Image

Usumu/Maambukizi kwenye chakula (Food poisoning): Yaweza kuzusha tafrani

Si mara chache tumewahi kushuhudia au kusikia mtu au kundi la watu likiugua ghafla baada ya kula chakula katika mkusanyiko au sherehe. Bila shaka nawe ni mmojawapo wa waliowahi kukumbwa na hali hii.

Aidha tumewahi pia kusikia au kushuhudia hata baadhi ya watu wakiamini kulishwa sumu baada ya kula chakula katika shughuli au sherehe fulani. Hali hii imewahi kuzusha tafrani na sintofahamu miongoni mwa wanajamii kwa vile si wengi wanaofahamu hasa chanzo cha hali hiyo.

Lakini usumu au maambukizi katika chakula (food poisoning) ni nini hasa?

Food poisoning ni hali ya kuchafuka kwa chakula kunakotokana na uwepo wa vimelea mbalimbali kama vile bacteria, virusi, au parasites au sumu zao ndani yake. Hali hii hutokea wakati unapokula chakula au kunywa vinywaji/maji yaliyochanganyika na vimelea hawa hususani vya bacteria wa jamii ya Staphylococcus au Escherichia coli (E. coli).

Ieleweke kuwa food poisoning haimaanishi sumu inayowekwa na mtu/watu kwenye chakula bali hutokana na vijidudu vya magonjwa mbalimbali kama vile bacteria.

Vihatarishi vyake

Kwa kawaida food poisoning hutokea zaidi baada ya kula vyakula vilivyoandaliwa kwenye mikusanyiko kama vile cafeteria za shule au kazini, kwenye misiba, matanga, hitma, maulid, ngoma, harusi, mahoteli, na mikusanyiko mingine yeyote ambayo inahusisha ulaji wa chakula cha pamoja; ambapo mtu mmoja au kundi la watu hupatwa na usumu huo na kuwa wagonjwa.

Watoto wadogo chini ya mwaka mmoja pamoja na wazee ni miongoni mwa makundi ya watu wanayoongoza kuwa katika hatari ya kuathirika zaidi na tatizo hili. Wengine ni pamoja na watu wenye matatizo ya kiafya kama vile magonjwa ya figo au kisukari, wenye upungufu wa kinga ya mwili, na wasafiri wanaotembelea maeneo yanayojulikana kuwa na vimelea wanaosababisha hali hii kwa wingi.

Visababishi

Kama ilivyotangulia kuelezwa hapo awali, food poisoning husababishwa na sumu inayotokana na vimelea vya bacteria, virusi, au parasites. Vimelea hawa hujumuisha bacteria jamii ya
• Clostridium botulinum wanaosababisha usumu unaoitwa botulism
• Campylobacter wanaosababisha uambukizi kwenye utumbo mdogo kuharisha na kutapika
• Vibrio cholera wanaosababisha kipindupindu
• E. coli ambao pia husababisha uambukizi katika utumbo mdogo, kuharisha na kutapika
• Bakteria wengine ni pamoja na Staphylococcus aureus, Salmonella, Listeria na Shigella ambao husababisha kuharisha damu, na aina fulani ya bacteria wanaopendelea kuishi kwenye magamba ya samaki.

Vimelea vya sumu huingiaje kwenye chakula?

Kuna njia kadhaa ambazo hutumiwa na bacteria kuvamia chakula na hatimaye kuzalisha sumu zao na hivyo kukichafua. Njia hizo ni pamoja na
• Maandalizi pamoja na upikaji mbaya wa chakula
• Maji yasiyo safi na salama yanaweza kuwa na kinyesi cha binadamu au wanyama ambacho huwa kimebeba vimelea hawa
• Nyama inapogusana na utumbo/matumbo ya wanyama yenye vimelea hawa wakati wa kuchinja, kuchuna ngozi na kuandaa nyama

Aidha mtu anaweza kupata food poisoning baada ya kula au kunywa

• Chakula kilichoandaliwa na mtu mwingine au yeye mwenyewe bila kusafisha vema mikono yake
• Chakula kilichoandaliwa kwa kutumia vyombo vichafu kama vile masufuria machafu, majungu, vijiko, visu, vikombe, sahani au vyombo vingine vinavyotumika kuandaa au kulia chakula.
• Vyakula vya jamii ya maziwa, jibini, mtindi ambao umewekwa kwenye friji kwa muda mrefu bila uangalizi wa kutosha.
• Vyakula vilivyohifadhiwa kwenye jokofu katika joto lisilo sahihi bila kuvipasha tena moto
• viporo visivyohifadhiwa vema
• samaki wabichi/wasioiva au kamba kochi
• matunda au mboga mboga mbichi zisizooshwa vizuri
• saladi isiyoandaliwa vema
• nyama isiyoiva vema au mayai mabichi
• maji kutoka katika bomba bila kuchemsha hususani kama limepasuka

Zipi ni dalili za food poisoning?

Dalili za mtu mwenye food poisoning hutegemea na aina ya vimelea wanaosababisha hali hii. Kwa kawaida, vyanzo vingi vya food poisoning huwa na dalili zinazojitokeza ndani ya saa 2 mpaka 6 tangu mtu anapokula chakula chenye usumu. Baadhi ya dalili za ujumla ni pamoja na
• maumivu ya tumbo. Tumbo huwa kama linakata au kusokota.


• Homa na kujihisi baridi
• Kuumwa kichwa
• Kichefuchefu na kutapika
• Kuharisha, kulingana na chanzo mtu anaweza kuaharisha majimaji au kuharisha damu
• Mwili kuwa dhaifu na kulegea. Ulegevu wa mwili unaotokana na usumu wa botulism waweza kuwa mbaya sana kufikia kusababisha mtu kushindwa kupumua sawasawa na hatimaye kifo.

Vipimo na uchunguzi

Mara unapofika kwa hospitali, daktari pamoja na kukuuliza maswali ili afahamu vizuri historia na chanzo cha ugonjwa, pia atakupima ili kutambua viashiria vingine kama vile upungufu wa maji mwilini au maumivu ya tumbo. Daktari atakuuliza kuhusu vyakula au vinywaji ulivyokula na kunywa saa kadhaa zilizopita, kama uliandaa mwenyewe au la, ulikuwa au kunywa wapi, kama kuna wengine wenye dalili kama zako, dalili nyingine kama kuharisha, kutapika, vichefuchefu, maumivu ya tumbo, homa au dalili nyingine kama zilivyotajwa hapo juu.

Daktari pia anaweza kushauri ufanyike uchunguzi kama wa damu, mkojo, choo, matapishi, au masalia ya vyakula ili kutambua chanzo cha ugonjwa wako. Hata hivyo ieleweke kuwa wakati mwingine vipimo hivi vinaweza kushindwa kuthibitisha kwamba ugonjwa wako unatokana na kuwepo kwa usumu kwenye chakula. Baadhi ya wagonjwa wanaoharisha damu wanaweza kuhitaji kufanyiwa vipimo zaidi ili kutambua chanzo cha kuharisha damu ili kujiridhisha kuwa hakuna uhusiano na food poisoning.

Matibabu

Wagonjwa wengi wa food poisoning kwa kawaida hupona kabisa baada ya siku chache tangu kujitokeza kwa dalili. Jambo la msingi ni kuhakikisha unaendelea kula na kunywa vinywaji au maji ya kutosha ili kurejesha kiasi chochote cha maji kitakachopotea kutokana na kuharisha au/na kutapika.

Haishauriwi kula vyakula vigumu mpaka kuharisha kutakapokoma, na jiepushe kula vyakula vya jamii ya maziwa (maziwa, mtindi) ili kupunguza uwezekano wa kuharisha zaidi, wakati huo huo kunywa maji ya kutosha au vinywaji vingine kwa wingi.

Watoto wadogo ni vema wapewe maji yenye madini maalum ya ORS au kama hayapatikani, maji yenye mchanganyiko wa chumvi na sukari hufaa sana. Wagonjwa hususani watoto wanaoharisha na kutapika na ambao hawawezi kunywa maji wala vinywaji kwa sababu ya kutapika hawana budi kutibiwa kwa kutumia drip (i.v. fluids) ili kurejesha maji yaliyopotea.

Mara nyingi, matibabu ya food poisoning hayahusishi utumiaji wa dawa za jamii ya antibiotics isipokuwa mara chache sana daktari wako anaweza kushauri utumie dawa hizo hususani kama kunaambatana na kuharisha damu.

Nini cha kutarajia kwa mtu aliyepatwa na food poisoning?

Kwa kwaida watu wengi wenye kupatwa na hali hii hupata nafuu kamili ndani ya saa 12 mpaka siku mbili; ingawa wapo baadhi ambao hali zao zinaweza kuwa mbaya sana. Ni mara chache food poisoning husababisha kifo lakini kama mgonjwa anaharisha sana na kutapika bila kutibiwa, kifo kinaweza kutokea kwa sababu ya upungufu mkubwa wa maji mwilini.

Nini madhara ya hali hii?

Madhara yaliyozoeleka zaidi ya hali hii ni upungufu wa maji mwilini unaotokana na kutapika na kuharisha kupita kiasi bila kurejesha maji yanayopotea.

Madhara mengine hutegemeana na aina ya bacteria anayesababisha ugonjwa huu. Bacteria wengine husababisha madhara kama vile magonjwa ya figo, matatizo ya kutokwa damu bila kukoma, magonjwa ya viungo vya mwili, magonjwa ya mfumo wa fahamu, na madhara katika moyo.

Kinga ni bora kuliko tiba

Kujikinga ni bora kuliko kusibiri mpaka tatizo litokee. Unashauriwa kuepuka kula vyakula ambavyo ubora na usafi wake unatia shaka. Aidha epuka kunywa vinywaji au maji ambayo si safi na salama pamoja na kuacha kula nyama au samaki wasiopikwa vizuri.

Unashauriwa kwenda hospitali haraka iwapo utaona damu au usaha katika kinyesi chako, kinyesi kimekuwa cha rangi nyeusi, tumbo linazidi kusokota hata baada ya kujisaidia, kujihisi dalili za kukaukiwa maji mwilini kama vile kiu, kizunguzungu au kujihisi kichwa chepesi, kuharisha pamoja na homa kali, moyo unakwenda kasi au una dalili nyingine za tatizo hili.

Imesomwa mara 7465 Imehaririwa Jumatatu, 18 Februari 2019 16:42
Dr Fabian P. Mghanga

Daktari bingwa na Mhadhiri katika kitivo cha Afya Chuo Kikuu Kishiriki cha Askofu Jacob, Songea

Anwani ya barua pepe hii inalindwa kutokana na spambots. JavaScript lazima iwe itawezeshwa kwa kuweza kuona.

Makala shabihana