Katika siku za karibuni, kumekuwa na changamoto kubwa kwa wanawake walio katika umri wa uzazi kutokupata hedhi (Amenorrhea) au kupata hedhi nje ya mpangilio maalumu. Hali hii siyo tuu hupelekea mawazo kwa baadhi ya wanawake bali pia husababishwa kushindwa kupangilia uzazi wa mpango kwa njia ya kufuatilia tarehe. Hivyo, katika makala hii itaangazia aina, sababu, dalili na njia ya matibabu.
Aina za kukosa hedhi
- Primary (ya awali): Hali hii hutokea ambapo binti ambaye ameshapevuka lakini bado hajaanza kupata hedhi.
- Secondary: Hali hiihutokea kwa wanawake ambao wameshapevuka na wameshaanza kupata hedhi ila kuna wakati hawapati hedhi, hali hii huweza kuwatokea hata miezi mitatu au zaid.
Amenorrhea ya awali (Primary Amenorrhea)
Hali hii hutokea wakati msichana hajawahi kupata hedhi kufikia umri wa miaka 15. Sababu zake zinaweza kua:
Matatizo ya Kijenetiki:
- Ugonjwa wa Turner (Turner syndrome): Hii ni hali ya kijenetiki inayowaathiri wanawake na hutokea wakati kromosomu moja ya X inakosekana au haipo kabisa. Hali hii siyo ya kurithi ila hutokea baada ya makosa kwenye ugawanyikaji wa seli wakati wa hatua za awali kabisa za ujauzito. Hali hii husababisha mfuko wa mayai (ovari) kushindwa kufanya kazi hivyo mwili unakosa sababu ya kutenegeneza ukuta wa damu ambao huja kuvunjika kama kusipokuwa na uchavushaji.
- Matatizo ya tezi ya adrenal: Tezi hizi hutumika kutengeneza Homoni mbalimbali ambazo moja ya kazi zake ni kuchunga mzunguko wa hedhi wa mwanamke. Matatizo ya tezi hizi huathiri uzalishaji wa homoni.
Matatizo ya maumbile:
- Kutokuwepo kwa mji wa mimba au uke.
- Imperforate hymen: Bikra iliofunika kabisa au ambayo haina uwazi, hivyo kuzuia damu ya hedhi kutoka.
Matatizo ya Homoni:
- Matatizo ya tezi ya pituitary au hypothalamus katika ubongo.
- Kushamiri kwa homoni za kiume
Amenorrhea ya Sekondari (Secondary Amenorrhea)
Hali hii hutokea wakati mwanamke ambaye alikuwa anapata hedhi kawaida kuacha kupata hedhi kwa miezi mitatu au zaidi. Sababu zake zinaweza kua:
- Ujauzito: Hii ni sababu kubwa ya kawaida inayoweza kusababisha mwanmke asione hedhi.
- Kunyonyesha Mtoto: Wakati wa kunyonyesha, mwili hutengeneza Homoni za Lactation ambazo huzuia hedhi.
- Kukoma kwa Hedhi (Menopause): wanaweke waliofika umri wa kukata kuona hedhi (miaka 45 –60), Ovari huacha kuzalisha Homoni haswa ya Estrogen ambayo husika na mzunguko wa hedhi.
- Matatizo ya Homoni: Ugonjwa wa Polycystic Ovary Syndrome (PCOS). Matatizo ya tezi ya thyroid (hypothyroidism, hyperthyroidism). Matatizo ya tezi ya pituitary kama vile uvimbe kwenye ubongo unaoathiri eneo la pituitary au hypothalamus.
- Matatizo ya Uzito: Uzito mdogo sana (kama watu wenye anorexia nervosa au utapia mlo). Uzito mkubwa sana (unene kupita kiasi).
- Mazoezi Makali: Mazoezi makali sana yanaweza kuathiri homoni. Na kupelekea kukata kwa hedhi.
- Msongo wa Mawazo (Stress): Msongo wa mawazo unaweza kuathiri homoni.
- Matumizi ya Dawa: Baadhi ya dawa zinaweza kusababisha kukata kwa (kama vile dawa za kupunguza msongo wa mawazo, dawa za shinikizo la damu, na dawa za saratani).
- Magonjwa Mengine: Uvimbe kwenye tezi ya Pituitary au Ovari. Asherman's Syndrome (makovu kwenye mji wa mimba). Magonjwa ya mfumo wa Endocrine kama ugonjwa wa Cushing, na kisukari ambacho Magonjwa ya mfumo wa chakula kama ugonjwa wa Celiac. Magonjwa ya mfumo wa kinga kama ugonjwa wa Addison.
Dalili zinazoweza kuambatana na kukata kwa hedhi ni:
- Mwili kupata wakati ambapo joto linapanda na kua kali.
- Chuchu kutoa/kuvuja maziwa.
- Uke kavu.
- Maumivu ya kichwa.
- Matatizo ya macho.
- Chunusi
- Ukuaji wa nywele nyingi kwenye uso(ndevu) na mwili wako.n.k
Umuhimu wa Uchunguzi
- Kama unakumbana na tatizo la kutokuona hedhi au kukata kwa hedhi, ni muhimu kuonana na daktari kwa uchunguzi kamili.
- Daktari atafanya vipimo vya damu ili kuangalia viwango vya homoni, ikiwa ni pamoja na homoni za tezi ya thyroid, pamoja na uchunguzi wa kimwili na labda ultrasound ili kuangalia matatizo yoyote ya anatomia.
Matibabu
Matibabu ya amenorrhea yatategemea sababu inayoisababisha;
- Matatizo ya tezi ya thyroid yanaweza kutibiwa na dawa za homoni.
- PCOS inaweza kutibiwa na dawa za kudhibiti homoni, kama vile vidonge vya uzazi wa mpango.
- Matatizo ya anatomia yanaweza kuhitaji upasuaji.
Ni muhimu kupata matibabu sahihi ili kuzuia matatizo zaidi, kama vile utasa na kudhoofika kwa mifupa.
Katika miaka ya hivi karibuni, kama wewe ni daktari, mfanyakazi wa kada ya afya,binti au kijana hasa wa miaka 15-24 ni dhahirikabisa jina la P2 si ngeni masikioni mwako. Dawa hii imejizoelea umaarufu mkubwa miongoni mwa mabinti hasa wa umri tajwa kama ni njia kuu ya kuzuia kupata ujauzito. Ingawa dawa hii inaweza kuwa na manufaa yaliyokusudiwa, lakini matumizi yasiyo sahihi huweza kuleta madhara makubwa ukizingatia wengi wanaotumia hawana uelewa mpana juu yake.
Kwa uzoefu niliopata nikiwa kazini mabinti wengi wanaotumia dawa hii ni wale ambao bado hawapo kwenye ndoa lakini wamekuwa wanashiriki tendo na wenza wao, pia, wapo wanawake wachache ambao wapo kwenye ndoa lakini wanatumia P2 kama ni sehemu ya uzazi wa mpango.
Ukweli ni kuwa, mabinti wengi wanaotumia dawa hii ya P2 hujikuta wakitumia kwa sababu;
- Hupatikana kwa urahisi katika maduka mengi ya dawa baridi, na huuzwa bila ya maswali mengi ya ‘kwanini kwanini’-unalipa- unapewa dawa-unaondoka.
- Kutokana na kuona aibu ya kuonekana wanashiriki tendo kabla ya ndoa, mabinti wengi wanaogopa kuhudhuria vituo vya afya kupata ushauri wa uzazi salama na uzazi wa mpango, wengi wao huwa na hofu ya kunyanyapaliwa au kukutana na ndugu wanaowafahamu hivyo kuzua taharuki kwenye familia- kuwa sasa binti huyu ameanza kujihusisha na mapenzi- kumbuka kuwa watumiaji wengi ni kuanzia miaka 15 mpaka 24 (inawezekana ikawa chini au zaidi ya umri huo pia) wengi wao bado hawapo kwenye ndoa.
P2 ni nini:
P2 ni kifupi cha dawa (Postinor-2) hii ni dawa/kidonge kilicho na vichocheo vya homoni kwa ajili ya kuzuia mimba zisizotarajiwa (emergency contraceptive pills) au wengine huita (morning after pills).
Hii ni kati ya dawa nyingi za namna hii ambazo huzuia mwanamke asipate ujauzito inapotokea amefanya mapenzi wakati wa siku za hatari (fertile days) bila kutumia kinga au alitumia kinga (kondomu) ambayo labda ilipasuka (kuachana mkeka) wakati wa tendo na akawa na hofu ya kupata ujauzito.
Dawa hii hushauriwa kutumika si zaidi ya masaa 72 toka mwanamke aliposhiriki tendo la ndoa. Pakiti moja huwa na vidonge viwili ambapo kimoja kinatakiwa kunywa mara tu na kingine hutumia masaa 12 baada ya kunywa kidonge cha kwanza. Ifahamike kuwa vichocheo vya homini katika dawa hizi ni vya kiwango cha juu sana kulinganisha na vidonge vingine vya homini vya kuzuia mimba vya muda mrefu.
Je P2 hufanyaje kazi:
Vidonge hivi hufanya kazi kwa namna kadhaa:
- Hatua ya kwanza kabisa ni kufanya yai lichelewe kupevuka hivyo kuchelewesha uwezekano wa haraka wa kukutana na mbegu na kurutubishwa.
- Pili hufanya ute ute wa ukeni kuwa mzito hivyo huzifanya mbegu za mwanamume (sperms) kushindwa kuogelea kwa haraka kulifuata yai kwa ajili ya kulipevusha. Unaweza kusoma makala ya jinsi gani yai linavyochavushwa hapa.
- Pia, Homoni zilizotolewa na dawa hii ya P2, huufanya mji wa mimba kutokuwa tayari kwa ajili ya kupokea yai lililorutubishwa hivyo huondoa uwezekano wa yao lililochavushwa kwenda kujishikiza tayari kwa ajili ya ukuaji.
Hivyo basi, dawa hii haiwezi kutumika kama dawa ya kutoa ujauzito (abortion) kwa mtu ambaye tayari ni mjamzito.
Faida
Ikitumiaka kwa namna sahihi inaweza kusaidia kuzuia ujauzito usiotarajiwa.
Madhara:
- Dawa hii inavichocheo vya homoni vya kiwango cha juu hivo havimpasi mtu kutumia mara kwa mara lasivyo inaweza leta madhara ya kuharibu utaratibu wa kifisiolojia wa upevukaji wa mayai kwani mara nyingi mwili wa binadamu hubadilika badilika kulingana mazingira, madhara ya mabadiliko haya ya kifisiolojia ni kama:
- Kuchelewa kupata ujauzito kutokana na mayai kutopevuka kwa wakati
- Kupata hedhi isiyotabirika
- Kupata hedhi nyingi kuliko kawaida
- Kutokupata hedhi kabisa
- Mimba kutunga nje ya kizani (ectopic pregnancy)
Mimba hutunga nje ya uzazi endapo mimba imetungwa nje ya mji wa mimba (uterus), mara nyingi hutokea kwenye mirija ya folopian ambapo uchavushwaji hutokea na yai lililochavushwa likashindwa kusafiri kwenda mji wa Mimba. Hii huchangiwa na mabadiliko ya Homoni ambapo P2 hufanya lakini ni nadra sana kutokea kwa sababu ya P2.
- Kuleta shida zaidi au dawa kutofanya kazi kwa usahihi kama utakuwa na magonjwa kama homa ya ini, moyo,figo,sukari au saratani-unatoka damu bila mpangilio-au kama unatumia dawa za muda mrefu kama vile dawa za kufubisha virusi vya ukimwi au dawa za kifaa hivyo ni salama zaidi kujua afya yako kwa ujumla au kuzungumza na mtaalam wa afya kabla ya kumeza/kutumia vidonge hivi.
Maudhi mengine yanaweza kutokea ni pamoja na kichefuchefu, kizunguzungu nk.
Mambo ya msingi ya kuzingatia:
P2 inatumika kuzuia mimba kwa dharura, hivyo haupaswi kuitumia kama njia ya kudumu au kunywa mara kwa mara kwa ajili ya kuzuia mimba- tafadhali kama unafanya hivyo basi tembelea kituo cha afya cha karibu kwa ushauri zaidi.
Hata kama umetumia P2, bad kuna uwezekano wa kupata ujauzito, hivyo kama umetumia P2 na ukakosa hedhi hedhi basi ni vizuri ukapima ujauzito. Watu wengi wanaotumia P2 na bado wakapata ujauzito huamua kufanya utoaji wa mimba kwa njia wanazozijua wao ambazo ni hatari zaidi. Unapogundua hali hiyo ni vyema kutembelea kituo cha afya kwa ushauri zaidi.
Lakini pia wanawake wengi wanasahau kuwa dawa hizi hazizuii magongwa ya zinaa kama vile HIV, Kisonono, Kaswende- hivyo kuwafanya waangalie upande mmoja wa afya yao na kuacha upande mwingine ambao pia ni hatari zaidi kwa faya yao ya uzazi kwa ujumla- kwa sababu magonjwa haya yasipotibika yanaweza kuleta athari kubwa kwenye via vya uzazi na kuleta madhara ya kutopata ujauzito ambao kwa sasa wanaukimbia.
Hivyo wazazi na walezi ni vizuri kuchukua hatua za makusudi kutenga muda wa kuongea na vijana wetu`kuhusu afya ya uzazi,kuwasikiliza, kutambua na kufuatilia mienendo yao kwa karibu.
Lakini pia serikali kwa kushirikiana na wahudumu wa afya pamoja na wizara ya elimu kuweka mazingira sahihi ili kuwasaidia vijana kuweza kupata elimu Rafiki ya afya ya uzazi pia uwoga au kunyanyapaliwa- wanapokuwa na uelewa sahihi inawasaidia kufanya maamuzi sahihi ambapo ni pamoja kujizuia kufanya tendo la ndoa kabla ya wakati au kijihusisha na mahusiano yanayoweza kuhatarisha afya yao kwa ujumla.
Safari ya kila mtoto kuzaliwa ni ya kipekee sana, lakini safari zote huanzia kwenye muungano wa yai la mwanamke (ovum) na mbegu ya kiume (sperm). Mchakato huu unaendelea kwa miezi tisa ndani ya mwili wa mwanamke, na hatimaye kuzaliwa kwa mtoto. Katika makala hii, tutafuatilia kwa karibu hatua zote muhimu katika safari ya kupevushwa yai na mpaka kuzaliwa kwa mtoto.
Upevukaji wa Yai
Kwa kawaida, mtoto wa kike huzaliwa akiwa na mayai yanayokadiriwa milioni 1 hadi 2. Kwa wakati huu wa utotoni, mayai haya huwa yamesinzia (dormant) hadi kufika kipindi cha kubalehe (kuvunja ungo). Baada ya kubalehe, na endapo hakuna changamoto yoyote katika mfumo wa uzazi, basi kila mwezi mwili wa mwanamke huruhusu mayai kadhaa kepevuka ndani ya mfuko wa mayai (Ovary).
Kwa mazingira ya kawaida (isipokuwa mapacha wasiofanana) yai moja tu lililo bora zaidi kati ya mengi yaliyopevuka ndiyo huruhusiwa kutoka (Ovulation) na yale mengine yaliyopevuka na hayaruhusiwa kutoka huliwa na mwili. Yai hili lililotolewa linapotoka kwenye mfuko wa mayai hupita kwenye mirija ya fallopian na kisha kufika katika mji wa mimba (uterus) tayari kwa ajili ya uchavushwaji (fertilization), yai hili lina uhai wa masaa kati ya 12 hadi 24, na ndio wakati mzuri kwa mbegu ya kiume kuungana nalo ili kutunga ujauzito.
Uchavushaji:
Wakati wa tendo la ndoa, mamilioni ya mbegu za kiume(sperm) huingia kwenye uke wa mwanamke na mbegu hizi huogelea kwa msaada wa kimiminika kilichopo kwenye manii kupitia kizazi hadi kwenye mirija ya fallopian katika kutafuta yai. Kati ya mbegu nyingi zilizofanikiwa kufika kwenye yai, ni mbegu moja tu yenye ubora zaidi ndiyo itafanikiwa kuingia kwenye yai la kike na hapa ndipo uchavushaji (Fertilization) inakuwa imekamilika.
Baada ya mbegu moja kuingia, yai hujifunga na kutoruhusu tena mbegu za kiume kuingia kwenye yai kwa ajili ya uchavushaji. Mchanganyiko huu wa yai na mbegu huunda seli moja inayoitwa zygote. Seli hii ndio mwanzo wa maisha mapya na ina mchanganyiko wa DNA kutoka kwa wazazi wote wawili. Kisayansi, mtoto huchukua 50% ya DNA kutoka kwa kila mzazi. Nusu kutoka kwa baba na nusu kutoka kwa mama.
Ndani ya DNA kuna vitu vinaitwa chromosomes, na kila binadamu ana chromosomes 46 tu, 23 kutoka kwa baba na 23 kutoka kwa mama.Kati ya hizi chromosomes 23, 22 zinafanana kabisa lakini chromosomes ya 23 huitwa Sex chromosome na ndio itakayo amua jinsia ya mtoto.
Endapo kwa sababu zozote zile, hakutokuwa na yai lililochavunshwa, basi ukuta ulioundwa ndani ya uterus kwa ajili ya mapokeo ya zygote huvunjika na ndiyo sababu kila mwezi mwanamke ambaye bado hajakoma siku hupata hedhi.
Upachikanaji:
Zygote huanza kugawanyika na kuunda seli nyingi zaidi huku ikitafuta mahali pakujipachika katika mji wa mimba. Kujipandikiza huku hutokea ndani ya siku 6 hadi 12 baada ya fertilization. Baada ya hatua hii kumalizika kikamilifu Kondo (placenta) huundwa na ndiyo tunaweza kusema kuwa mwanamke ana ujauzito. Mwili wa mwanamke huanza kutengeneza hormone ya HCG (Human Chorionic Gonadotropin) ambayo itaanza kuleta dalili za mimba.
Ukuaji wa Mtoto
Baada ya kujipachika, seli zile huanza kugawanyika na kujipanga ili kuunda viungo vya mtoto.
Katika wiki za mwanzo, mtoto anaitwa embryo. Baada ya wiki ya nane, mtoto anaitwa fetus.Fetus huendelea kukua na kutengeneza viungo vyote vya muhimu. Ujauzito umeganyika katika vipindi vitatu tangu fertilization hadi kujifungua. Vipindi hivi huitwa trimesters.
Trimester ya Kwanza (Wiki 1-12):
- Wiki 1-2: Fertilization hufanyika, na zygote huanza kugawanyika na kufanya implantation.
- Wiki 3-8: Mtoto anaitwa embryo na viungo vyote muhimu huanza kuundwa. Moyo huanza kudunda, ubongo na mfumo wa fahamu huanza kuundwa. Wakati huu ni muhimu sana mama apate madini ya folic acid ili kuhakikisha mifumo hii inaundwa kwa usahihi.
- Wiki 9-12: Mtoto anaitwa fetus sasa. Viungo vyote muhimu vimeundwa, na mtoto anaanza kufanya harakati ndogo ndogo huku viungo vikiendelea kukomaa na kuimarika.
Trimester ya Pili (Wiki 13-27):
- Wiki 13-16: Mtoto anakua kwa kasi, na mama anaweza kuanza kuhisi mtoto akisogea au kucheza tumboni.
- Wiki 17-20: Ngozi ya mtoto inakuwa laini, na nywele za kichwa zinaanza kukua. Wakaiti huu kipimo cha ultrasound kinaweza kuonyesha jinsia ya mtoto.
- Wiki 21-24: Mapafu ya mtoto yanaanza kukomaa, lakini bado hayajakamilika na mtoto akizaliwa wakati huu, hataweza kupumua mwenyewe.
Trimester ya Tatu (Wiki 28-40):
- Wiki 28-32: Mtoto anaendelea kukua na kuongezeka uzito. Mafuta huanza kujilimbikiza chini ya ngozi, lakini bado hayupo tayari kwa maisha nje ya mji wa wimba.
- Wiki 33-37: Viungo vyote vya mtoto vimemaliza kukua. Mpaka wiki ya 34 kukamilika, mapafu nayo yanakua tayari yamekomaa na mtoto anaweza kuzaliwa wakati wowote baada ya hapo na akawa na uwezo mkubwa wa kuendelea kuishi nje ya tumbo la mama.
- Wiki 38-40: Mtoto anazingatiwa kuwa amekomaa kikamilifu na anaweza kuzaliwa wakati wowote. Mtoto akizidi kukaa tumboni zaidi ya hapo ni hatari, na uchungu usipoanza wenyewe, harakati za kuanzisha uchungu zinaweza kuanzishwa ili mama na mtoto wote waweze kuwa salama.
Kuzaliwa:
Baada ya miezi tisa, mtoto atakuwa tayari kuzaliwa. Mchakato wa kuzaliwa huanza na uchungu (contractions), ambao husaidia kufungua njia ya kizazi. Njia inapofika sentimita 10 mama huanza kusukuma na mtoto hutolewa. Kuna sababu kadhaa zinazoweza kuzuia mama kujifungua kwa njia hii na kuhitaji njia mbadala ambayo ni ya upasuaji (Cesarean section). Baada ya mtoto kutoka, kitovu (umbilical cord) hukatwa na kisha kondo kutolewa.
Hitimisho
Uzazi ni safari ya kipekee yenye kustaajabisha, Kutoka kwa mchanganyiko wa yai na mbegu hadi kuzaliwa kwa mtoto mpya, kila hatua ni muhimu katika kuunda maisha mapya. Kwa kuelewa mchakato huu, tunaweza kufahamu zaidi umuhimu wa afya ya uzazi na kuunga mkono wanawake wajawazito katika safari hii ya ujasiri.
Unaweza kutumia TanzMED App kwa ajili ya kufuatilia ujauzito au kupanga ujauzito wako.
Wasiwasi kwa watoto ni jambo la kawaida na linaweza kujidhihirisha kwa njia nyingi tofauti. Ingawa hofu na wasiwasi ni sehemu ya ukuaji wa mtoto, wakati mwingine inaweza kuwa kali na kuathiri maisha yao ya kila siku. Katika makala hii, tutajadili kwa undani zaidi kuhusu wasiwasi kwa watoto, sababu zake, dalili, na njia za kukabiliana nayo.
Sababu za Wasiwasi kwa Watoto
Sababu za wasiwasi kwa watoto ni nyingi na zinaweza kuwa za kibinafsi, za mazingira, au mchanganyiko wa zote mbili. Baadhi ya sababu zinazosababisha wasiwasi kwa watoto ni pamoja na:
- Kukabiliana Matukio hasi : Matukio kama vile kushuhudia vurugu, kutengana na wazazi, au kubadilisha shule yanaweza kusababisha wasiwasi kwa watoto.
- Kurithi : Watoto ambao wana wazazi au ndugu walio na matatizo ya wasiwasi wana uwezekano mkubwa wa kupata matatizo haya pia.
- Unyanyasaji au Kudhalilishwa: Watoto wanaofanyiwa unyanyasaji wa kimwili, kihisia, au kingono wana uwezekano mkubwa wa kupata wasiwasi na matatizo mengine ya afya ya akili.
- Matatizo ya Kimwili: Matatizo ya kiafya sugu kama vile mzio (allergy) , pumu, au maumivu ya muda mrefu yanaweza kuchangia katika wasiwasi.
Dalili za Wasiwasi kwa Watoto
Dalili za wasiwasi kwa watoto zinaweza kutofautiana kulingana na umri na aina ya wasiwasi. Baadhi ya dalili za kawaida ni pamoja na:
- Dalili za Kimwili: Maumivu ya tumbo, kichwa, au misuli; matatizo ya kulala; na mabadiliko ya hamu ya kula
- Dalili za Kihisia: Kutokuwa na utulivu, kukasirika kwa urahisi, kulia mara kwa mara, na kujisikia kuwa na hofu kila wakati.
- Dalili za Tabia: Kuepuka shule au shughuli za kijamii, kuzingatia sana mambo mabaya, na kuwa na shida kuzingatia.
Aina za Wasiwasi kwa Watoto
Kuna aina nyingi za wasiwasi kwa watoto, lakini baadhi ya aina za kawaida ni pamoja na:
- Wasiwasi wa Kutengana (separation anxiety disorder): Hofu ya kutengana na wazazi au walezi.
- Phobia Mbali mbali: Hofu kali ya vitu au hali maalum kama vile wanyama, giza, au urefu.
- Wasiwasi wa Jamii: Hofu ya kukataliwa au kuhukumiwa (judged) na wengine katika hali za kijamii.
- Wasiwasi wa Jumla: Wasiwasi wa mara kwa mara kuhusu mambo mbalimbali.
- Mashambulizi ya Hofu: (panic attack) Vipindi vifupi vya hofu kali na dalili za kimwili kama vile kupumua kwa kasi na kutetemeka.
Njia za Kukabiliana na Wasiwasi kwa Watoto
Kuna njia nyingi za kukabiliana na wasiwasi kwa watoto, na matibabu bora itategemea sababu na ukali wa tatizo. Baadhi ya njia za kawaida ni pamoja na:
- Cognitive behaviour therapy: Hii ni aina ya tiba inayomfundisha mtoto jinsi ya kutambua na kubadilisha mawazo na tabia zinazosababisha wasiwasi.
- Dawa: Katika baadhi ya hali, dawa zinaweza kutumika pamoja na tiba ili kudhibiti dalili za wasiwasi.
- Msaada wa Familia: Wazazi na walezi wana jukumu muhimu katika kusaidia mtoto kukabiliana na wasiwasi kwa kujenga mazingira ya usalama na upendo.
- Mabadiliko ya Maisha: Mabadiliko katika mtindo wa maisha (lifestyle), kama vile kulala vya kutosha, kula chakula chenye afya, na kufanya mazoezi ya kawaida, yanaweza kusaidia kupunguza wasiwasi.
Hitimisho:
Ni muhimu kutambua kwamba wasiwasi kwa watoto ni tatizo linaloweza kutibiwa. Ikiwa unashuku kuwa mtoto wako ana tatizo la wasiwasi, ni muhimu kumpeleka kwa mtaalamu wa afya ya akili kwa uchunguzi na matibabu.
Utangulizi:
Umewahi kujiuliza kwa nini mara nyingine watoto wachanga hufa ghafla bila sababu za kueleweka? Jibu la swali hili lipo katika uelewa wa janga la sudden infant death syndrome (SIDS).
SIDS ni kifo cha ghafla cha mtoto mchanga mara nyingi chini ya mwaka mmoja na mwenye kuonekana na afya njema ambacho hakina sababu za kueleweka hata baada ya uchunguzi wa kina wa kitabibu. Vifo hivi vimekuwa chanzo cha majonzi kwa wazazi wengi, na bado havijapata tiba kamili.
SIDS HUSABABISHWA NA NINI?
Ingawa sababu halisi za SIDS hazijulikani kabisa, kuna baadhi ya mambo ambayo yanaweza kuongeza hatari ya kutokea kwake:
-
Unywaji wa Pombe na Uvutaji Sigara: Wazazi wanaotumia pombe au sigara wanaongeza hatari kwa mtoto wao.
-
Kulala Kifudifudi: Kumlaza mtoto kifudifudi kabla hajawa na uwezo wa kujigeuza mwenyewe kunaongeza hatari ya SIDS. Ni vyema mtoto alazwe chali chali au awe na muda maalumu wa kulala kifudifudi wenye uangalizi maalumu (supervised tummy time).
-
Unyonyeshaji: Kuna njia sahihi ambazo zinatakiwa kufuatwa ili kuzuia mtoto kupaliwa au kuziba njia ya hewa.
-
Mazingira ya Kulala: Mahali anapolala mtoto panapaswa pawe tambarare (flat surface) pagumu (sio godoro la kubonyea), panapaswa kuwa salama bila vitu vingi kama vile mito, midoli au blanketi nyingi. Pia ni hatari kwa mzazi/mlezi kulala kitanda kimoja na mtoto mchanga!!
-
Matatizo ya Afya ya Mtoto: Baadhi ya matatizo ya afya ya mtoto, kama vile matatizo ya kupumua au matatizo ya moyo, ubongo na viungo vingine yanaweza kuongeza hatari ya SIDS.
Kuzuia SIDS
Ingawa hakuna njia ya kuzuia kabisa SIDS, kuna hatua ambazo wazazi wanaweza kuchukua ili kupunguza hadhari:
- Kulala Mtoto Chali: Siku zote mlaze mtoto wako chali.
- Epuka Vitu Vingine Vitandani: Epuka kuweka vitu vingi kama mito, blanketi, au vitu vya kuchezea kitandani.
- Unyonyeshaji: Nyonyesha mtoto wako kwa muda mrefu iwezekanavyo kwa kutumia njia salama.
- Mazingira ya Kulala: Hakikisha chumba cha kulala cha mtoto ni chenye joto la wastani na mzunguko mzuri wa hewa.
- Usiweke Mtoto Katika Kitanda cha Wazazi: Epuka kulala na mtoto kitandani.
- Mahudhurio mazuri ya Kliniki: Wazazi wanapaswa kuhakikisha kuwa mama na mtoto wanahudhuria kliniki kila appointment bila kukosa. Hii itasaidia kuzuia matatizo ya afya ya mtoto ambayo yanaweza kuongeza hatari ya SIDS.
Umuhimu na Uchunguzi wa Kitaalamu
Ikiwa mtoto wako atafariki ghafla, ni muhimu sana kufanya uchunguzi wa kina wa kitabibu ili kubaini sababu halisi ya kifo. Hii itasaidia kuzuia matukio kama haya katika siku za baadaye.
Hitimisho:
Kwa kuzingatia hatua za kuzuia SIDS, tunaweza kupunguza idadi ya vifo vya watoto wachanga na kuhakikisha kwamba kila mtoto ana nafasi ya kuishi maisha yenye afya na furaha.
References:
- World Health Organization. (2023). Sudden infant death syndrome. https://platform.who.int/mortality/themes/theme-details/topics/topic-details/MDB/sudden-infant-death-syndrome
- American Academy of Pediatrics. (2023). Reducing the Risk of Sudden Infant Death Syndrome (SIDS). https://www.aap.org/en/patient-care/safe-sleep/
Note: Kwa maelezo zaidi na ushauri, wasiliana na daktari wa watoto.
SHAKEN BABY SYNDROME (SBS) NI NINI?
Utangulizi:
Umewahi kuwaza kwamba unaweza kumpoteza mwanao mchanga kwasababu ya kumtikisa?
Shaken Baby Syndrome (SBS), au "sindromu ya watoto kutikiswa," ni hali ambayo inajielezea kwenye jina lake. Hali hii hutokea pale mtoto mchanga anapotikiswa kwa nguvu na kusababisha athari katika ubongo wa mtoto, na inaweza kusababisha madhara makubwa katika kimwili na afya afya kwa ujumla.
SBS ni sababu kubwa zaidi ya kifo/ athari ya ubongo inayosababishwa na unyanyasaji wa watoto.
Kwa jumla 95% ya watoto wachanga walio na jeraha kubwa la kichwani wametikiswa. Asilimia inayobaki husababishwa zaidi na majeraha makubwa ya kichwa kama vile ajali za magari.(Blumenthal, 2002)
Ni Kitu gani hupelekea mtoto kutikiswa?
SBS mara nyingi hutokea kutokana na hasira au kukata tamaa kwa mzazi au mlezi, hasa wakati mtoto analia kwa muda mrefu. Wakati mwingine ni unyanyasaji wa mtoto(child abuse) kutoka kwa mlezi hupelekea hadi mtoto kutikiswa. Wakati mwingine ni kutokujua kwa mlezi na akafanya shughuli ya mtikisiko kama kurukaruka huku akiwa amembeba mtoto mchanga.
Nini hutokea baada ya mtoto kutikiswa?
- Kutikiswa kwa nguvu kunaweza kusababisha ubongo wa mtoto kugonga ndani ya fuvu lake, na hivyo kusababisha uharibifu mkubwa wa seli za ubongo.
- Mishipa ya damu midogomidogo huweza kupasuka na kusababisha kuvuja damu ndani ya ubongo.
- Mabonge makubwa ya damu yanaweza kutengenezwa na kugandamiza ubongo na kusababisha kuvimba.
- Misuli ya shingo ya mtoto mchanga haijakomaa hivyo haina nguvu ya kulinda mifupa inayozunguka uti wa mgongo ili isikandamize uti wa mgongo.
- Majeraha yanayotokana na mtikisiko huu wa ubongo yanaweza kusababisha ulemavu wa akili,kupooza, upofu, uziwi na hata kifo.
Dalili za SBS
Dalili za sbs zina wigo mpana na zinaweza kua dalili ndogo zisizo na kiashiria dhahiri cha jeraha la ubongo au zinaweza kua dalili kubwa na mbaya zaidi.
a)Dalili za SBS zinaweza kujitokeza papo kwa hapo au zikatokea baada ya muda.
- Baadhi ya dalili zisizo na kiashiria dhahiri cha jeraha la ubongo ni kama:
- Mtoto anaweza kuwa na shida ya kulala,
- Kutapika mara kwa mara
- kushindwa kula.
- Uchovu na kulegea
- Kuwa na usingizi wa kupita kiasi: Mtoto anaweza kuwa na usingizi mwingi zaidi ya kawaida.
- Mabadiliko ya tabia: Hali kama vile kukasirika bila sababu au kuwa mpweke.
- Kukosa uchangamfu
b)Dalili kubwa zinazoweza kuashiria athari kwenye ubongo na uti wa mgongo:
- Degedege (seizure)
- Kushindwa kupumua
- Kupooza (paralysis)
- Kupoteza fahamu (coma)
Athari za kudumu
Madhara ya SBS yanaweza kuwa makubwa na ya kudumu. Mfano wa madhara haya ni kama:
- Ulemavu wa akili (intellectual disability)
- Changamoto na uzito katika kujifunza (learning difficulties)
- Matatizo ya mihemko (emotional problems)
- Kichwa kujaa maji (hydrocephalus)
Kinga na Elimu
Ni muhimu kutoa elimu kwa wazazi na walezi kuhusu madhara ya SBS. Mifano ya njia za kuzuia ni pamoja na:
- Kujifunza njia bora za kushughulikia hasira na msongo wa mawazo.
- Kutafuta msaada wa kitaalamu wakati wa hali ngumu, msongo wa mawazo, ugonjwa wa akili na sonona wakati wa kujifungua. (post-partum psychosis and post-partum depression)
- Wenza na ndugu kumsaidia mzazi mpya kulea na Kuelewa kuwa mtoto anahitaji upendo na uvumilivu.
Hitimisho
Shaken Baby Syndrome ni tatizo kubwa linalohitaji umakini na elimu ya kina. Kwa kuwajulisha wazazi na jamii, tunaweza kusaidia kuzuia hali hii na kulinda watoto wetu. Kila mtoto anastahili kuwa na mazingira salama na yenye upendo.
Marejeo
- Medscape
- I Blumenthal, Shaken baby syndrome, Postgraduate Medical Journal, Volume 78, Issue 926, December 2002, Pages 732–735, https://doi.org/10.1136/pmj.78.926.732
Utangulizi:
Kuna hatua muhimu katika ukuaji na maendeleo ya watoto zinazoitwa developmental milestones) ingawa kila mtoto ni tofauti na maendeleo yanaweza kutofautiana, kuna hatua tunazotarajia kuona mtoto anapofikia umri fulani ili kuthibitisha kuwa makuzi yake yanaendelea vizuri. Tutajadili sababu, athari, na hatua zinazoweza kuchukuliwa. Mfano wa milestones hizi ni:
Miezi 3:Mtoto awe anaweza kutabasamu na kukaza shingo.
Mpaka miezi 6:Mtoto awe na uwezo wa kugeuza kichwa kufuata sauti, kujigeuza, kukaa mwenyewe, kushika vitu, na kutambua watu wa karibu.
Mwaka 1-2 :Mtoto awe anaweza kutembea bila msaada, kuunda sentensi fupi, na kuelewa maelezo mepesi.
Sababu za Kuchelewa kwa Milestones
- Kuzaliwa kabla ya wakati (prematurity).
- Jeraha wakati wa kuzaliwa (birth injuries).
- Ulemavu wa ubongo unaosababishwa na upungufu wa oksijeni wakati wa leba au uzazi (hypoxic-ischemic encephalopathy).
- Matatizo ya kigenetiki kama Down Syndrome au dystrophy ya misuli.
- Matatizo ya kimetaboliki, mfano phenylketonuria (PKU).
- Majeraha kwenye ubongo wakati au baada ya kuzaliwa.
- Uwepo wa sumu kama vile pombe au madini ya lead katika mwili wa mtoto.
- Maambukizi ya magonjwa kwa mama wakati wa ujauzito (mfano, magonjwa ya zinaa).
- Magonjwa sugu kama vile magonjwa ya moyo, sickle cell, au saratani.
- Utapiamlo (malnutrition).
Mambo Mengine Yanayoweza Kuchangia
- Mazingira duni nyumbani, mfano unyanyasaji wa kimwili na kihisia. Mtoto anayeishi kwenye mazingira yasiyo salama anaweza kuchelewa kufikia milestones.
Athari za Kuchelewa
- Kujifunza na masomo: Watoto wanaochelewa milestones wanaweza kukumbana na changamoto shuleni.
- Kuhusiana na wenzake: Kuchelewa kunaweza kuathiri uwezo wa mtoto kuunda na kudumisha urafiki.
- Afya ya kihisia: Watoto wanaweza kujisikia tofauti na wenzao, na hii inaweza kuleta changamoto za kihisia kama huzuni au wasiwasi.
Hatua za Kuchukua
- Tafuta msaada wa kitaalamu: Endapo kuna wasiwasi juu ya maendeleo ya mtoto, ni muhimu kumwona daktari wa watoto kwa uchunguzi na tiba kama vile mazoezi ya kuongea (speech therapy), mazoezi ya viungo (physiotherapy), na occupational therapy.
- Tengeneza mazingira rafiki kwa mtoto: Mazingira ya nyumbani yenye michezo na vitabu vinaweza kusaidia ukuaji wa mtoto, na kufuatilia ikiwa kuna unyanyasaji wowote.
- Kuwa mvumilivu na kujitoa: Wazazi wanapaswa kutenga muda wa kutosha kwa ajili ya watoto wao, kuwasaidia katika shughuli za kijamii na kiakili, na kushirikiana na watoa huduma za afya.
Hitimisho
Kuchelewa kwa milestones za watoto inaweza kuwa jambo la kawaida kwa baadhi ya watoto, kwani kila mmoja ana safari yake ya ukuaji. Hata hivyo, linaweza pia kuwa kiashiria cha tatizo kubwa zaidi. Ni muhimu kutambua dalili za kuchelewa na kuchukua hatua mapema. Kwa msaada sahihi, watoto wanaweza kurudi kwenye hali ya kawaida au kupatiwa matibabu yanayoweza kurahisisha maisha yao.
Kipindi cha ujauzito ni wakati muhimu sana kwa afya ya mama na mtoto. Ili kuhakikisha mama anajifungua salama na mtoto anazaliwa akiwa na afyanjema, ni muhimu kuhudhuria kliniki mara kwa mara kama inavyoshauriwa na Watoa huduma. Kampeni nyingi zimeanzishwa ili kuhamasisha akina mama wajawazito wanaanza kuhudhuria kliniki mapema, pia kwenye App kama TanzMED kuna feature maalumu ambayo inakuongoza na kukukumbusha kuhudhuria kliniki, lakini je, unajua kwa umuhimu wa kuhudhuria kliniki ya ujauito?
Kuzuia Matatizo ya Afya kwa Mama na Mtoto Aliye Tumboni
Wakati wa kliniki, mama mjamzito hupatiwa dawa, vipimo na chanjo mbalimbali ambazo husaidia kumlinda yeye na mtoto wake kutokana na magonjwa hatari. Baadhi ya dawa hizi ni:
A: Dawa za Kuongeza Damu (FEFO)
Dawa za kuongeza damu ni muhimu sana kwa mama mjamzito. Fefo ina madini ya chuma na folic acid ambayo husaidia kuzuia upungufu wa damu unaosababishwa na matumizi ya ziada wakati wa ujauzito. Madini ya chuma humlinda mama dhidi ya upungufu wa damu, na folic acid husaidia ukuaji wa mtoto, hasa katika wiki za mwanzoni, kabla ya kuunda uti wa mgongo na mfumo wa mishipa ya fahamu. Matumizi ya folic acid pia yanasaidia kuzuia kasoro kama mgongo wazi na tatizo la kichwa kikubwa. Unzaweza kusoma kuhusu vichwa vikubwa hapa Fahamu ukweli, hatari na matibabu ya Vichwa vikubwa
FIG 1: Mtoto mwenye kichwa kikubwa FIG 2: Mtoto mwenye mgongo wazi
B: Dawa za Kuzuia Malaria
Malaria ni hatari sana kwa mama mjamzito kwani vimelea vya malaria vinaweza kuathiri kondo la nyuma na kusababisha matatizo makubwa kwa mtoto na mama, ikiwemo kifo. Mama wajawazito hupewa dawa za kuzuia malaria pamoja na vyandarua vilivyowekwa dawa.
C: Dawa za Minyoo
Minyoo inaweza kudhoofisha hali ya afya ya mama kwa kunyonya virutubisho muhimu vinavyotakiwa kwa ukuaji wa mtoto. Pia, minyoo inaweza kusababisha upungufu wa damu, hivyo ni muhimu kwa mama wajawazito kupatiwa dawa za kuzuia minyoo.
D: Chanjo ya Tetenasi
Mama wajawazito pia hupewa chanjo ya tetenasi ambayo husaidia kumkinga dhidi ya ugonjwa huo hatari ambao unaweza kuathiri afya ya mama na mtoto wakati wa kujifungua.
Kutambua Magonjwa ya Mama na Mtoto Mapema
Mahudhurio ya kliniki pia husaidia kugundua matatizo au magonjwa ambayo mama anaweza kuwa nayo kabla au wakati wa ujauzito. Magonjwa kama vile shinikizo la damu, kisukari, upungufu wa damu, magonjwa ya zinaa, na virusi vya ukimwi vinaweza kuathiri mama na mtoto. Kwa kugundua matatizo haya mapema, mama anaweza kupatiwa matibabu sahihi ili kuepusha athari mbaya kwa mtoto kama vile ulemavu wa akili, kifafa cha mimba, au kifo.
Elimu ya Afya na Ujauzito
Kliniki hutoa nafasi kwa mama mjamzito (na wenza wao) kupata elimu kuhusu jinsi ya kutunza ujauzito. Elimu hii inahusisha lishe bora, tabia hatarishi zinazopaswa kuepukwa, na dalili za hatari zinazohitaji matibabu ya haraka. Kupata elimu hii ni muhimu ili kuhakikisha mama anajua namna ya kujilinda yeye na mtoto wake wakati wote wa ujauzito.
Kujua Maendeleo ya Ujauzito
Kupitia mahudhurio ya kliniki, mama anaweza kufuatilia maendeleo ya mtoto aliye tumboni. Hii inahusisha mambo kama kubaini umri wa ujauzito, kutambua kama mimba ipo katika nafasi sahihi (ili kugundua mimba zilizotunga nje ya mji wa mimba), kuangalia kiasi cha maji ya uzazi, na kuchunguza jinsi mtoto alivyolala ili kupanga njia sahihi ya kujifungua.
Elimu ya Uzazi wa Mpango
Baada ya kujifungua, ni muhimu kwa mama kufahamu mbinu za uzazi wa mpango ili kuhakikisha mwili wake unapata muda wa kupona vizuri kabla ya kupata ujauzito mwingine. Hii inasaidia kulinda afya ya mama na mtoto wake ajaye.
Hitimisho
Mwanamke anatakiwa kuanza mahudurio ya kliniki hata kabla hajabeba ujauzito. Lakini hata kama ukigundua tayari umeshabeba ujauzito ni muhimu kunza mahudhurio ya kliniki mapema. Jilinde na umlinde mwanao kwa kuhakikisha unahudhuria kliniki kila mwezi mara tu baada ya kujua umebebe ujauzito!! Pia, unaweza kutumia App ya TanzMED kufuatilia ujauzito wako.
Kuelewa ADHD kwa Watoto: Mwongozo kwa Wazazi
Kulea mtoto ni safari iliyojaa furaha, changamoto, na kujifunza. Hata hivyo, ikiwa mtoto wako anaonekana kupambana zaidi katika kuzingatia, kubaki tuli,kuwa makini au kutenda kwa haraka bila kufikiri, hii inaweza kuwa ishara ya Upungufu wa Makini na kutozingatia Kutokana na Utendaji wa Kupita Kiasi, maarufu kama Attention Deficit Hyperactivity Disorder (ADHD).
Kwa watoto wenye ADHD, kubaki tuli, na kutenda kasi ni mara kwa mara na kali zaidi, ikiwaathiri shuleni, katika kupata na kutunza marafiki. Kuelewa ADHD na kujua jinsi ya kuitambua kunaweza kumsaidia mtoto wako kuishi maisha ya furaha na yenye kuridhisha.
ADHD si nadra. Utafiti unaonyesha kwamba inathiri karibu 9.4% ya watoto nchini Marekani. Ingawa data mahususi kuhusu Tanzania hazijaainishwa bado , ni wazi kwamba watoto wa Tanzania pia wanakabiliwa na hali hii. Wavulana wana uwezekano mkubwa zaidi wa kupata utambuzi wa ADHD kuliko wasichana, lakini inaweza kuathiri jinsia zote mbili.
Dalili za ADHD
Dalili za ADHD zimegawanyika katika makundi matatu: kutozingatia, kuongezeka kwa shughuli, na msukumo. Hapa ni jinsi dalili hizi zinaweza kuonekana kwa mtoto wako:
- Kutozingatia: (in attention)
- Ugumu wa kuzingatia kazi au kufuata maelekezo (lack of attention and following instructions )
- Mara nyingi yuko mbali kifikira
- Mara nyingi husahau vitu na kupoteza vitu muhimu
- Hupambana katika kuwa na mpangilio mzuri wa kazi na shughuli (poor organisation skills)
- Kuongezeka kwa shughuli: (hyperactivity)
- Daima huwa katika mwendo, kana kwamba "wanaendeshwa na injini" (hyperActivity)
- Ana shida kubaki ameketi na mara nyingi huwa na wasiwasi
- Anazungumza kupita kiasi na ana shida kucheza kimya kimya
- Msukumo: (impulsitivity)
- Anatenda bila kufikiria, kama vile kukatiza barabarani bila kuweka umakini
- Anakatiza wengine wakati wa mazungumzo au michezo
- Ana shida kusubiri zamu yake na anaweza kutoa majibu kwa msukumo
Aina za ADHD
Watoto wenye ADHD wanaweza kuwa na moja ya aina tatu:
- Aina ya Kutozingatia: (inattentive type ) Watoto hawa hupambana zaidi katika kuzingatia.
- Aina ya Kuongezeka kwa Shughuli/Msukumo: (Hyperactive and Impulsive type) : wana shughuli nyingi kwa wakati mmoja wakitenda mambo kwa haraka haraka bila kufikiri kabla ya kutenda ila hutulia wanapoamua kwenye shughuli wanayoipenda zaidi.
- Aina ya Kuchanganya: (combined type) : Hii ndiyo aina ya kawaida zaidi, ambapo watoto wana dalili zilitajwa kwenye aina zote mbili hapo awali.
Unapaswa kufanya nini ikiwa unashuku mtoto wako ana ADHD?
Ikiwa mtoto wako anaonyesha dalili hizi mara kwa mara kwa zaidi ya miezi sita, inaweza kuwa wakati wa kuzungumza na mtaalamu wa afya, kama vile daktari wa watoto. Huko Tanzania, hii inaweza kuwa daktari wako wa karibu au mtaalamu wa afya ya mtoto. Ni muhimu kukumbuka kwamba watoto wengi wanaweza kuonyesha tabia zinazofanana kutokana na mkazo, kuchoka, au kupitia kipindi kigumu cha maisha. Hata hivyo, ikiwa tabia hizi zinaendelea, kutafuta msaada ni muhimu.
Kwa nini kuwatambua na kuwasaidia mapema ni muhimu?
Bila usimamizi sahihi, ADHD inaweza kusababisha changamoto za muda mrefu, ikiwa ni pamoja na utendaji mbaya shuleni, matatizo katika mahusiano, na ugumu katika kudumisha kazi baadaye katika maisha. Aidha, inaweza kuchangia kujiamini kuwa chini, matatizo ya kulala, na hata matumizi mabaya ya vitu dawa na kileo. Lakini kwa msaada sahihi, watoto wenye ADHD wanaweza kustawi.
Tiba mara nyingi inajumuisha mchanganyiko wa tiba ya tabia (Behavioral Therapy), msaada wa elimu, na wakati mwingine dawa. Utambuzi wa mapema na uingiliaji (early identification and intervention) huongeza sana uwezekano wa matokeo mazuri.
Wazazi Wanaweza Kusaidiaje?
Kama mzazi, unacheza jukumu muhimu katika kudhibiti ADHD ya mtoto wako. Hapa kuna hatua ambazo unaweza kuchukua:
Uelewa wa kina: Jifunze kuhusu ADHD ili uweze kuelewa vizuri changamoto ambazo mtoto wako anakabiliana nazo kihususa
Mazingira yenye utulivu: Tengeneza mazingira ya nyumbani yenye utulivu
Ratiba thabiti: Fuata ratiba ya kila siku ili kuwasaidia watoto kutabiri kile kinachofuata na kupunguza wasiwasi
Matokeo chanya: Zingatia na kusherehekea mafanikio madogo madogo ya mtoto wako ili kuongeza kujiamini kwake.
Ushirikiano na mwalimu: Shirikiana na walimu wa mtoto wako ili kuhakikisha kuwa anapokea msaada anaohitaji shuleni.
Utunzaji wa afya: Hakikisha mtoto wako anapata lishe bora, mazoezi ya kutosha, na usingizi wa kutosha.
Tafuta msaada wa kitaalamu: Usisite kutafuta msaada kutoka kwa wataalamu kama vile mwanasaikolojia wa watoto au mtaalamu wa tabia.
Ujumbe wa mwisho:
Kumbuka, ADHD sio udhaifu, bali ni tofauti katika jinsi ubongo unavyofanya kazi. Kwa msaada sahihi na upendo , watoto wenye ADHD wanaweza kufanikiwa katika maisha. Kila mtoto ni wa kipekee, na hakuna njia moja inayofaa kwa wote. Usisite kuuliza maswali, kutafuta msaada, na kujenga mtandao wa usaidizi ambao utawasaidia wewe na mtoto wako.
Utangulizi:
Labda umekua ukijiuliza kwanini mwanamke hatakiwi kunywa pombe wakati wa ujauzito, na je pombe kiasi gani inaleta madhara kwa mtoto ambaye yuko tumboni. Madhara hayo kama yapo ni yapi?
Katika makala hii tutaenda kujifunza kuhusu FASD (fetal alcohol spectrum disorder)na FAS (fetal alcohol syndrome) dalili zake , madhara yake na matibabu. Lakini pia tutajibu swali lililo hamasisha makala hii.
FASD
FASD ni wigo mpana wa dalili zinzoweza kumuathiri mtoto aliye tumboni baada ya mama kutumia pombe wakati wa ujauzito, Wigo huu huanzia dalili ndogo ndogo hadi dalili kubwa zaidi. Dalili kubwa zaidi ndio hujulikana kama FAS ( Ugonjwa wa pombe kwa mtoto aliye tumboni).
Pombe ni teratojeni inayojulikana wazi na inaweza kusababisha madhara makubwa kwa maendeleo ya mtoto pindi akiwa tumboni, ambayo yanaweza kudumu maisha yote.
FASD ni moja ya sababu kuu ya ulemavu wa akili ambao hauhusiani na urithi wa kijenetiki.
Epidemolojia
“Uchambuzi wa hivi karibuni wa meta ulithamini kwamba kiwango cha ulimwengu cha Ugonjwa wa Pombe kwa Watoto (FASD) katika idadi ya watoto na vijana (miaka 0–16.4) ni 7.7 kwa kila watoto 1000” (Symons and Pedruzzi #).
“Hatari ya mama kuzaa mtoto mwenye FASD ina visababishi vingi”. Hii inamaanisha kwamba hatari anazoweza kukabiliana nazo mama wakati wa ujauzito zinaweza kuwa za aina nyingi na zinaweza kuathiriwa na mambo tofauti. (May & Gossage, 2011, #)
Dalili za FASD
Kasoro za Kimwili
Kasoro za kimwili zinaweza kujumuisha:
- Sifa za uso wa kipekee kama kuwa na macho madogo, mdomo wa juu mwembamba sana, pua ndogo inayopanda juu na ngozi laini isiyokua na mikunjo kati ya pua na mdomo wa juu,masikio yaliyo shuka chini.
- Ukuaji wa mwili wa duni wakati wa ujauzito na baada ya kuzaliwa.(kuchelewa kukaza shingo, kukaa, kutambaa, kusimama, kuongea n.k)
- Maumbile yasiyo ya kawaida kwenye mikono na vidole.
- Matatizo ya kuona na kusikia.
- Kichwa kidogo na/au ubongo mdogo.
- Kasoro za moyo na matatizo ya mifupa na figo
Matatizo ya Ubongo na Mishipa ya fahamu
Matatizo ya ubongo na mishipa ya fahamu yanaweza kujumuisha:
- Ukosefu uratibu (co-ordination)
- Kumbukumbu duni
- Matatizo ya kutulia na kuchakata taarifa
- Ulemavu wa akili na kuchelewa kwa maendeleo ya ukuaji
- Ulemavu wa kujifunza
- Kutoweza kuelewa matokeo ya vitendo
- Hoja duni na kushindwa kutatua matatizo
Matatizo ya Tabia
Matatizo ya katika kufanya kazi na kuwasiliana na wengine yanaweza kujumuisha:
- Ujuzi duni wa kujichanganya katika jamii (poor social skills)
- Ugumu wa kuungana au kujumuika na wenzao
- Kushindwa kuzoea mabadiliko
- Ugumu wa kuzingatia majukumu
Madhara ya FASD
- Ulemavu wa kujifunza na matatizo ya akili.
- Matatizo ya kitabia na kijamii.
- Matatizo ya afya ya akili kama vile wasiwasi na unyogovu.
- Matatizo ya mwili, kama vile kasoro za moyo, matatizo ya kusikia na kuona.
Je, kiwango gani cha pombe ni hatarishi kwa mtoto alieko tumboni?
Hakuna kiwango cha pombe kinachojulikana kuwa ni salama kwa mama mjamzito. Hivyo basi, Inashauriwa kwamba wanawake wajawazito wasitumie pombe kabisa ili kuepuka hatari ya matatizo kama Ugonjwa wa Pombe kwa mtoto alieko tumboni (FASD).
Ili kuwa salama jua kwamba viwango vyote vya pombe ni hatarishi kwa mama mjamzito na mtoto aliye tumboni.
Utambuzi na Matibabu
Utambuzi:
Wakati bora wa kugundua Ugonjwa wa Pombe kwa watoto walio tumboni (FAS) au FASD ni wakati wa kuzaliwa, lakini kesi nyingi hazigunduliwi hadi umri wa mtoto kuanza shule. Uchelewaji huu unasababishwa hasa na wataalamu wa afya kushindwa kukusanya taarifa za matumizi ya pombe kwa mama wakati wa ujauzito kama inavyotakiwa kwasababu ya kukosekana utayari wa mama mjamzito kukubali au kusema kama alikuwa anatumia pombe wakati wa ujauzito. Hii hufanya utambuzi kuwa mgumu kipindi mtoto akiwa mchanga.
Zaidi ya hayo, sifa za kipekee za uso zinaweza zisionekane wazi awali ila zikawa dhahiri kadri mtoto anavyoendelea kukua na kufikia ujana.
Matibabu:
Ingawa hakuna tiba ya FASD na FAS, kuna matibabu yanayoweza kufanyika kusaidia kuboresha maisha ya walioathirika. Matibabu yanaweza kujumlisha:
- Elimu maalum na msaada wa kujifunza.
- Tiba ya usemi na lugha. (speech therapy)
- Tiba ya mwili na kazi. (physiotherapy and occupational therapy)
- Huduma za afya ya akili na ushauri.
Hitimisho
FASD na FAS inaweza kuzuilika kabisa kwa kuepuka pombe wakati wa ujauzito!!
Ni muhimu kwa wanawake kuelewa hatari za matumizi ya pombe wakati wa ujauzito na kutafuta msaada wa matibabu ikiwa wanajikuta wakiwa na shida ya kuacha pombe wakati wa kujaribu kupata mtoto au wakati wa ujauzito.
Marejeleo
- Medscape
- Journals
- May PA, Gossage JP. Maternal risk factors for fetal alcohol spectrum disorders: not as simple as it might seem. Alcohol Res Health. 2011;34(1):15-26. PMID: 23580036; PMCID: PMC3860552.
- Symons, M., Pedruzzi, R.A., Bruce, K. et al. A systematic review of prevention interventions to reduce prenatal alcohol exposure and fetal alcohol spectrum disorder in indigenous communities. BMC Public Health 18, 1227 (2018). https://doi.org/10.1186/s12889-018-6139-5