Image

Ugonjwa wa Figo Unaotokana na Kisukari (Diabetic nephropathy)

Moja ya madhara ya ugonjwa wa kisukari katika mwili wa binadamu ni ugonjwa wa figo (diabetic nephropathy). Ugonjwa huu ambao huwapata watu wenye kisukari, hutokea muda mrefu baada ya mtu kugunduliwa kuwa na kisukari.

Kinachotokea (Pathofiziolojia)

Figo zinaundwa na mamia kwa maelfu ya vijiumbo vidogo vidogo viitwavyo nefroni (nephrons). Kazi ya hizi nefroni ni kuchuja damu na kutoa uchafu mwilini mwako kwa njia ya mkojo.

Kwa watu wenye kisukari, nefroni huwa na tabia ya kukakamaa, kuzeeka na kuwa na makovu kadiri miaka inavyopita. Baada ya muda fulani, hushindwa kabisa kazi yake ya kuchuja uchafu, matokeo yake protini ambazo kwa kawaida huwa haziwezi kuchujwa, huchujwa na kutoka katika mkojo.

Chanzo hasa cha kuzeeka, kukamaa na kuwa makovu huku kwa nefroni hakijulikani. Hata hivyo inadhaniwa kuwa uthibiti mbaya wa sukari husababisha uharibifu wa figo, na madhara huongezeka maradufu kwa watu wenye shinikizo la damu lisilothibitiwa na kisukari kwa pamoja.

Ukubwa wa tatizo

Ifahamike kuwa si kila mwenye kisukari anaweza kupata ugonjwa wa figo. Inasemekana, kwa baadhi ya watu, hali hii ina uhusiano mkubwa na historia ya kisukari katika familia.

Wagonjwa wa kisukari ambao pia ni wavutaji wa sigara, na wale wenye aina ya kwanza ya kisukari (type 1 Diabetes Mellitus) kilichoanza kabla hawajafika miaka 20, wana hatari kubwa ya kupata matatizo ya figo.

Dalili

Kwa kawaida, mtu mwenye tatizo hili anaweza asioneshe dalili zozote katika miaka ya mwanzo ya ugonjwa. Mara nyingi dalili huanza kujitokeza miaka 5 mpaka 10 baada ya figo kuathirika. Dalili huanza taratibu kabla ya kuwa dhahiri.

Dalili kwa watu waliopata madhara makubwa katika figo hujumuisha kukosa hamu ya kula, kujihisi uchovu na kwa ujumla kutojihisi vizuri. Dalili nyingine ni pamoja na kuumwa kichwa, kichefuchefu na kutapika, kuvimba miguu pamoja na dalili nyingine kama zilivyoainishwa katika ugonjwa sugu wa figo.

Vipimo na uchunguzi

Kwa watu wenye kisukari, ni vema kufanya uchunguzi wa figo zao walau mara moja kwa mwaka. Daktari wako kwanza atakuchunguza kama una dalili zozote zinazoashiria matatizo ya figo. Kipimo mojawapo ni kuchunguza mkojo kwa ajili ya kuchunguza kiwango cha protini aiitwayo albumin au microalbuminuria.

Kuwepo kwa kiasi kingi cha protini katika mkojo ni mojawapo ya dalili za kuwepo kwa tatizo katika figo.

Vipimo vingine ni pamoja na kiasi cha Urea Nitrogen katika damu (BUN), kiwango cha creatine katika damu (serum creatinine), kiasi cha protini katika mkojo wa saa 24 (24-hour urine protein), kiasi cha madini ya phosphorus, calcium, bicarbonate, PTH, na potassium katika damu, kiasi cha wingi wa damu (Hemoglobin), na wakati fulani kufanya biopsy ya figo kwa ajili ya uthibitisho wa tatizo.

Matibabu

Lengo kuu la matibabu ni kufanya figo zisiendelee kuathirika. Mojawapo ya njia bora kabisa za kusaidia hilo ni kuthibiti kiwango cha shinikizo la damu kuwa chini ya 130/80 mmHg.

Dawa za jamii ya Angiotensin Converting Enzyme inhibitors kama vile Captopril pamoja na zile za angiotensin receptor blockers zimeonekana kuwa na uwezo mkubwa wa kushusha shinikizo la damu wakati huo huo kuthibiti kasi ya kuharibika kwa figo kutokana na kisukari.

Kula lishe yenye kiwango kidogo cha mafuta, matumizi ya dawa za kuthibiti kiasi cha mafuta mwilini, na kufanya mazoezi mara kwa mara pia husaidia sana kuzuia au kupunguza kasi ya kuathirika kwa figo.

Aidha uthibiti wa kiwango cha sukari kwa kubadilisha aina ya chakula unachokula, kutumia dawa za kisukari kama inavyoshauriwa na daktari wako, na kuchunguza kiwango chako cha sukari mara kwa mara, husaidia pia katika kuzuia tatizo hili. Kwa mtu mwenye uambukizi katika njia ya mkojo (UTI) ni vema kutibiwa kwa kutumia antibiotics.

Matarajio

Ugonjwa wa figo unaotokana na kisukari ni mojawapo ya vyanzo vikuu vya kuugua na kifo kwa wagonjwa wa kisukari.

Hata hivyo, iwapo tatizo litagunduliwa katika hatua zake za awali, kuna uwezekano mkubwa wa kuzuia na kuthibiti uharibifu wa figo. Mara baada ya protini kuonekana katika kojo, uharibu wa figo huanza kuwa mkubwa na wa kutisha kiasi cha kuhitaji kufanyiwa dialysis au kubadilishwa kwa figo.

Hali kadhalika, watu wenye ugonjwa wa figo unaotokana na kisukari huwa wana magonjwa mengine kama vile shinikizo la juu la damu, magonjwa ya moyo pamoja na magonjwa ya macho.

Imesomwa mara 8274 Imehaririwa Jumatano, 11 Julai 2018 16:24
Lucy Johnbosco

Diabetes Consciousness for Community is focusing on raising Diabetes awareness and healthy lifestyle

https://dicoco.or.tz | Anwani ya barua pepe hii inalindwa kutokana na spambots. JavaScript lazima iwe itawezeshwa kwa kuweza kuona.

Makala shabihana