  ana dalili za surua  mpeleke haraka hospitali ili kujithibitisha na kupata matibabu yanayofaa.