Image

Tatizo la kukosa hedhi ni jambo ambalo linawakumba wanawake wengi waliovunja ungo.Aidha suala hili limekuwa likiwaletea usumbufu mwingi wa kisaikolojia wanawake wengi waliowahi kukumbana nalo.
Tatizo la kukosa hedhi au amenorrhea linaweza kutokea awali kabisa (primary) au baadaye kabisa maishani (secondary).

Primary amenorrhea

Hiii hali ya kukosa hedhi inayoweza kumtokea msichana aliye katika umri wa kuvunja ungo na ambayo huweza kuendana na hali ya kukosa mabadiliko ya kubalehe kama vile kuota matiti au nywele za kinena, au msichana anaweza kuwa na mabadiliko ya kubalehe lakini asipate hedhi.

Secondary amenorrhea

Hii hali ya kukosa hedhi inayomtokea mwanamke ambaye si mjamzito, hanyonyeshi, na ambaye hajavuka umri wa kukosa hedhi (menopause) na wala hatumii njia za uzazi wa mpango kama vile sindano au vidonge, na ambaye hapo awali alikuwa akipata hedhi kama kawaida lakini akasimama kwa miezi mitatu au zaidi.

Mwanamke hupataje hedhi?

Ili mwanamke aweze kuwa na mzunguko ulio sahihi wa hedhi, ni lazima matezi yake ya hypothalamus na pituitary pamoja na kiwanda cha kutengeneza mayai ya kike (ovaries) na mji wa mimba (uterus) vifanye kazi zake sawasawa.

Hypothalamus huchochea tezi la pituitary kuzalisha hormone chochezi ya follicle au follicle-stimulating hormone (FSH) pamoja na homoni ya luteinizing (LH). Hizi FSH na LH kwa pamoja huchochea ovaries kuzalisha homoni za estrogen pamoja na progesterone. Kazi za estrogen na progesterone ni kusababisha mabadiliko katika ukuta wa uterus yaani endometrium ikiwepo kupata hedhi. Ili damu ya hedhi iweze kutoka nje, njia ya uzazi ya mwanamke haina budi kuwa huru yaani isiyo na matatizo yeyote yale.

Makala hii ni muendelezo wa makala ya kwanza kuhusu Sababu na Dalili za Kuharibika kwa Mimba, katika sehemu ya kwanza ya Sababu na dalili za Kuharibika kwa Mimba - Sehemu ya Kwanza tuliangalia maana ya kuharibika kwa mimba na baadhi ya visababishi vyake sehemu ya kwanza. Katika makala hii tutaangalia kuharibika kwa mimba miezi mitatu ya mwisho ya kipindi cha ujauzito (Third trimester miscarriage).

Kuharibika kwa mimba kwa kipindi hiki sio sana kama kipindi cha miezi mitatu ya mwanzo.

Visababishi vya kuharibika kwa mimba ni;

  • Kukaa vibaya kwa kitovu cha mtoto au hata kuwepo kwa fundo (knot) kwenye kitovu cha mtoto
  • Kulegea na kulainika kwa shingo ya kizazi (Cervical Incompetence)
  • Matatizo ya viashiria vya asili ambavyo havikugundulika hapo awali (Chromosomal defects)
  • Bawasiri (Hemorrhages)
  • Kukosekana kwa uwiano wa vichocheo mwilini (hormonal imbalance)
  • Utapia mlo
  • Vipimo vya vina saba kama Amniocentesis or Chorionic Villus Sampling (CVS) ambavyo hufanyika wiki ya 16 ya ujauzito
  • Maambukizi kama ugonjwa wa mafua, surua na ugonjwa wa mishipa ya fahamu au neva
  • Uvimbe katika mfuko wa uzazi (fibroids)
  • Mimba kupitiliza umri wake zaidi ya wiki 41 za ujauzito (post maturity )
  • Matatizo ya maumbile ya mfuko wa uzazi (Uterine structural abnormalities/defects)
  • Matumizi ya madawa ya kulevya kama cocaine
  • Uvutaji sigara na unywaji pombe
  • Matatizo ya kondo la nyuma la uzazi -Abruptio placenta au Placenta Previa

Abruptio Placenta ni kuachia kwa kondo hili kutoka kwenye ukuta wa mfuko wa uzazi. Ikumbukwe ya kwamba kondo hili ndilo linalohusika kumpa mtoto chakula pamoja na hewa ya oksijeni wakati wa ujauzito.

Chanzo cha tatizo hili hakijulikani isipokuwa kinahusishwa na ugonjwa wa kisukari, presha (140/90mmHg au zaidi), uvutaji sigara, matumizi ya madawa ya kulevya kama cocaine, kuwepo kwa historia ya kupata tatizo hili hapo awali,maumivu kwa mama mjamzito kutokana na kupigwa, kuzaa watoto wengi haya yote huchangia uwezekano wa kupata tatizo hili.

Viashiria vyake ni pamoja na kutokwa damu kwenye tupu ya mwanamke na maumivu makali sana ya tumbo.

Baadhi ya vichagizi (risk factors) vya kuharibika kwa mimba kipindi hiki ni;

  • Kubeba mimba yenye watoto wengi (Multiple pregnancy)
  • Kushika mimba tena ndani ya muda mfupi baada ya kujifungua hapo awali
  • Hypothyroidism-Ugonjwa wa tezi koo
  • Kutopata choo (Constipation)
  • Kuharisha
  • Polycystic ovary syndrome 

Viashiria vya kuharibika kwa mimba kipindi hiki ni kama ifuatavyo;

  • Kutokwa damu sana kupitia tupu ya mwanamke (Heavy vaginal bleeding)
  • Kuona matone ya damu kutokwa na matone ya rangi kutoka kwenye tupu ya mwanamke
  • Maumivu makali na kuhisi maumivu yanavuta sehemu za tumbo (cramps)
  • Maumivu ya kiunoni
  • Kichefuchefu, kutapika na kuharisha
  • Maumivu kwenye bega
  • Kubana na kuvimbiwa tumbo

Sio siri duniani kuna baadhi ya nchi ambazo zimeruhusu mama mjamzito kufanya uamuzi wa kutoa mimba (abortion) bila kuwepo kwa sababu zozote za msingi za kitabibu. Baadhi ya nchi hizo ni Marekani, Canada, Visiwa vya Guyana, Bahrain (isizidi umri wa mimba wa wiki 12),Uturuki, China, Singapore, Ubelgiji, Uswisi, Uholanzi nk. Kwa bara la Afrika ni nchi mbili tu ambazo zimeruhusu mama mjamzito kufanya uamuzi huu ambazo ni Afrika Kusini na Tunisia. Katika nchi hizi mbili za kiafrika, mama mjamzito ataruhusiwa kutoa mimba (abortion) iwapo mimba itakuwa na umri wa chini ya wiki 12 za umri wa mimba.

Suala la utoaji mimba bado haliruhusiwi katika mataifa mengi duniani isipokuwa tu pale panapokuwa na sababu za msingi za kitabibu ambazo zinaruhusu mimba hiyo iharibiwe/itolewe (abortion) pasipo mhusika/mama mjamzito kukumbana na mkono mkali wa sheria. Jamhuri ya muungano wa Tanzania ikiwa ni moja za nchi hizo ambazo haziruhusu mama mjamzito kutoa mimba ila pale tu kuna  sababu za msingi za kitabibu zinazoruhusu mama mjamzito kufanya hivyo.

Kuharibu/kutoa mimba kutokana na sababu za kitabibu ambazo kama mama ataendelea kubeba  ujauzito huo  hadi kipindi cha kujifungua  basi atahatarisha maisha yake mwenyewe au maisha ya kiumbe alichobeba ndio hujulikana kitaalamu kama induced abortion.

Leo tutaangalia sababu zinazompa mama haki ya kutoa mimba bila kukumbana na mkono wa sheria.Sababu hizi zimegawanyika katika makundi mawili

  • Sababu kwa upande wa mama
  • Sababu kwa upande wa mtoto

Kwa upande wa mama sababu  hizi  ni kama zifuatazo

  • Magonjwa ya moyo kama ugonjwa wa presha, ugonjwa wa presha wa mishipa ya palmonari (Pulmonary hypertension), kuwepo kwa historia ya mama kupata ugonjwa wa moyo unaosababishwa na ujauzito (Pregancy induced cardiomyopathy) na Eisenmenger's syndrome.
  • Magonjwa ya jenetikali/asili kama marfan syndrome
  • Ugonjwa wa mfumo wa damu kama Thrombotic thrombocytopenic purpura
  • Magonjwa ya mfumo wa fahamu (Neurological disease)-Kutotibiwa kwa ugonjwa wa mfumo wa damu wa ubongo (Untreated cerebrovascular malformations) kama aneurysm au arteriovenous malformation
  • Ugonjwa wa figo-Kupungua kwa uwezo wa figo kufanya kazi mwanzoni kabisa mwa kipindi cha ujauzito
  • Saratani-Saratani ya shingo ya kizazi (Cervical cancer) au saratani yoyote ile ambapo tiba ya mama inahusu kutumia dawa za saratani (chemotherapy) au kupewa tiba ya mionzi ya saratani (radiotherapy)
  • Magonjwa ya mfumo wa umengenyaji chakula (Metabolic disease)-Proliferative diabetic retinopathy

Kipindi cha kunyonyesha ni kipindi kigumu sana kwa mama kwani huambatana na uchovu mwingi unaotokana na kuongezeka kwa majukumu ya kumhudumia mtoto mchanga ambayo huchangia kwa mama kutokuwa katika hali nzuri ya kufikiria kufanya tendo la ndoa

Baada ya kujifungua, wanawake wengi hawaoni tendo la ndoa kama ni muhimu sana kwao hata kufikia hatua ya  kutojali hisia za wenza wao. Mwanamke anapojifungua huwa na kidonda, mchubuko na hata kuchoka  kwenye sehemu za tupu  yake kama atakuwa amejifungua kwa njia ya kawaida.

Kwa aliyejufungua kwa njia ya upasuaji, mama huyu huwa na kidonda kinachotokana na upasuaji kwenye tumbo lake na kwenye mfuko wa kizazi.

Je ni muda gani sahihi kwa mama aliyejifungua kuanza tena kujamiana?

Kitaalamu mama aliyejifungua hushauriwa  kusubiri mpaka wiki sita (baada ya kuanza kliniki- postnatal clinic) ndio aweze tena kufanya tendo la ndoa.

Kuzaa huathiri vipi tendo la ndoa?

Kipindi cha kupona baada ya kujifungua hutegemea na njia ya kujifungua aliyotumia mama.

Kwa wale ambao wakati wa kujifungua waliongezewa njia kwa ajili ya kurahisisha kupita kwa mtoto (Episiotomy) au walichanika (Tear) na kushonwa, nyuzi hupotea baada ya siku 10 mwilini na wiki mbili za ziada mpaka michibuko na kidonda/vidonda kupona kabisa. Mama huyu anashauriwa  kufanya staili (wakati wa kujamiana) ambazo zitapunguza kuegemewa kwa sehemu ya mshono. Staili ambazo mama hulazimika kunyanyua miguu au kukunja miguu mpaka kwenye kitovu chake ni bora akaziepuka. Anatakiwa kuwa muangalifu sana wakati wa kujamiana pamoja na kufanya tendo la ndoa kwa taratibu (slow and gentle).

Kwa mama aliyejifungua kwa njia ya kawaida (Spontaneous Vaginal Delivery, SVD) pasipo kuongezewa njia au kuchanika, kupona kwake ni haraka na anaweza kuanza tena kufanya tendo la ndoa mara tu damu inayotoka (Lochia) kuacha, mara nyingi  damu hii kutoka huacha kabisa ndani ya wiki nne hadi wiki sita.

Mama aliyejifungua kwa njia ya upasuaji (Caesarean section) huwa na wasiwasi , hofu kutokana na kidonda cha upasuaji, hivyo ni vyema kwa mama huyu kusubiri mpaka nyuzi kutoka  kabla ya kufanya tendo la ndoa na pia azingatie kufanya kwa utaratibu (gentle).Staili zitakazoongeza kugandamizwa kwa eneo la mshono ni bora akaziepuka.

Je, kunyonyesha huathiri tendo la ndoa?

Baada ya mama kujifungua, kunakuwepo na mabadiliko ya viwango vya vichocheo  mwilini mwake ambavyo ni;

  • Kupungua kwa kiwango cha Oestrogen-Kupungua kwa homoni hii husababisha;
  1. Mama kupata kinga dhidi ya kushika tena ujauzito ndani ya muda mfupi kwa kumzuia kuingia katika hatua ya ovulation.
  2. Ukavu kwenye tupu ya mwanamke (Dryness of vagina) kwa baadhi ya wanawake
  • Kupungua kwa hamu ya tendo la ndoa na hata kukosa msisimko kwenye kisime (Low clitoris sensation).
  • Kupungua kwa kiwango cha kichocheo aina ya testerone pia husababisha kupungua kwa hamu ya tendo la ndoa.
  • Kuongezeka kwa kiwango cha homoni aina ya Prolactin (ambacho pia hupatikana kwenye maziwa ya mama) husababisha mama kujihisi hali ya kuridhika kimapenzi.

Zifuatazo ni sababu za mama kupoteza hamu ya tendo la ndoa baada ya kujifungua:

  • Uchovu—Kutokana na kuongezea kwa majukumu ya kumlea na kumhudumia mtoto
  • Mabadiliko ya muonekano wa mwili-Kina mama wengi baada ya kujifungua hupoteza hali ya kujiamini kutokana na mabadiliko ya mwili kama kuongezeka uzito, matiti kuwa makubwa na hata kubadilika muonekano wa matiti yao, kubadilika shepu nk. Na hivyo kuchangia kupoteza hamu ya tendo la ndoa
  • Wasiwasi au hofu kuwa tendo la ndoa linaweza kuleta maumivu baada ya kujifungua
  • Kuogopa kushika ujauzito tena mara tu baada ya kujifungua
  • Ukavu kwenye tupu ya mwanamke kutokana na kupungua kwa homoni aina ya oestrogen (hutokea kwa baadhi ya wanawake)
  • Hali ya kuridhika kimapenzi kutokana na homoni ya Prolactin
  • Kupungua kwa kichocheoa aina ya Testerone

Mambo ya kuzingatia  Kwa mama aliyejifungua kabla ya kufanya tendo la ndoa tena

  • Mama anahitaji kuzungumza na baba mtoto na kumueleza ukweli kuhusu hisia zake juu ya tendo la ndoa
  • Baba anashauriwa kuwa mvumilivu kama mama bado anapata maumivu wakati wa kufanya tendo la ndoa kwani hali hii ni ya muda tu
  • Kumsaidia na kumpa ushirikiano mama katika kulea na kumtunza mtoto ili apate muda wa kupumzika na hivyo kuongeza utayari wa mama katika kufanya tendo la ndoa
  • Kumpenda, kumjali na kumjengea mama uwezo wa kujiamini kutokana na mabadiliko ya mwili wake yaliyotokana na ujauzito (kuongezeka uzito, kubadilika muonekano  wa matiti, shepu nk)
  • Mama anashauriwa  kuweka mazingira mazuri ya kukutana  kimwili na baba mtoto kwani hata yeye bado anamuhitaji katika kipindi hiki.
  • Kuchagua muda mzuri usiokuwa na usumbufu wowote ule kutoka kwa mtoto (muda mzuri ni baada ya kumnyonyesha mtoto)
  • Mama anatakiwa kujikagua na kujichunguza kwenye tupu yake taratibu kwa kutumia vidole vyake ili aweze kufahamu kama anaweza kupata maumivu wakati wa kujamiana

Kama unaendelea kupata maumivu, au uke kuwa mkavu sana ni vyema kumuona daktari kwa ajili ya ushauri na matibabu.

Kipindi hiki cha wiki sita ni muhimu sana kwa mama kuwa karibu sana mwenza wake na kumpa ushirikiano mpaka wote watakapo kuwa tayari kwa tendo la ndoa.

Ni vyema kutumia njia za uzazi wa mpango hata kama unanyonyesha  kwani unaweza kushika mimba usiyoitarajia, mimba hizi nyingi  zimepatikana katika kipindi hiki.

Kama bado mnaona hampo tayari kwa tendo la ndoa, ni vyema kuendeleza mapenzi mubashara  kama kupigana busu, kutomasana, kukumbatiana,  kupapasana sehemu tofauti za mwili ili hisia za tendo la ndoa zirudi kama hapo awali.

Usikose makala ijayo ya faida za kunyonyesha mtoto katika tovuti yako unayoipenda ya afya ya TanzMED.

Endapo una swali linalohusiana na makala hii, usisite kuuliza kwenye jukwaa la maswali hapa

Dalili za ujauzito hutofautiana kati ya mwanamke mmoja  na mwanamke mwingine, ingawa kuchelewa au kukosa hedhi ni dalili moja muhimu sana ya ujauzito.

Ni muhimu kuzitambua na kuzifahamu dalili hizi kwa sababu zinaweza kusaidia kujua kama kweli umeshika ujauzito au la  pamoja na kuweza kutofautisha matatizo mengine yanayoshahabiana kwa dalili na  ujauzito.

Hebu sasa tuangalie dalili na ishara za ujauzito:

  • Kutokwa damu kidogo ukeni wakati kiumbe kikipandikizwa kwenye mfuko wa uzazi, ingawa siyo wanawake wote hupatwa na dalili hii
  • Kukosa hedhi, hii ni moja ya dalili kubwa ya ujauzito
  • Maumivu kwenye matiti na kuvimba matiti (huweza kutokea kati ya wiki ya 1 hadi ya 2)
  • Uchovu, wanawake wengi huhisi uchovu na  na hali ya kutopenda kufanya lolote.
  • Kupoteza ladha au kuhisi ladha ya chuma mdomoni
  • Kuongezeka kwa hisia ya harufu, kipindi cha ujauzito wanawake wengi huongezeka hisia ya harufu
  • Kichefuchefu na kutapika
  • Maumivu ya kichwa
  • Kizunguzungu
  • Kukojoa mara kwa mara (hasa kati ya wiki 6-8)
  • Kubadilika rangi kwa ngozi inayozunguka chuchu kuwa nyeusi
  • Kutamani baadhi ya vyakula na kuchukia vingine
  • Kupanuka kwa mfuko wa uzazi
  • Tumbo kujaa au kuvimbiwa
  • Kununa na kukasirika haraka
  • Kiungulia au kupata choo kigumu
  • Kolostramu kuanza kutoka kwenye matiti 
  • Kuongezeka uzito
  • Kuweza kupapasa mtoto (palpation of the baby)
  • Kulainika na kuvimba kwa shingo ya uzazi (Hegars sign) - kuanzia wiki ya 6
  • Shingo ya uzazi kubadilika rangi kuwa ya samawati kutokana na msongamano wa damu katika mishipa ya vena. Ishara hii hujulikana kama Chadwick's sign

Tatizo la mimba kutoka au kutolewa ni jambo ambalo limewakumba kina mama wengi walio katika umri wa kuzaa. Aidha mijadala kuhusu kuhalalishwa au kuendelea kuharamishwa kwa utoaji mimba ni jambo linalochukua nafasi ya mazungumzo ya kila siku katika maisha yetu. 

Kwa baadhi ya nchi, suala la utoaji mimba ni jambo lililohalallshwa kisheria ingawa kwa nchi kama Tanzania, suala hili halijahalalishwa isipokuwa tu pale panapokuwa na sababu za kitabibu zinazolazimisha kufanya hivyo.

Nini maana ya mimba kutoka (abortion)

Kwa mujibu wa Shirika la Afya Duniani (WHO), utokaji mimba (abortion) hutokea pale ambapo kiumbe (mimba) kilicho chini ya wiki 22 kinapotoka kwa sababu moja ama nyingine, au kinapotolewa kwa njia yeyote ile. Aidha shirika la Afya limekwenda mbali zaidi na kutoa maana nyingine ya utokaji mimba kuwa ni pale mtoto (kiumbe) anapozaliwa akiwa na uzito wa chini ya gram 500.

Aidha baadhi ya matabibu hupendelea kutumia neno ‘abortion‘ kumaanisha kitendo cha utoaji wa mimba kinachofanywa na mtu mwingine ama kwa njia sahihi au zisizo sahihi na ‘miscarriage‘ kumaanisha kitendo cha mimba kutoka yenyewe kwa sababu nyingine yeyote. Ukiacha tofauti hizi za jinsi ya kuharibika kwa mimba, abortion na miscarriage humanisha kitu kilekile cha mimba kutoka.

Aina za utokaji mimba (Classification of abortion)

Utokaji mimba umeanishwa katika aina zifuatazo

  1. Utokaji wa mimba wa hiyari yaani kitendo cha mimba kutoka yenyewe (spontaneous abortion)
  2. Mimba inayotishia kutoka ingawa bado haijatoka (threatened abortion)
  3. Utokaji wa mimba usioepukika (inevitable abortion)
  4. Utokaji wa mimba ulio kamili (complete abortion)
  5. Utokaji wa mimba usio kamili (incomplete abortion)
  6. Mimba iliyotoka bila kugundulika kuwa imetoka (missed abortion)
  7. Utokaji wa mimba unaojirudia rudia (recurrent abortion)
  8. Utoaji mimba kinyume cha sheria (illegal abortion)
  9. Utoaji mimba kwa sababu za kiafya (therapeutic abortion)

1. Utokaji mimba kwa hiari au kitendo cha mimba kutoka yenyewe (spontaneous abortion)

Hii ni hali inayotokea pale mimba inapoharibika na kutoka bila kuwepo kwa sababu yeyote iliyo dhahiri, kwa maana nyingine mimba uharibika na kujitokea bila kusababishwa na mtu wala kitu chochote. Utokaji mimba wa namna hii umegawanyika katika aina kuu nne ambazo ni

  • Mimba inayotishia kutoka ingawa bado haijatoka (threatened abortion)
  • Mimba isiyoepukika kutoka (Inevitable abortion)
  • Mimba inayotoka yote au kamili (complete abortion), na
  • Utokaji mimba usio kamili (Incomplete abortion)


i. Mimba inayotishia kutoka (threatened Abortion)

Tatizo hili hutokea mapema wakati wa ujauzito. Hali hii hujionesha kwa damu kutoka ukeni wakati njia ya shingo ya uzazi ikiwa bado imefunga. Mara nyingi mimba inayotishia kutoka haina tabia ya kuambatana na maumivu yeyote ya tumbo.

Daktari anapompima mgonjwa hukuta shingo ya kizazi ikiwa imefunga na hakuna dalili zozote za kiumbe kutoka ingawa mgonjwa hutokwa na damu sehemu za siri. Aidha mgonjwa huwa hana maumivu yeyote ya tumbo.

ii. Mimba isiyoepukika kutoka (inevitable abortion)

Hii ni hali inayotokea mapema wakati wa ujauzito pale damu inapotoka ukeni wakati njia ya shingo ya kizazi ikiwa imefunguka au kuwa wazi. Aidha, kwa kawaida, kiasi cha damu kinachotoka ni kingi na mgonjwa hujisikia maumivu makali sana ya tumbo.

Utokaji mimba usioepukika waweza kupelekea

  • Utokaji mimba ulio kamili (complete abortion), au
  • Utokaji mimba usio kamili (incomplete abortion).

iii. Utokaji mimba usio kamili (incomplete abortion)

Utokaji mimba usio kamili huambatana na utokaji damu kwa wingi sehemu za siri za mgonjwa, kufunguka kwa njia ya shingo ya kizazi, kutoka kwa baadhi ya mabaki ya kiumbe (products of conception) ingawa mengine hubakia, na mgonjwa kujisikia maumivu makali ya tumbo hususani sehemu za chini ya kitovu.

iv. Utokaji wa mimba ulio kamili (complete abortion)

Hali hii huambatana na mama kutokwa damu sehemu za siri, kujisikia maumivu makali ya tumbo pamoja na kutoka kwa kiumbe ikiambatana na kondo lake la nyuma. Aidha baada ya muda, mgonjwa hueleza kupotea kwa maumivu ya tumbo, damu kupungua kutoka sehemu za siri na kufunga kwa njia ya njia ya shingo ya kizazi (cervix).

v. Mimba iliyotoka bila kugundulika kuwa imetoka (missed abortion)

Hali hii hutokea pale ambapo, kiumbe kinapokuwa kimekufa bila ya mimba kutoka. Mara nyingi, damu huwa haitoki sehemu za siri, na mgonjwa huwa hajisikii maumivu yeyote ya tumbo. Aidha huwa hakuna dalili zozote za ukuaji wa mimba na hata mapigo ya moyo ya mtoto hayawezi kutambulika hata kama vipimo maalum vitatumika.

vi. Utokaji wa mimba unaojirudia rudia (recurrent abortion)

Hali hii hutokea pale ambapo mama huwa na historia ya mimba kutoka mara tatu au zaidi kwa mfululizo.

vii. Utoaji mimba kinyume cha sheria (illegal abortion)

Utoaji mimba kinyume cha sheria ni usitishwaji wa maisha ya mimba au kutolewa kwa kiumbe kinyume na sheria za nchi husika zinavyoagiza. Katika mazingira kama haya, sababu dhahiri za kitaalamu hukosekana isipokuwa wahusika hutenda kulingana na sababu zao binafsi zikiwemo za kutoitaka mimba au kama ni muhusika ni mwanafunzi huogopa kufukuzwa shule.

viii. Utoaji mimba kisheria kwa sababu za kitabibu (therapeutic abortion)

Utoaji mimba ulioidhinishwa kitabibu ni usitishwaji wa mimba kwa ajili ya kuokoa maisha ya mama. Usitishwaji huu ni hufanywa kitaalamu na daktari. Sababu zinazoweza kufanya mimba ikasitishwa ni pamoja na

  • iwapo kiumbe kina mapungufu mengi ya kimaumbile (fetal anomally) ambayo yatamletea mtoto atakayezaliwa matatizo na hata kusababisha kifo chake
  • iwapo mama mjamzito alipata ujauzito kwa kubakwa na asingependa kuzaa, au
  • iwapo mama mjamzito ana kansa , kwa mfano, kansa ya kiwanda cha mayai ya kike (ovarian cancer), kansa ya damu (leukemia) au kansa ya tezi la goita (thyroid cancer)

Mambo gani hufanya mimba kutoka kwa hiyari?

Kuna sababu kadhaa zinazoweza kupelekea mimba kutoka kwa hiyari (spontaneous abortion). Miongoni mwa sababu hizo ni

  • Matatizo kwenye mfumo wa jenetiki (genetic abnormalities) ambayo husababisha kuharibika na kutoka kwa mimba katika miezi mitatu ya mwanzoni.
  • Matatizo kwenye mfuko wa uzazi (uterine problems): matatizo kama vile kuwepo kwa uvimbe kwenye mfuko wa uzazi wa mwanamke (uterine fibroids), au kulegea kwa milango ya shingo ya kizazi (cervical incompetence) husababisha mimba kutoka katika theluthi ya pili ya ujauzito (second trimester).
  • Sababu nyingine ni pamoja na maradhi wakati wa ujauzito kama malaria, kisukari, shinikizo la damu, kifafa cha mimba, matatizo kwenye tezi ya ‘goita’ (hypothyroidism). Aidha maambukizi kama Rubella, toxoplasmosis na mengineyo nayo pia huweza kusababisha mimba kutoka.
  • Kukosekana kwa ulinganifu katika baadhi ya homoni mwilini (hormonal imbalance)
  • Matumizi ya baadhi madawa kwa mfano zinazotumika katika kutibu msongo wa mawazo kama vile paroxetine au venlafaxine nayo yaweza kusababisha utokaji wa mimba.

Tabia hatarishi zinazoweza kusababisha utokaji wa mimba

  • Unywaji pombe uliopitiliza.
  • Uvutaji sigara
  • Utumiaji madawa ya kulevya kama vile kokeini (cocaine)
  • Utumiaji kwa wingi wa vinywaji vyenye kiasili cha caffeine kama vile kahawa au kakao.

Vipimo na Uchunguzi

Ili kutambua kuwepo kwa hali hii ya mimba kutoka, vipimo vifuatavyo vyaweza kufanywa na tabibu

  • Kipimo cha mimba kwa kutumia mkojo (Urine for hCG)
  • Kupima damu ili kufahamu kiasi cha wingi wa damu (haemoglobin level), kundi la damu (blood group) na muda wa damu kuganda (bleeding and clotting time).
  • Kuchunguza iwapo shingo ya uzazi imefunga au ipo wazi, na pia kuchunguza iwapo kuna dalili ya kiumbe kutoka ama la. Uchunguzi huu huitwa speculum examination.
  • Ultrasound ya nyonga (pelvic utrasound) kwa ajili ya kutambua iwapo kiumbe kipo ama la, na kama kipo je ki hai ama kimekufa.
  • Aidha ni muhimu pia kufanya uchunguzi wa magonjwa mbali ya zinaa ambayo husababisha mimba kutoka.

Matibabu ya utokaji wa mimba

Matibabu ya utokaji wa mimba hutegea sana aina ya utokaji wa mimba. Hata hivyo, ni muhimu kuzingatia vitu vifuatavyo wakati wa kutoa matibabu kwa mtu aliyepoteza mimba
Wahudumu wa afya huzingatia kanuni zote (ABC) za kuokoa maisha ya mgonjwa kama vile

  • kuhakikisha njia ya hewa ya mgonjwa ipo wazi na hewa inaingia na kutoka vizuri kwenye mapafu
  • kuhakikisha mgonjwa anapumua vizuri bila shida
  • kuhakikisha mishipa ya damu ya mgonjwa imewekwa mrija wa veni (intravenous line) na mgonjwa anapewa dripu ya maji ya normal saline.
  • kuhakikisha mgonjwa anaongezwa damu haraka iwapo vipimo vitaonesha kuwa alipoteza damu kwa wingi

Matibabu ya mimba inayotishia kutoka (threatened abortion)

Kwenye hali hii, mgonjwa hutakiwa

  • kupumzika kitandani bila kufanya kazi yeyote (complete bed rest) angalau kwa wiki moja au zaidi mpaka hapo damu itakapoacha kabisa kutoka
  • kumpa ushauri na uhakika mama ili kumfanya atulie kiakili (assurance and proper councelling)
  • Mama pia hupewa dawa za kumtuliza na kumfanya apumzike (sedatives) kama vile phernobabitone
  • Aidha mama hupewa dawa kwa ajili ya kupunguza kusukuma kwa uterus (antispamodics) kama vile salbutamol
  • Kutofanya tendo la ndoa kwa wiki mbili au tatu
  • Aidha mama na mumewe hupewa ushauri juu ya tatizo hilo na jinsi ya kuendelea na matibabu

Matibabu ya mimba iliyotoka kamili (complete abortion)

Mara nyingi mgonjwa huwa haitaji matibabu zaidi ya uangalizi wa karibu kwa vile kiumbe pamoja na kondo lake la nyuma vyote huwa vimetoka kikamilifu. Mara chache sana, kulingana na jinsi daktari atakavyoona, mgonjwa anaweza kupewa antibiotiki kwa ajili ya kuzuia uwezekano wa kupata maambukizi.

Matibabu ya utokaji wa mimba usiokuwa kamili (incomplete abortion)

Matibabu ya aina hii ya utokaji wa mimba uhitaji mgonjwa kusafishwa kwa ajili ya kuondoa mabaki ya kiumbe (products of conception) yaliyobakia. Usafishaji huu huweza kufanywa kwa kutumia njia inayoitwa Manual Vacuum Aspiration (MVA).

Aidha mgonjwa hupewa dawa za antibiotiki kwa ajili ya kuzuia uwezekano wa maambukizi ya vimelea vya bakteria.

Matibabu mimba iliyotoka bila kugundulika kuwa imetoka (missed abortion)

Matibabu ya aina hii ya utokaji wa mimba ni pamoja na mgonjwa kuwekewa maji ya uchungu ili kiumbe kiweze kutoka. Wakati mwingine, daktari anaweza kuamua kusafisha mfuko wa uzazi (uterus) kwa kutumia njia inayoitwa dilatation and curettage. Sambamba na matibabu hayo, mgonjwa pia hupewa dawa za antibiotiki kwa ajili ya kuzuia maambukizi ya vimelea vya bakteria.

Matibabu ya tatizo la utokaji wa mimba unaojirudia (recurrent abortion)

Jambo la msingi katika matibabu ya tatizo la utokaji mimba unaojirudia (recurrent abortion) ni kugundua na kutambua chanzo kinachosababisha tatizo hilo na kisha kukishughulikia ili kuondoa kabisa kujirudia rudia kwa tatizo hili.

Ukurasa 3 ya 3