Image

Yajue Baadhi ya Magonjwa Yenye Uhusiano Mkubwa na UKIMWI Katika Kinywa na Maeneo ya Uso

Ukimwi  “upungufu wa kinga mwili”, ni ugonjwa unaoshambulia na kuua chembe chembe nyeupe za damu zinazosaidia mwili kupambana na magonjwa. Kutokana na upungufu huu wa kinga, magonjwa nyemelezi huanza kumpata muathirika wa ukimwi. Magonjwa yatokanayo na ukimwi uweza kujidhihirisha sehemu mbali mbali za mwili ikiwemo eneo la kinywa na uso. Kwa sasa nitaandika juu ya magonjwa ya eneo la kinywa na uso.

Fangasi za mdomoni (oral candidiasis)

Ugonjwa huu hujidhihirisha kama utando mweupe kwenye ulimi, paa la kinywa au kuta za kinywa, utando huu ni rahisi kukwanguliwa na kuacha ngozi laini yenye vipele vipele vyekundu. Wakati mwingine uonekana kama vipele vipele vyeupe kwenye kinywa.

Matibabu

Ugonjwa huu hutibika kwa kutumia dawa za kawaida za fangasi, ziwe vidonge, za maji au za kumun’gunya katika hali ya gel
 

       fangasi kwenye paa la kinywa        

                                                                                                                                

                     fangasi kwenye ulimi                              

Kaposi’s sarcoma

Hii ni kansa itakanayo na chembe chembe zinazotengeneza ngozi ya ndani ya mishipa ya damu.

Kansa hii ilikuwepo tangu zamani lakini imeongezeka kwa kasi baada ya kugundulika kwa Ukimwi. Tafiti nyingi kwa sasa zinaonyesha kansa hii ina uhusiano mkubwa na Ukimwi.

Kansa hii kwenye kinywa inajidhihirisha kama uvimbe tepetepe wenye rangi ya zambarau japo wakati mwingine nyekundu damu ya mzee.

Wakati mwingine yawezekana usiwe uvimbe bali eneo fulani la ngizi zilizo tanda kinywa kubadilika rangi na kuwa zambarau au nyekundu.

Kansa hii inaweza jitokeza sehemu yoyote mdomoni, kama kwenye ulimi, kuta za kinywa, paa la kinywa na kwenye fizi na hata kwenye tonsili.

Nje ya kinywa kwenye uso, kansa hii hushambulia mitoki iliyo chini ya kidevu na kwenye shingo. Mitoki uvimba bila sababu ilyo wazi (kwa kawaida mitoki uvimba kama kuna kidonda sehemu fualani au ugonjwa).

Matibabu: Kwa wagonjwa wa Ukimwi kansa hii ikijitokeza ni miongoni wa sababu za kuanza kutumia dawa za kupunguza makali ya Ukimwi hata kama kinga yako bado iko juu. Matibabu yanaweza kuwa upasuaji kuondoa uvimbe, mionzi kuunguza chembe chembe za kansa, dawa za kansa au muunganiko wa njia njia mbili kati ya hizo au zote kwa pamoja.


Magonjwa ya fizi

Kwa kawaida magonjwa ya fizi huwapata watu wasiopiga mswaki au wanaopiga mswaki isivyo paswa. Mara nyingi utakuta mtu mwenye magonjwa haya meno yakiwa na tando za uchafu na wadudu (dental plaque) au hata ugaga uliojishikiza kwenye meno kama miamba (calculus). Lakini kwa mgonjwa wa ukimwi waweza kuta kinywa ni kisafi lakini fizi zimejaa vidonda vidonda, na vidonda hivi husambaa kwa kasi.

Magonjwa haya fizi hushambulia pia mifupa inayoshikilia mizizi ya meno hivyo kupelekea meno kulegea na hatimaye kutoka

Matibabu yake ni Kusafisha meno na kutumia dawa za antibiotic za kusukutua na vidonge vya kumeza.

Kuvimba kwa tezi kubwa la mate lililopo jirani na sikio (parotid salivary gland enlargement)

Huku ni kuvimba hadi kuonekana kwa tezi la mate lililopo jirani ya sikio. Kwa kawaida tezi ili halionekani, hivyo ukiliona limevimba jua kuna tatizo. Ugonjwa huu huenda sambamba na kukauka kwa kinywa, kwani matezi haya ndiyo hutoa kiwango kikubwa cha mate mdomoni. Unaweza kuvimba tezi la upande mmoja au pande zote mbili.

Ugonjwa huu huweza kujiponea wenyewe lakini wakati mwingine yaweza kuhitaji matibabu.

Kuvimba kwa mitoki ya maeneo chini ya kidevu na shingo

Kama nilivyokwisha sema hapo juu, katika hali ya kawaida mitoki haionekani na wala huwezi kuihisi kwa kugusa. Ukiweza kuiona kwa macho kuwa imevimba au hata ukaweza kuihisi kwa kugusa hiyo ni dalili kwamba mitoki imevimba. Mbali ya majeraha na vidonda eneo la kinywa na uso mitoki hii pia huweza kushambuliwa na kansa ya karposi’s sarcoma au hata TB, lakini wakati mwingine inavimba tu bila sababu zilizo wazi.

Mitoki hii uweza kupona bila matibabu, lakini wakati mwingine matibabu yanatakiwa

Muhimu

Magojwa yote niliyotaja hapo juu yalikuwepo kabla ya Ukimwi isipokuwa yameongezeka baada ya Ukimwi kuingia, hivyo si kila mwenye magonjwa hayo ana Ukimwi. Kimsingi wagonjwa walio wengi wenye magonjwa hayo wana virusi vya Ukimwi.

Katika utumishi wangu, ukiondoa fangasi za mdomoni, wagonjwa wote niliowatibu na wakakubali kupima wote waligundulika wana Ukimwi. Lakini nasisitiza si lazima mwenye magonjwa hayo awe na Ukimwi.

Makala hii imeandikwa na Dr. Augustine Rukoma, daktari bingwa wa magonjwa ya kinywa na meno. Kwa makala zaidi, maswali na ushauri mtembelee kwenye blog yake ya http://rukomadentalanswers.blogspot.com

 

Imesomwa mara 42378 Imehaririwa Jumatatu, 14 Januari 2019 14:12
Dr. Augustine Rukoma

Dr Dr. Augustine Rukoma ni daktari na mtaalamu wa meno, anapenda kutumia muda wake wa ziada kuandika makala na kubadilishana mawazo juu ya afya ya kinywa na Meno.

rukomadentalanswers.blogspot.com | Anwani ya barua pepe hii inalindwa kutokana na spambots. JavaScript lazima iwe itawezeshwa kwa kuweza kuona.

Makala shabihana