Image

Matatizo ya Akili (Mental Retardation) -Sehemu ya 1

Upungufu wa akili ni tatizo ambalo kwa ujumla hutokea kabla ya mtu kuwa mkubwa (adulthood) na huambatana na dalili za kupunguwa uwezo wa akili ya utambuzi na kutafakari (cognitive functions) pamoja na kushindwa kukua kwa tabia za kuendana na mazingira yanayomzunguka mtu (adaptive behavior). Pia kitaalamu, upungufu wa akili hujulikana kama mtu yoyote mwenye IQ (Intelligence Quotient) chini ya 70.

Upungufu wa akili ni hali ya kuwa na mapungufu katika ukuaji (development deficit) yanayoanza utotoni ambayo husababisha kupungua uwezo wa kusoma (intellect), kutafakari, utambuzi na kutoweza kuendana na majukumu ya kila siku ya maisha.

Ukubwa wa Tatizo (Epidemiology)

Upungufu wa akili ni tatizo kubwa sana duniani.Huathiri asilimia 1-2 ya watu wote duniani.Huonekana sana kwa wanaume kuliko wanawake (inakisiwa huonekana mara mbili zaidi kwa wanaume kuliko wanawake). Upungufu wa akili wa kati (mild mental retardation) huonekana sana kwa watu wa kipato cha chini lakini upungufu wa akili wa kiwango cha juu hutokea uwiano sawa katika jamii ya matabaka yote na huonekana sana katika umri kati ya miaka 10 hadi 14.

Upungufu wa akili sio ugonjwa (axis II disorder in DSM-IV) kutokana na dalili na viashiria vyake bali ni tatizo la mfumo wa utambuzi wa watu wenye kuhitaji huduma za kijamii na elimu maalum ili kuweza kumudu majukumu yao ya kila siku. Mara nyingi upungufu wa akili hutokea kabla ya mtu kufikisha umri wa miaka 18.

Tungependa kwa yoyote mwenye takwimu kutoka afrika mashariki za tatizo hili la upungufu wa akili kutoka katika hospitali za magonjwa ya akili za Butabika National Referral and Teaching Mental Hospital (Kampala, Uganda), Port Reitz District Hospital (Mombasa, Kenya), Mathare Mental Hospital (Nairobi, Kenya), Lutindi Mental Hospital (Tanga, Tanzania) na Mirembe Psychiatric Referral Hospital (Dodoma, Tanzania).

Tabia za Kuendana na Mazingira (Adaptive behavior) ni nini?

Tabia za kuendana na mazingira ni jinsi mtu anavyoweza kumudu matakwa ya kujihudumia mwenyewe kila siku pasi na kumtegemea mtu yoyote kutokana na umri wake, tabaka lake, utamaduni pamoja na jamii inayomzunguka kutokana na vipengele viwili kati ya hivi vifuatavyo;

  • Mawasiliano (Kuweza kuwasiliana na watu)
  • Kuweza kujihudumia katika shughuli zinazohitaji kutumia akili (functional academic skills)
  • Kuweza kuishi mazingira ya nyumbani na kazini
  • Kuwa na uwezo wa kuchanganyikana na jamii katika masuala ya afya na usalama wake
  • Kuweza kutumia huduma za jamii ambazo zitamfanya kuishi maisha ya furaha

Ni vizuri kutambua ya kwamba tabia hizi hutegemea sana elimu, uhamasishaji, tabia za mtu binafsi, kupewa fursa za kijamii na za kiufundi (vocational skills), matatizo ya akili na magonjwa mbalimbali ya akili.

Intelligence kitaalamu ni uwezo wa ubongo katika kufikiri, kutatua matatizo, kuchagua au kuwa na busara (reason), na kuelimika.

IQ= Mental age (Umri wa akili) × 100

Chronological age (Umri wa kawaida wa binadamu)

Makundi ya Upungufu wa Akili Kipimo cha IQ

Upungufu wa akili uliopitiliza kabisa (Profound Mental Retardation) Chini ya 20

Upungufu wa akili mkubwa (Severe Mental Retardation) 20-34

Upungufu wa akili wa kati (Moderate Mental Retardation) 35-49

Upungufu wa akili (Mild Mental Retardation) 50-69

Upungufu wa akili wa kawaida (Borderline Intellectual Functioning) 70-84

Mtu aliye kwenye kundi la upungufu wa akili (Mild Mental Retardation) anaweza kuelimika, na Yule aliye na upungufu wa akili wa kati, mtu huyu anaweza kufunzwa kazi za kumuwezesha kumudu maisha yake ya kila siku. Wale walio na upungufu wa akili mkubwa (Severe MR) na kundi la waliopitiliza (Profound MR) hawawezi kufunzwa chochote na kufundishika.

Kwa hiyo mtoto aliye na umri sawa wa akili na umri sawa wa kibinadamu atakuwa na kipimo cha akili 100 (yaani IQ=100). Kwa wale watoto wenye vipaji maalum, kipimo cha akili yao huwa zaidi ya 100 (IQ>100), na kwa wale wenye akili ya kawaida kipimo cha akili huwa chini ya 100 lakini hakishuki chini ya 85.

Upungufu wa Akili wa Kawaida (Borderline Mental Retardation)

Huwa na akili yakipimo cha IQ= 70-85%. Wanauelewa mdogo shuleni (Slow learners) lakini wanaishi maisha ya kawaida yaani bila kupata taabu yoyote katika maisha yao ya kila siku na wanaweza kuajiriwa.

Upungufu wa akili (Mild Mental Retardation)

Huwa na akili ya kipimo cha IQ=50-70. Asilimia kubwa ya watu wenye upungufu wa akili huwa kwenye kundi hili (asilimia 85-95). Wanatambulika kama wanaoweza kuelimika. Wanaweza kujifunza kusoma, kuandika, na kufanya hesabu rahisi rahisi (simple arithmetic calculations). Hawa wanahitaji shule maalum ili waje kuweza kumudu majukumu yao ya maisha ya kila siku baada ya muda mrefu.Wanakuwa na upungufu mdogo katika uwezo wao wa kuhisi na utambuzi wa vitu (minimal sensorimotor deficits) na ni vigumu kutambua kwamba wanaupungufu wa akili mpaka baadae maishani. Katika ujana wao wanaweza kupata elimu hadi darasa la sita.Ukubwani, hupata uwezo wa kujihudumia wenyewe katika mahitaji yao ya kila siku lakini wanahitaji uangalizi, ushauri, kupewa mwongozo katika majukumu yao ya kifamilia na hasa wanapopata msongo wa mawazo au wakati wamepata matatizo ya kiuchumi.

Upungufu wa Akili wa Kati (Moderate Mental Retardation)

Huwa na akili yakipimo cha IQ=35-50. Asilimia 10 tu ya watu wote wenye upungufu wa akili ndio huwa kwenye kundi hili.Wanatambulika kama wasioweza kufundishika (untrainable) ingawa wengi wao wanaweza kuelimika. Utotoni mwao wanakuwa na mawasiliano mabaya ya kijamii, lakini wanaweza kujifunza kuzungumza, kutambua majina yao na baadhi ya maneno rahisi ambapo kutokana na haya ambayo nimeelezea hapo juu, kwa sasa wanatambulika kama kundi linaloweza kufundishika.Kawaida, huacha shule baada ya kufika darasa la pili (Standard 2). Wanaweza kufundishika katika kazi ambazo hazihitaji kutumia akili ama kazi za mikono.Msongo wa mawazo huathiri mafunzo yao hivyo ni muhimu kuboresha mazingira yao na kuwahudumia vizuri ili wasipate msongo wa mawazo.

Mara nyingi, uwezo wao wa kuelewa watu wanapozungumza ni mzuri kuliko uwezo wao wa kuzungumza na hii huwafanya kupata msongo wa mawazo. Uzungumzaji wao ni wa kawaida na hueleweka vizuri na wale wanaoishi nao au wale wanaofahamiana nao vizuri. Vitendo kama uvaaji nguo, kula, na kujiweka msafi, huchukua muda mrefu kwao kujifunza. Wanahitaji msaada katika matumizi ya hela na hata kuvuka barabara.

Upungufu wa Akili Mkubwa (Severe Mental Retardation)

Huwa na akili ya kipimo cha IQ=20-35 na huonekana kwa watu wenye upungufu wa akili kwa asilimia 5 tu. Hutambulika mapema kwa kutokuwa na uwezo wa kutambua vitu mbalimbali (Poor motor development). Watu hawa hawana uwezo wa kuzungumza na kuwasiliana au hupata uwezo huo baadae maishani. Huitaji shule maalum pamoja na wataalamu wa tiba ya sauti ili waweze kujifunza kuzungumza.Chini ya uangalizi, huweza kujifunza shughuli ndogondogo.

Upungufu wa Akili Uliopitiliza (Profound Mental Retardation)

Huwa na akili ya kipimo cha chini ya 20 yaani IQ<20. Asilimia 1-2 ya watu wenye upungufu wa akili ndio walio kwenye kundi hili. Mara nyingi wanakuwa na ugonjwa au matatizo ya sehemu ya mishipa ya fahamu ambayo husababisha upungufu wa akili.Dalili za kuwa na uwezo finyu wa kutambua na kuhisi mambo mbalimbali, kushindwa kuelimika, kujihudumia, kufanya kazi, kujitunza huonekana mapema sana. Huitaji msaada wa kijamii pamoja na kuhudumiwa katika maisha yao ya kila siku.

Aina za Upungufu wa Akili

Kuna aina mbili za upungufu wa akili ambazo ni

  • Syndromic mental retardation – Hii ni upungufu wa akili (intellectual deficits) unaoambatana na magonjwa mbalimbali pamoja na viashiria na dalili za kitabia (behavioral signs).
  • Non syndromic mental retardation – Upungufu huu wa akili hausiani na magonjwa au ugonjwa wowote.

Pathofiziologia (Pathophysiology)

Upungufu wa akili ni mjumuiko wa matatizo katika mfumo wa fahamu (CNS functions) ambapo sehemu inayojulikana kama cortical structures (ambayo huusisha pamoja na sehemu zingine kama hippocampus na medial temporal cortex) ndio huathirika. Watu wengi wenye upungufu wa akili hawaonyeshi kuathirika katika mfumo wao wa fahamu. Ni aslimia 10-15 ya watu wote wenye upungufu wa akili ambao ndio wanaonyesha kuathirika katika mfumo wao wa fahamu.

Matatizo katika mfumo wa fahamu ambayo huonekana sana ni kichwa maji (hydrocephalus), neural tube defects, microcephaly na (disorders of migration- the lissencephalis na muunganiko wa mwatuko wa ubongo {agenesis of corpus carlosum} ambayo huonekana mara chache).

Watu wengi wenye upungufu wa akili aina ya mild mental retardation na wenye matatizo mengine ya ufahamu (other learning disorders), huwa hawana matatizo katika mfumo wao wa fahamu, madhara katika neva na dysmorphisms lakini wana uwezekano mkubwa wa kutoka katika familia zenye hali duni ya kiuchumi, familia yenye kipimo cha akili ndogo (low IQ), na elimu duni.

Nini husababisha upungufu wa akili?

Zipo sababu nyingi ambazo husababisha upungufu wa akili ambazo ni kama ifuatavyo

  • Matatizo ya kurithi (genetic factors)
  • Antenatal factors
  • Postnatal factors
  • Matatizo ya kijamii na kitamaduni (socio-cultural factors)
  • Magonjwa ya akili (psychiatry disorders)

Thuluthi moja (1/3) ya watu wenye upungufu wa akili chanzo hasa hakijulikani.

Matatizo ya viashiria vya urithi (genetic factors)

  • Chromosal abnormalities kama down syndrome, fragile X syndrome (mgonjwa anakuwa na kichwa kikubwa, masikio makubwa kama ya popo, uso mrefu, korodani kubwa kupitiliza na nyayo zinakuwa bapa {flat feet},huwa na matatizo ya lugha na sauti, hii husababishwa na matatizo katika ncha ya mkono mrefu wa chromosome)
  • Metabolic disorders kama phenylketonuria, homocystinuri, galactosemia nk.
  • Magonjwa kwenye ubongo (Gross disease of the brain) kama cerebral dysgenesis, tuberose sclerosis, neurofibrosis nk.
  • Madhara ya kwenye ubongo (brain malformations) kama nueral tube defects, kichwa maji na microcephalus

Antenatal factors

Matatizo ambayo hutokea wakati mtoto bado hajazaliwa (yaani yanayompata mtoto wakati bado yupo tumboni mwa mama yake). Haya yanaweza kuwa;

  • Magonjwa kama ugonjwa wa kaswende (syphilis), TORCH
  • Sumu (intoxications) kama madini ya risasi (lead), madawa ya kulevya, unywaji pombe wakati wa ujauzito nk.
  • Physical damage – Tiba ya mionzi au vipimo vya mionzi, injury, ukosefu wa hewa ya oksijeni kwa mtoto (hypoxia).
  • Matatizo ya kondo la uzazi (Placental dysfunctions) – Toxaemia, ukosefu wa virutubisho sahihi katika ukuaji wa kondo (Nutritional growth retardation).
  • Matatizo katika mfumo wa vichocheo mwilini (Endocrine disorders) – Hypothyroidism (ugonjwa wa tezi la koo), ugonjwa wa kisukari kwa mama mjazito, hypoparathyroidism.

Perinatal factors

Matatizo yanayotokea wakati mtoto anazaliwa (wakati wa kujifungua kwa mama mjazito)

  • Ukosefu wa hewa ya oksijeni (Birth asphyxia), cerebral palsy nk
  • Madhara ya mtoto kuzaliwa njiti (complications of prematurity) kama uvujaji damu ndani ya ubongo (intraventricular haemorrhage).
  • Hypoxic Ischemic encephalopathy

Post-natal factors

Matatizo yanayotokea baada ya mtoto kuzaliwa

  • Injury – Head injury (kuumia kichwa)
  • Sumu (Intoxication) kutokana na madini ya risasi, mercury nk.
  • Magonjwa kama ugonjwa wa uti wa mgongo (meningitis), encephalitis (maambukizi kwenye ubongo)

Socio-cultural factors (Matatizo ya kijamii na kitamaduni)

Kutokuwa na uwezo wa kujumuika na jamii huchochewa na ukosefu wa elimu, kiwango duni cha uhamasishaji, tabia ya mtu, ucheshi wa mtu,utapia mlo, mimba za utotoni (kwani huleta umaskini, utapia mlo, afya duni, kuathirika kwa mama na hivyo kumuathiri mtoto), vocational opportunities pamoja na magonjwa ya akili na magonjwa mbalimbali. Kukosekana kwa vichocheo hivyo au kuwepo kwa magonjwa ya akili na baadhi ya magonjwa mbalimbali huweza kusababisha upungufu wa akili. Ikumbukwe ya kwamba akili ya mtoto huwa inakuwa kwa hiyo ni muhimu apewe fursa ya kuweza kukuza akili yake.

Magonjwa ya akili (Psychiatric disorders)

  • Pervasive developmental disorders (Autistic spectrum disorders)

----USIKOSE KUFUATILIA MWENDELEZO WA MAKALA HII----

Imesomwa mara 9682 Imehaririwa Jumatano, 23 Oktoba 2019 17:34
Dr Khamis

Dr. Khamis H.Bakari (MD PhD) ni daktari bingwa,mhadhiri katika chuo cha afya cha Chuo  Kikuu cha Dodoma,mtaalamu wa Tiba na Uchunguzi kwa kutumia mionzi ya nyuklia (Nuclear medicine).

Anwani ya barua pepe hii inalindwa kutokana na spambots. JavaScript lazima iwe itawezeshwa kwa kuweza kuona.