Image

Magonjwa ya Zinaa - 1: (Sexual Transmitted Diseases)

Kati ya magonjwa yanayoathiri watu wengi sana duniani ni magonjwa ya zinaa. Haya ni magonjwa yanayoambukizwa kutoka kwa mtu mmoja kwenda kwa mwingine kupitia vitendo vya ngono. Vitendo hivi vya ngono vinaweza kuwa kujamiana, kupiga denda (kissing), vitendo vya ngono kwa kutumia mdomo (oral genital sex), kujamiana kupitia njia ya haja kubwa (anal sex) iwe kwa mwanamume na mwanamke au kati ya wanaume wenyewe na hata wale wanaotumia vifaa vya kufanyia ngono (vibrators). Magonjwa ya zinaa huathiri sana watu walio katika umri wa miaka 15 – 24 lakini hata kwa watu wengine ambao wana umri chini au zaidi ya huu niliotaja pia yanaonekana kwa wingi.

Kuna magonjwa ya zinaa zaidi ya ishirini yanayotambulika duniani, baadhi ya magonjwa ya zinaa ni

  • Kisonono (Gonorrhoea – “Gono” kama wengi wanavyopenda kuita kwa kifupi).
  • Chlamydia
  • Kaswende (Syphillis)
  • Human papilloma virus (HPV)
  • HIV/AIDS (Ukimwi/Upungufu wa kinga mwilini)
  • Hepatitis B, C, A
  • Herpes virus
  • Trichomoniasis
  • Bacteria Vaginosis
  • Pubic lice (chawa kwenye nywele za kinena)
  • Chancroid

Magonjwa mengi ya zinaa yanatibika lakini kuna baadhi ambayo hayana tiba ya uhakika kama HPV, Hepatitis B na C, na HIV. Mengine yameanza kuwa sugu kutokana na matumizi ya dawa za antibiotics bila mpangilio, magonjwa hayo ni kama gono (gonorrhoea) na nk.

Visababishi vya magonjwa ya zinaa

  • Vitendo vya ngono kama nilivyoeleza hapo awali
  • Kuanza vitendo vya ngono mapema au wakati wa umri mdogo
  • Kuwa na wapenzi wengi
  • Kufanya mapenzi ambao sio salama
  • Maambukizi kupitia michibuko au sehemu zilizokatika kwenye ngozi kwa kugusana na majimaji ya aina yoyote yanayotoka kwa mtu mwenye ugonjwa wa zinaa kama damu, shahawa nk. Hii inaweza kutokea bila mtu kujua kwani mara nyingi dalili za magonjwa ya zinaa zinakuwa hazionekani kwa wanawake na hata baadhi ya wanaume.

Watu wengi huhisi kitendo cha kula denda (kissing) ni salama lakini si kama wanavyofikiria kwani baadhi ya magonjwa kama kaswende, herpes nk, yanaweza kuambukizwa kupitia njia hii. Kondomu husaidia kupunguza maambukizi ya magonjwa ya zinaa kama gono, Chlamydia lakini sio kinga muafaka dhidhi ya magonjwa ya zinaa kama kaswende, genital herpes, genital warts, na magonjwa ya upungufu wa kinga mwilini (AIDS).

Nitaanza kuzungumzia ugonjwa wa gono (gonorrhea) kwa leo na makala zitakazofuata nitakuwa nazungumzia ugonjwa mmoja baada ya mwengine

Kisonono (gonorrhea) ni nini?

Kisonono ni ugonjwa kati ya magonjwa ya zinaa unaosababishwa na bakteria aina ya Neisseria gonorrhoeae, bakteria ambao hukuwa na kuzaliana kwa haraka katika sehemu zenye unyevunyevu na joto mwilini kama kwenye shingo ya kizazi kwa wanawake (cervix), mirija ya kupitisha mkojo au shahawa (urethra), mdomoni na kwenye puru. Maambukizi mengi kwa wanawake hutokea kwenye shingo ya kizazi (cervix). Asilimia 75 ya ugonjwa wa gono hutokea kwa watu wenye umri wa miaka 15 – 29, wanawake walio katika umri wa miaka 15 -19 na wanaume walio katika umri wa miaka 20 – 24 wako kwenye hatari zaidi ya kupata ugonjwa huu.

Ugonjwa huu huambukizwa vipi?

Ugonjwa huu huambukizwa kupitia vitendo vya ngono kupitia uke, njia ya haja kubwa (anus), kupitia mdomoni (oral sex). Ugonjwa unaweza kujitokeza kwenye sehemu za kujamiana, kwenye mdomo na kwenye puru (rectum). Ugonjwa wa gono huonekana sana kwa vijana, watu wenye maisha duni kiuchumi, watu wanaoishi mijini, watu weusi na watumiaji madawa ya kulevya.

Dalili za ugonjwa wa kisonono

Dalili za ugonjwa wa kisonono huanza kujitokeza kuanzia siku ya 2 hadi ya 7 baada ya mtu kupata maambukizi na huweza kuchelewa kwa wanawake. Dalili ni kama zifuatazo

Kwa wanaume

  • Kuhisi kama kichomi wakati wa kukojoa (burning sensation)
  • Kutokwa na majimaji ya njano au meupe au ya kijani kutoka kwenye uume yanayoambatana na maumivu makali sana
  • Wakati mwengine maumivu au kuvimba kwa korodani (swollen testicles)
  • Maambukizi yakiwa kwenye puru (rectum) huambatana na maumivu wakati wa kujisaidia haja kubwa, kuwashwa sehemu za haja kubwa, na hata haja kubwa inaweza kutoka ikiambatana na damu, hii inatokea kwa wanaume na wanawake.

Kwa wanawake

Dalili kwa wanawake huwa si nyingi lakini wanawake wengi hawaonyeshi dalili zozote

  • Maumivu au kuhisi kama kichomi wakati wa kukojoa
  • Kuongezeka kwa kutoka majimaji kutoka kwenye tupu ya mwanamke ambayo ni ya njano au yamechanganyika na damu
  • Kutokwa na damu kupitia tupu ya mwanamke kabla ya hedhi kufika.
  • Kutokwa na damu baada ya kujamiana au baada ya tendo la ndoa
  • Kichefuchefu
  • Homa (fever)
  • Kutapika

Vipimo vya ugonjwa wa kisonono

  • Swab for culture – Kipimo hiki hufanyika maabara kwa kupandikiza bakteria baada ya kufuta sehemu za siri kwa kutumia swab ili kuona kama kuna bakteria wanaosababisha gono.
  • Polymerase Chain Reaction (PCR) – Kipimo cha kuangalia vina saba (DNA) ya bakteria, ni ghali sana.

Tiba ya ugonjwa wa kisonono ni nini?

Tiba ya gono inahusisha na tiba ya ugonjwa wa Chlamydia kwani mara nyingi magonjwa haya huambatana kwa pamoja.Tiba hutegemea na umri wa mgonjwa na kama mtu ni mjamzito au la. Tiba ya gono ambayo sio sugu iliyo kwenye shingo ya kizazi (cervix), urethra na puru, dawa zinazotumika ni aina za cephalosporin dozi moja pamoja na dawa za aina ya macrolide antibiotics (mfano azithromycin) na za jamii ya penicillin (mfano doxycyclin) ili kutibu ugonjwa wa chlamydia. Mara nyingi kwa wale chini ya miaka 18 na wanawake wajawazito, hutibiwa kwa kuchomwa sindano.

Fuata ushauri wa daktari kabla ya kutumia dawa hizi kwani dawa nyingi zina madhara kwa wajawazito (mfano doxycyclin). Ushauri nasaha hutolewa kwa wapenzi wote wawili na ni vizuri wapenzi wote wawili kutibiwa hata kama mmoja hana dalili za ugonjwa huu.

Madhara ya ugonjwa wa kisonono

  • Kutoweza kuzaa kwa mwanamke (tasa) au kutoweza kutungisha mimba kwa mwanamume (infertility)
  • Huweza kuathiri moyo (heart valves), ubongo,ngozi nk ambayo ni hatari sana kwa mtu yoyote.
  • Madhara kwenye sehemu za maungio au jointi (joint inflammation)
  • Kwa wanawake wale ambao hawajatibiwa wanaweza kupata ugonjwa wa PID (Pelvic Inflammatory Disease) ambao huongeza asilimia ya mwanamke kuwa tasa.
  • Wale wanawake ambao ni wajawazito na wameambukizwa gono wako kwenye hatari ya mimba kutoka au kuzaa mapema kabla mimba haijatimiza umri wake (preterm labor).
  • Kwa wale wanaoambukizwa gono kipindi cha kukaribia kujifungua, wanaweza kuwaambukiza watoto wao na hivyo watoto kupata ugonjwa wa uti wa mgongo (meningitis), kuwa kipofu (blindness), homa ya mapafu (pneumonia) na ugonjwa wa mifupa (septic arthritis).

Kinga ya kisonono

  • Kutumia kondomu wakati wa kujamiana
  • Kuwa na mpenzi mmoja mwaminifu
  • Kuacha vitendo vya ngono kama matumizi ya vifaa vya ngono hasa kwa wanawake mfano vibrators nk.
  • Kwa wanawake wajawazito – Hakikisha unahudhuria kliniki mapema ili upate kuchunguzwa na kupatiwa tiba muafaka kama utagundulika na ugonjwa wa gono au ugonjwa mwengine wowote.
  • Wanawake wajawazito wanashauriwa kujifungulia hospitali ili kama mtoto ameathirika na gono apate matibabu ya haraka baada ya kuzaliwa kuepusha kuwa kipofu.
  • Epuka kufanya ngono na mtu aliyeambukizwa gono.

“Kumbuka ya kwamba hakuna kitu kama ngono salama kwani huwezi kujua kama wewe au mwenzako wakati wa kujamiana ameathirika au la, au una michibuko au umekatika kwenye ngozi au la kwani michibuko mengine inaweza isionekane au kugundulika kwa urahisi. Njia pekee na nzuri ni kuacha au kujikinga na vitendo vya ngono”. Mtu aliyepata gono awali anaweza kupata tena.

Usikose mwendelezo wa makala hii.........

 

Imesomwa mara 17803 Imehaririwa Alhamisi, 05 Julai 2018 15:17
Dr Khamis

Dr. Khamis H.Bakari (MD PhD) ni daktari bingwa,mhadhiri katika chuo cha afya cha Chuo  Kikuu cha Dodoma,mtaalamu wa Tiba na Uchunguzi kwa kutumia mionzi ya nyuklia (Nuclear medicine).

Anwani ya barua pepe hii inalindwa kutokana na spambots. JavaScript lazima iwe itawezeshwa kwa kuweza kuona.

Makala shabihana